2012-10-23 15:11:29

Watoa rushwa wachukieni na washitakini ili wakione kilicho mnyoa Kanga manyoya!


Hotuba ya Rais Kikwete wakati wa hafla ya kufunga mkutano mkuu wa nane wa Umoja wa Wanawake Tanzania, Mkoani Dodoma, tarehe 21 Oktoba 2012.

Nakushukuru sana Ndugu Mwenyekiti kwa kunialika kuja kujumuika nanyi katika sherehe za kufunga Mkutano Mkuu wa Nane wa UWT. Nawapongeza wajumbe wote wa Mkutano huo kwa kukamilisha vizuri shughuli ya uchaguzi wa watu watakaoongoza Jumuiya yetu kwa miaka mitano ijayo.

Nakupongeza wewe Ndugu Mwenyekiti na Makamu wako kwa kuchaguliwa tena kushika nafasi hizo za juu kabisa za Jumuiya ya Wanawake. Pia nawapongeza wale wote waliobabatika kuchaguliwa katika nyadhifa mbalimbali ndani ya Jumuiya yetu. Nawapongeza wale wote waliojitokeza kugombea ambao hawakujaaliwa kuchaguliwa. Nyote nawapa pole kwa misukosuko iliyowakuta kwani kugombea si kazi rahisi hasa siku hizi ambapo kuna mchanganyiko wa mambo mengi. Yapo mengine yasiyopendeza hata kuyasema, kusimulia ambavyo lazima Chama chetu kiendelee kuyapiga vita.

Mheshimiwa Mwenyekiti; Uchaguzi umekamilika kilichoko mbele yenu ninyi viongozi ni kuchukua nafasi zenu na kutimiza wajibu wenu wa kuongoza Jumuiya ya Wanawake na wanachama wake kutekeleza wajibu na malengo yaliyofanya CCM iunde Jumuiya hii.

Shabaha ya CCM katika kuunda Jumuiya hii ni kukiwezesha Chama kutekeleza madhumuni yaliyotamkwa katika Ibara ya 5 ya Katiba ya Chama cha Mapinduzi: Nanukuu: “…………. kwa hiyo malengo na madhumuni ya CCM yatakuwa yafuatayo: Kushinda katika uchaguzi wa Serikali Kuu na Mitaa, Tanzania Bara na Zanzibar ili kuunda na kushika Serikali Kuu na Mitaa katika Jamhuri ya Muungano kwa upande mmoja na Zanzibar kwa upande wa pili“… Kwa mujibu wa Ibara hiyo, madhumuni ya msingi ya Chama cha Mapinduzi ni kushinda uchaguzi katika ngazi zote tangu kitongoji mpaka taifa.

Tunataka Mwenyekiti wa Kitongoji awe wa CCM, Mwenyekiti wa Mtaa au Kijiji awe wa CCM, Serikali ya Mtaa au Kijiji iwe ya CCM, Diwani awe wa CCM, Halmashauri iwe ya CCM, Mbunge au Mwakilishi awe wa CCM na Rais wa Jamhuri ya Muungano na Rais wa Zanzibar wawe wa CCM, Serikali zetu mbili ziwe za CCM. Hiyo ndiyo sababu na maana ya kuundwa na kuwepo kwa Chama cha Mapinduzi.

Mheshimiwa Mwenyekiti; Hiyo pia ndiyo sababu ya kuundwa na kuwepo kwa Jumuiya ya Wanawake, Jumuiya ya Vijana na Jumuiya ya Wazazi. Kwa vile nchi yetu ni ya demokrasia na kwamba ushindi unapatikana kwa njia ya kupigiwa kura na wananchi. Tunapozungumzia ushindi wa chaguzi za dola tunazungumzia kupigiwa kura na wananchi. Tena katika mfumo wa demokrasia ya vyama vingi ushindi huo unapatikana kwa kushindana na vyama vingine vya siasa ambavyo idadi yake imefikia 20 pamoja na CCM.

Hivyo tunashindania kukubaliwa na wananchi wengi zaidi kuliko wenzetu. Jumuiya za Chama zimeundwa kuisaidia CCM kukubalika na kuungwa mkono na wananchi. Kila Jumuiya imepewa kazi maalum ya kufanya katika jamii na Jumuiya ya wanawake imekabidhiwa kufanya kazi hiyo miongoni mwa wanawake hapa nchini.

Ndugu Wananchi;Kwa vile sasa mmemaliza uchaguzi jipangeni kisawasawa kutimiza wajibu wenu huo. Kazi yenu ya awali ni kujenga Jumuiya yenu. Anzeni kwanza kabisa na kujenga umoja na mshikamano miongoni mwa viongozi, miongoni mwa viongozi na wanachama na miongoni mwa wanachama kwa wanachama. Demokrasia ya uchaguzi ndiyo njia bora kuliko zote za kupata viongozi. Lakini, ina hatari zake na hasa kusababisha mgawanyiko au hata mpasuko miongoni mwa viongozi na miongoni mwa wanachama.

