2012-10-30 10:45:01

Uhusiano wa Kidiplomasia kati ya Vatican na Croatia unafumbata utajiri wa kijiografia, kihistoria na kidini


Askofu mkuu Dominique Mamberti, Katibu mkuu wa Mambo ya nje na ushirikiano wa kimataifa mjini Vatican, katika maadhimisho ya miaka ishirini tangu Croatia ilipoanzisha uhusiano wa kidiplomasia, hapo tarehe 29 Oktoba, 2012 amegusia kwa namna ya pekee, utajiri wa kijiografia, kihistoria na kidini unaofumbatwa katika mahusiano ya kidiplomasia kati ya Vatican na Croatia.

Katika historia ya nchi ya Croatia, daima imejitahidi kuonesha uaminifu kwa Injili ya Kristo na Khalifa wa Mtakatifu Petro, kama Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, alivyobainisha wakati wa hija yake ya kichungaji nchini Croatia, kunako mwaka 2011.

Hili ni taifa ambalo limechangia kwa kina na mapana katika kulinda na kudumisha tunu msingi za maisha ya kiroho, kiutu na kimaadili sanjari na kutoa utambulisho kwa watoto wake. Ilikuwa ni tarehe 13 Januari 1992 Croatia ilipotambuliwa na Vatican kuwa ni taifa huru na tangu wakati huo, mchakato wa uhusiano wa kidiplomasia baina ya pande hizi mbili ukaanza katika njanja za: kisheria, elimu, utamaduni, huduma za kiroho kwa vikosi vya ulinzi na usalama pamoja na uchumi.

Askofu mkuu Mamberti anasema kwamba, kumekuwepo na maendeleo makubwa katika kudumisha uhusiano wa kidiplomasia kati ya Vatican na Croatia; hasa kwa kukuza majadiliano kati ya viongozi wa Kanisa na Serikali pamoja na Croatia kuendelea kuchangia katika ustawi na maendeleo ya Jumuiya ya Kimataifa.

Amewashukuru viongozi mbali mbli wa Kanisa na Serikali walioendelea kuboresha uhusiano huu wa kidiplomasia katika kipindi cha miaka ishirini iliyopita, jambo ambalo limepanua na kuendeleza majadiliano na ushirikiano, huduma pamoja na kusimama kidete kulinda, kutetea haki msingi za binadamu, utu na heshima ya binadamu; daima wakitafuta mafao ya wengi pamoja na kuendeleza tunu msingi za maisha ya kiroho na kimaadili.







All the contents on this site are copyrighted ©.