2012-10-27 15:04:33

Marehemu Padre Salutaris Lucas Massawe kuzikwa Jimboni Iringa hapo tarehe 30 Oktoba 2012


Jimbo kuu la Dar es Salaam linapokea kwa majonzi na masikitiko makubwa habari za kifo cha Padre Salutaris Luca Massawe, Mkuu wa Shirika la Waconsolata Tanzania, kilichotokea hapo tarehe 25 Oktoba 2012 kwa kuzama baharini, eneo la Msalaba Mtakatifu, mjini Bagamoyo nyakati za Alasiri na mwili wake kupatikana asubuhi tarehe 26 Oktoba 2012.

Kanisa limempoteza kiongozi mahiri na mchapakazi aliyetekeleza kazi zake kwa ufanisi. Kabla ya kuchaguliwa na Wanashirika wenzake hapo tarehe 7 Septemba 2011 kuliongoza Shirika nchini Tanzania, alishiriki kikamilifu katika maisha na utume wa Kanisa Jimbo Kuu la Dar es Salaam.

Anakumbukwa sana kutokana na mchango wake wa ushauri katika maboresho ya Taasisi ya Tumaini Media, ambayo iko chini ya Jimbo kuu la Dar es Salaam, inayosimamia TV Tumaini, Radio Tumaini na Gazeti la Tumaini Letu. Alikwisha wahi kufanya utume wake katika Kituo cha Sala cha Waconsolata kilichoko Bunju, nje kidogo ya Jiji la Dar es Salaam.

Askofu Msaidizi Eusebius Nzigilwa wa Jimbo Kuu la Dar es Salaam amesema kwamba, kifo cha Padre Salutaris Lucas Massawe kimeacha pengo kubwa, ambalo halitakuwa rahisi kuweza kuzibika.Waamini wa Jimbo Kuu la Dar es Salaam wanatarajiwa kufanya Ibada ya Misa Takatifu kwa ajili ya kumwombea Marehemu Padre Salutaris Massawe tarehe 29 Oktoba 2012 kabla ya kusafirishwa kwenda Jimboni Iringa kwa mazishi yanayotarajiwa kufanyika hapo siku ya Jumanne tarehe 30 Oktoba 2012, kwenye Makao Makuu ya Shirika la Wamissionari wa Consolata nchini Tanzania.







All the contents on this site are copyrighted ©.