Kazi kubwa ya awali ya kufanya katika kujenga Jumuiya baada ya uchaguzi ni kuziba nyufa za uchaguzi, migawanyiko na nongwa za uchaguzi. Ukomavu na ustahamilivu unahitajika sana. Kwanza lazima mtambue kuwa kugombea ni haki ya kila mwanachama wa Jumuiya, tena ipo kwa mujibu wa Katiba ya Chama na Jumuiya kila baada ya miaka mitano. Hivyo, hakuna sababu ya kumchukia mwanachama aliyejitokeza kugombea. Pia si dhambi kwa mwanachama kumuunga mkono au kumpigania mgombea yeyote anayemuona yeye anafaa.

Ukimchukia au kumuona adui mtu aliyeamua kugombea nafasi unayogombea au kutokukuunga mkono wewe katika uchaguzi na akamuunga mkono mgombea mwenzako, wewe utakuwa unaonyesha udhaifu wa hali ya juu wa kiuongozi. Si mwana demokrasia. Utakuwa hutoshi, ni kiongozi usiyejiamini au unayejikweza na kupenda makuu na kuabudiwa. Na, daima utakuwa kiongozi wa makundi na mwenye visasi. Daima Chama au Jumuiya itakuwa na misuguano isiyoisha chini ya uongozi wako au wewe usipopata uongozi.

Ninaposema maaneno haya nayasema kwako dada yangu Sofia na kwako dada yangu Anna. Uchaguzi umeisha sasa mshirikiane kujenga Jumuiya. Na nyie mlioshinda ndiyo muongoze njia kuwajumuisha wenzenu. Na, nyie mlioshindwa muwe mfano wa kuwa tayari kufanya kazi na wenzenu. Yaliyopita si ndwele tugange yajayo.

Nisieleweke kuwa hata watenda maovu muwapende. La hasha! Watoa rushwa wachukieni na washtakini.

Ndugu Mwenyekiti;Hatua hizo zitasaidia sana kuleta utulivu katika Jumuiya na hivyo kuwapa nafasi ya kufanya kazi ya msingi ya kuijenga na kuiimarisha. Miongoni mwa kazi hizo ni pamoja na kuingiza wanachama wapya, kuwandaa wanachama hao wapya na wa zamani kutimiza ipasavyo majukumu ya msingi ya Jumuiya hiyo. Pia, lipo jukumu la kuwajengea uwezo viongozi wa Jumuiya waweze kutekeleza majukumu yao ya uongozi, kuhakikisha kuwa vikao vinafanyika, vinazungumza mambo ya msingi na vinaendeshwa vizuri. Pia, kuijengea Jumuiya uwezo wa rasilimali fedha na vitendea kazi.

Inatia faraja sana kuwa katika miaka mitano iliyopita, Jumuiya yetu imetimiza vyema majukumu yake ya kujenga na kuimarisha Jumuiya hii. Taarifa ya kazi za Jumuiya zinaonyesha kuwa wanachama wameongezeka kwa wingi wakiwemo wasomi na vijana.

Ila hapa lazima nisema kuwa, wakati tunapitia majina ya wagombea, wanawake wasomi hatukuwaona kwa wingi kujitokeza kugombea. Dada Sophia nilimuuliza, naomba na nyie lazima mjiulize kwa nini? Jumuiya yetu hii muhimu ikikosa wanawake wasomi kuchukua nafasi za uongozi miaka ijayo itakuwa vigumu sana kwa Jumuiya yetu kufanikisha majukumu yake ya kutafuta ushindi na kufanya kazi ndani ya umma na kuipatia CCM ushindi.

Mheshimiwa Mwenyekiti;
Nimefurahi pia kuona Jumuiya inafanya jitihada kubwa kutekeleza Azimio la Halmashauri Kuu ya CCM ambalo limekiagiza Chama na Jumuiya zake kuanzisha miradi ya kiuchumi ili kuongeza kipato kwa lengo la kujitegemea. Nafurahi kuona juhudi za uongozi unaomaliza muda wake zimeanza kuzaa matunda kwani mapato ya Jumuiya hii sasa yameanza kuwa na mwelekeo wa matumaini. Naomba juhudi ziongezwe maradufu ili muda si mrefu ujao Jumuiya ijitegemee na kutoa ruzuku kwa chama.

Kwa bahati nzuri, Jumuiya ina rasilimali za kutosha, hususan majengo na viwanja kwenye maeneo mazuri. Naomba tuzitumie rasilimali hizi vizuri kwa faida ya Jumuiya. Najua peke yenu hamuwezi kuendeleza kila kitu mlichonacho. Simamieni vizuri utaratibu mlioanzisha wa kuingia ubia na wawekezaji mbalimbali. Hakikisheni mnafaidika na ubia mnaouingia. Isiwe ubia ambao anayefaidika ni mwekezaji na kiongozi au viongozi wachache wa Jumuiya. Uwe ni ubia unaofaidisha Jumuiya na kuiwezesha kufikia malengo yake.

