Waziri Mkuu Mizengo Pinda amewataka Watanzania wahakikishe kuwa wao wenyewe na watoto
wao wanatumia fursa ya kudahiliwa kwenye Chuo Kikuu Huria badala ya kuendelea kusubiri
mabweni yajengwe kwenye Vyuo Vikuu.
“Kama tutasubiri mashirika na taasisi za
dini au watu binafsi wajenge vyuo vikuu vya mabweni, ni dhahiri wanafunzi wengi wasio
na uwezo wa kulipia ada katika vyuo hivyo watasubiri kwa muda mrefu ili wadahiliwe
au wakose kabisa nafasi kwenye Vyuo Vikuu,” alisema.
Waziri Mkuu ametoa kauli
hiyo Jumamosi, Oktoba 27, 2012, wakati akiwahutubia washiriki wa mahafali ya 20 ya
Chuo Kikuu Huria cha Tanzania (OUT) yaliyofanyika kwenye viwanja vya chuo hicho eneo
la Bungo, wilayani Kibaha, Pwani.
Alisema kuwepo kwa Chuo Kikuu Huria kumetoa
fursa ya kuongeza udahili wa wanafunzi kwenye vyuo vikuu kwa kiwango kikubwa kwa vile
kinaweza kuchukua wanafunzi wengi kwa wakati mmoja.
“Napenda kuwasihi wananchi
kujiunga na chuo hiki kutokana na ubora wa elimu inayotolewa pamoja na uhakika wa
kuendelea na shughuli za kazi, ajira binafsi na kumwezesha mtu kukaa pamoja na familia,”
alisema.
Waziri Mkuu aliahidi kufuatilia ombi la ujenzi wa barabara ya lami
iendayo kwenye chuo hicho ambayo haizidi kilometa nne ili ikamilike mapema. Pia alimtaka
Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Dk. Shukuru Kawambwa ashirikiane na Wakala wa
Majengo (TBA) kuharakisha upatikanaji haraka wa majengo mikoani kwa taratibu zinazokubalika
ili yasaidie kutatua tatizo la vituo vya kufundishia wataalamu mikoani.
Jumla
ya wahitimu 2,787 walitunukiwa vyeti, stashahada, shahada za kwanza, na stashahada
za juu katika fani za Sayansi ya Jamii, Ualimu, Elimu Maalum, Biashara na Fedha, Sayansi,
Sheria, Uhasibu, Uchumi, Mazingira, Utalii, Masoko, Kiswahili, Utawala, Uandishi wa
Habari na Teknolojia ya Habari na Mawasiliano.
Miongoni mwa viongozi waliohitimu
jana ni Mke wa Waziri Mkuu, Mama Tunu Pinda aliyehitimu Shahada ya Uongozi wa Biashara
na Biashara ya Kimataifa (BBA – International Business). Wengine ni wakuu wa mikoa
ya Shinyanga na Simiyu, Bw. Ali Nassoro Rufunga na Bw. Pascal Mabiti wakiwemo pia
Mkuu wa Wilaya ya Wilaya ya Mbeya, Dk. Norman Sigalla na Mbunge wa Tandahimba, Bw.
Juma Njwayo.
Akihojiwa na waandishi wa habari mara baada ya kupatiwa shahada
yake, Mama Tunu Pinda alisema anawasihi wanawake wote wajiendeleze bila kujali wako
kwenye nafasi ipi kwani elimu haina mwisho. “Umuhimu wa elimu hauangalii kama wewe
ni mke wa kiongozi au la, elimu inawahusu watu wote!,” alisema.
Alisema mahafali
hayo yamempa hamasa ya kusoma tena zaidi na zaidi kwani ameona wahitimu wengine wakipata
shahada za juu zaidi. “Nimeona wenzagu wakipokea Ph.D zao nikasema mimi nina Bachelor
tu, hapana. Lazima niende mbele zaidi,” alisema bila kufafanua kuwa atasomea fani
gani.
Mapema, Mwenyekiti wa Baraza la Chuo hicho, Prof. Samwel Wangwe alisema
Chuo hicho tayari kinashirikiana na vyuo vingine vya elimu ya juu vya umma hapa nchini
kama SUA, MUHAS, DIT na CBE ili kuongeza udahili wa wanafunzi vyuoni.
Alisema
chuo hicho kina mpango wa kutumia teknolojia ya habari na mawasiliano kwa kuchapisha
vitabu vya kujisomea kwenye CD na DVD ili kupunguza gharama za uchapishaji wa vitabu.
Aliziomba wizara zenye majengo yasiyotumika huko mikoani ziyatoe kwa chuo
hicho ili yafanyiwe ukarabati na yaweze kutumika kutoa elimu kwa wataalam wengi zaidi
nchini.
Alitumia fursa hiyo kuiomba Wizara ya Ujenzi waiingize barabara iendayo
stesheni ya Soga kupitia chuoni hapo katika mpango wake wa muda mfupi ili iwekewe
lami na hivyo kurahisisha mawasiliano kwa wakazi wa eneo hilo.
Naye Makamu
Mkuu wa Chuo hicho, Prof. Tolly Mbwete alisema Chuo hicho kina eneo la ekari 105 na
kwamba kinatarajia kuanza ujenzi wa majengo mawili kwa ajili ya madarasa na ofisi
za chuo ambao utagharimu sh. bilioni 15/-.
Kuhusu changamoto zinazokikabili
Chuo hicho, Prof. Mbwete alisema wanakabiliwa na changamoto ya uhaba wa rasilmali
fedha, uhaba wa mabweni na uhaba wa wanataaluma. Aliomba wapatiwe fedha kwa ajili
ya kuimarisha miundombinu yake. Aliomba kuwe na ushirikiano wa karibu zaidi na Ofisi
ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma ili wapatiwe fedha za malimbikizo ya mishahara
ya wafanyakazi wa Chuo hicho.