Kardinali Pengo: Maadhimisho ya Sinodi ya Uinjilishaji Mpya kimekuwa ni kipindi cha:
Sala, Tafakari na Uinjilishaji
Mababa wa Sinodi ya Maaskofu juu ya Uinjilishaji Mpya katika Ujumbe wao kwa Watu wa
Mungu sehemu ya mwisho, wanaangalia utume na maisha ya Kanisa katika sehemu mbali
mbali za dunia na kuwapatia neno la matumaini kwa ajili ya sehemu husika.
Wanawatia
moyo Waamini kutoka Makanisa ya Mashariki ili waweze kutangaza Injili ya Kristo katika
mazingira ya amani na uhuru wa kuabudu; kwa Kanisa Barani Afrika, wanawaalika kukoleza
moyo na ari ya Uinjilishaji kwa njia ya utamadunisho ili imani iweze kuzama na kuota
mizizi katika maisha ya waamini.
Mababa wa Sinodi katika Ujumbe wao wanazichangamotisha
Serikali mbali mbali Barani Afrika kuzingatia misingi ya utawala bora, sheria, uhuru
wa kuabudu, ili kuondokana na kinzani na vurugu za kidini, kisiasa na kikabila. Wakristo
wanaoishi Amerika ya Kaskazini wanahimizwa kuiishi imani yao katika ulimwengu ambao
watu wengi wamekengeuka na kuzama zaidi katika malimwengu; wajitahidi kutubu na kuongoka;
waoneshe moyo wa ukarimu kwa wageni na wahamiaji.
Wakristo huko Amerika ya
Kusini wanahimizwa na Mababa wa Sinodi katika ujumbe wao kuendeleza utume wa Kanisa
kama sehemu ya mchakato wa kupambana na baa la umaskini na ongezeko la madhehebu na
dini katika maeneo yao. Wakristo Barani Asia hata katika udogo wao kwa idadi wanaendelea
kuhimizwa kuimaarisha imani yao kwa Kristo na Kanisa lake.
Mababa wa Sinodi
wanawaangalisha Waamini Barani Ulaya kuwa makini zaidi ili wasimezwe na malimwengu,
daima wawe mstari wa mbele kulinda na kutetea utu na heshima ya binadamu, wawe tayari
kutafuta mafao ya wengi ndani ya Jamii. Matatizo na magumu wanayokabiliana nayo iwe
ni changamoto ya kukuza na kuimarisha Imani yao kwa Kristo na Kanisa lake. Wakristo
huko Oceania wanaalikwa kwa namna ya pekee, kushiriki katika mchakato mzima wa Uinjilishaji
Mpya.
Kardinali Polycarp Pengo, Rais wa Shirikisho la Mabaraza ya Maaskofu
Katoliki Afrika na Madagascar, SECAM katika mahojiano na Idhaa ya Kiswahili ya Radio
Vatican anabainisha kwamba, Maadhimisho ya Sinodi ya Maaskofu juu ya Uinjilishaji
Mpya kama njia ya kutangaza Imani ya Kikristo, yamekuwa ni muda muafaka wa kusali,
kutafakari na kushirikishana mang’amuzi mbali mbali katika maisha na utume wa Kanisa.
Kimekuwa
ni kipindi cha neema, toba na wongofu wa ndani, kwani Mababa wa Sinodi wamepata nafasi
ya kuweza kupembua kwa kina na mapana kuhusu: matatizo, changamoto na fursa mbali
mbali ambazo zimejitokeza mintarafu azma ya Uinjilishaji Mpya unaogusa undani wa maisha
na utume wa Kanisa katika Ulimwengu mamboleo.
Dhana ya Uinjilishaji Mpya inapania
kwa namna ya pekee kabisa, kutangaza Imani ya Kristo na Kanisa lake kwa ari, nguvu
na ujasiri mkubwa zaidi, daima wakiendelea kusoma alama za nyakati, changamoto iliyotolewa
na Mababa wa Mtaguso Mkuu wa Pili wa Vatican, yapata miaka hamsini iliyopita, lakini
ujumbe wake bado ni hai kabisa katika maisha na utume wa Kanisa katika ulimwengu mamboleo.
Vita,
kinzani na migogoro ya kidini, kisiasa na kijamii ni matunda ya ubinafsi, tamaa ya
mali na madaraka; uvunjaji wa haki msingi za binadamu, uhuru wa kuabudu pamoja na
kutomheshimu binadamu na utu wake. Hili ni Fundisho kuu hata kwa nchi za Kiafrika
kwamba: maadili, utu wema, na haki msingi za binadamu zinapaswa kushughulikiwa kikamilifu
kwa ajili ya mafao ya wengi ndani ya Jamii, vinginevyo Bara la Afrika linaweza kujikita
likiogelea katika hatari kubwa kwa sasa na kwa siku za baadaye.
Kardinali Pengo
anasema, kwa hakika, maadhimisho ya Sinodi ya Maaskofu juu ya Uinjilishaji Mpya yamesaidia
mchakato wake wa Kuinjilishwa na kwa sasa anajisikia kwamba, yuko tayari hata yeye
kuendeleza dhamana ya Uinjilishaji Mpya inayokazia kwa namna ya pekee; toba, wongofu
wa ndani na utakatifu wa maisha. Ikumbukwe kwamba, maadhimisho ya Sinodi ni tukio
la Kikanisa linaloishirikisha Familia ya Mungu katika ujumla wake.
Baada ya
Sinodi, Waamini wanapaswa kufahamu yale yaliyozungumzwa na Mababa wa Sinodi, kuyasambaza
ili ukweli huu uweze kuwafikia wengi zaidi pamoja na kuibua mbinu mkakati wa utekelezaji
wake kwa ajili ya mafao na ustawi wa Kanisa katika ngazi mbali mbali.
Anawaalika
Waamini na wote wenye mapenzi mema, kusoma kwa makini Ujumbe wa Mababa wa Sinodi juu
ya Uinjilishaji Mpya ili waweze kuumwilisha katika uhalisia na vipaumbele vya maisha
yao, wakati wanapoendelea kusubiri Waraka wa Baba Mtakatifu mara baada ya Sinodi ya
Maaskofu juu ya Uinjilishaji Mpya kama njia ya kutangaza Imani ya Kikristo.