Ndugu Mwenyekiti;
Kukamilika kwa uchaguzi wa taifa kunahitimisha mchakato wa uchaguzi kuanzia ngazi ya Tawi mpaka taifa. Viongozi wapya waliochaguliwa, kwa muhtasari, wamekabidhiwa dhamana kubwa ya kuhakikisha kuwa yale mazuri yaliyofanywa na viongozi waliopita yanadumishwa na mafanikio yaliyopatikana yanaendelezwa. Wasibweteke na hali ilivyo sasa, lazima wawe wabunifu na wenye kuona mbali - visionary leaders. Wabuni mipango mipya itakayoendelea kuimarisha Jumuiya na Chama kwa ujumla ili tuweze kuzikabili kikamilifu changamoto zilizopo

Katika kufanya kazi ndani ya umma naomba Jumuiya yetu ijipange vizuri kutimiza wajibu huo. Hakikisheni mna wanachama walio hai, wenye kulipia ada zao kwa wakati, wenye kujitolea michango yao ya hali na mali kwa ajili ya kuendeleza Jumuiya.

Tembeleeni wanachama wenu mara kwa mara, muwaongoze na kuwahamasisha kukisemea na kukitetea Chama cha Mapinduzi. Watembeleeni wanawake, kwa jumla zungumzeni nao, fafanueni sera za Chama cha Mapinduzi. Jihusisheni na shida zao na mahitaji yao. Jitambulisheni nao ili waone Jumuiya yetu hii ndiyo mtetezi wao na mkombozi wao. Kwa kufanya hivyo mtaimarisha imani yao kwa UWT na kwa yule mwenye Jumuiya yake ambae ni CCM.

Ndugu Mwenyekiti;
Viongozi wapya wa UWT hawana budi kuwa na mawazo mapya na mbinu mpya za namna ya kujenga Jumuiya kwa kuzikonga nyoyo za wanachama na akina mama nchini. Jumuiya ikiweza kusimamia ipasavyo haki zao, itaheshimiwa na wengi; ikitetea maslahi ya wanawake ya kijamii na kiuchumi, itakuwa kimbilio la wengi. Lazima UWT muonekane mkiwasemea akina mama pale ambapo wengi wao hawana msemaji, itasikilizwa na kuungwa mkono na wengi. Kwa ujumla itatumainiwa na kupendwa na wengi. Vile vile, viongozi wanatakiwa kuwa wabunifu zaidi ili Jumuiya iendelee kuwa kiungo muhimu cha wanawake wote wa mijini na vijijini. Iwe ni Jumuiya yenye manufaa kwa vijana na wazee, wasiokuwa wasomi, wenye elimu ya kati na wasomi.

Kwangu mimi, hiyo ndio namna nzuri na endelevu ya kuongeza wanachama wengi zaidi kwenye Jumuiya yenu. Mimi binafsi nikiangalia asasi mbalimbali zinazojishughulisha na masuala ya wanawake, hakuna kama UWT. Hakuna taasisi yenye mtandao mpana, yenye wanachama wengi nchi nzima na uzoefu kama UWT. Iweje leo zisikike taasisi hizo, tena baadhi yao zinaishia Dar es Salaam badala ya UWT iliyopo nchi nzima? Hii ni changamoto inayohitaji kushughulikiwa ipasavyo na uongozi mpya.

Ndugu Mwenyekiti;
Kabla sijamaliza hotuba yangu napenda kutoa rai moja kwenu. Nawaomba mhimize viongozi na wanachama wenu wajitokeze kwa wingi kutoa maoni yao kwa Wajumbe wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba watakapotembelea maeneo yao. Hii ni fursa adhimu kwa wanawake. Wahamasisheni wajitokeze kwa wingi kutoa maoni yao. Huu ndio wakati wake.

Ndugu Mwenyekiti,
Waheshimiwa Wajumbe wa Mkutano Mkuu,
Wageni Waalikwa;
Mabibi na Mabwana;

Mwisho, nawashukuru tena kwa kunialika na kunikaribisha vizuri. Nawapongeza kwa kumaliza vizuri uchaguzi na kupata viongozi wapya wa UWT. Kupitia kwenu, nawashukuru wanawake wote wa Watanzania kwa kuendelea kukiunga mkono Chama cha Mapinduzi na Serikali zake mbili, yaani Serikali ya Mapinduzi Zanzibar na Serikali ya Jamhuri ya Muungano. Tunaahidi tutaendelea kuongeza jitihada za kushughulikia changamoto mbalimbali zinazowakabili Watanzania. Azma yetu ipo pale pale “maisha bora kwa kila Mtanzania”

Nawatakia viongozi wote waliochaguliwa mafanikio katika utendaji wa majukumu yao mapya. Rai yangu kwenu ni muwe na umoja, ushirikiano na upendo. Mkifanya hivyo Jumuiya yenu itapata mafanikio na kujiletea maendeleo ya haraka. Na, kwa wanachama na wanawake wote kwa ujumla tafadhali wapeni viongozi wenu mliowachagua ushirikiano unaostahili.
Ahsanteni sana kwa kunisikiliza.
Kidumu Chama Cha Mapinduzi!








All the contents on this site are copyrighted ©.