Mwongozo wa uhamasishaji wa mchakato wa mabadiliko ya Katiba ya Tanzania
Tume ya Haki na Amani ya Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania, imekuwa mstari wa mbele
kuwahamasisha waamini pamoja na watu wote wenye mapenzi mema kuhakikisha kwamba, wanashiriki
katika kutoa maoni yao, jambo ambalo linaungwa mkono na Maaskofu mbali mbali. Idhaa
ya Kiswahili ya Radio Vatican inapenda kukushirikisha Mwongozo huu kama changamoto
iliyotolewa hivi karibuni na Maaskofu walipokutana na Jumuiya ya Wanafunzi Wakatoliki
Roma. MCHAKATO WA MABADILIKO YA KATIBA Mwongozo wa uhamasishaji UTANGULIZI Ni
mara ya kwanza katika historia ya Tanzania wananchi kushirikishwa katika kuandika
Katiba ya nchi. Ni fursa ya pekee, kwa hiyo inatupasa kuitumia vizuri ili kupata Katiba
nzuri itakayoweza kuongoza Taifa letu kwa kadiri ya mpango wa Mwenyezi Mungu. Ni
wajibu wetu sote, na ikiwa hatutautimiza, tuelewe tunawaachia wengine ambao kwa nia
mbaya ama kwa kutoelewa watatumia nafasi hiyo kusukuma mambo ambayo yanaweza kuathiri
vikali misingi mikuu ya taifa letu ambayo ni umoja, mshikamano, maelewano, utulivu,
udugu na amani. Kila siku tunamwomba Mungu adumishe amani katika Taifa letu. Hii ni
nafasi ya kipekee ya kutekeleza kwa matendo wajibu wetu kushiriki kupatikana kwa mwongozo
au “muundombinu” thabiti wa jinsi Taifa letu litakavyoongozwa na kutawaliwa ili kuhakikisha
viashiria vya uvunjifu wa amani, kama kero kuu za wananchi, vinathibitiwa kwa ufanisi
zaidi. Kwa hiyo kila mmoja ajione ana wajibu huo, aupokee na kuutimiza bila kusitasita.
I. KANUNI MSINGI Kujitambua sisi ni nani katika Tanzania
Sisi
ni raia na pia Wakristo Wakatoliki. Ukristo wetu utuongoze tuweze kuwa raia wema ikiwa
ni pamoja na kushiriki mchakato huu wa kuandika Katiba. Ushiriki wetu uwekee mkazo
kanuni za Mafundisho ya Kanisa kuhusu Jamii. Kanuni hizo ni kujali utu wa kila mtu,
upendo, kushughulikia manufaa na ustawi wa wote hasa wanyonge na Mshikamano.
Maana ya Katiba
Ni makubaliano ya wananchi kwa pamoja
juu ya namna ya kuongoza maisha yao kama Taifa na hasa jinsi wanavyotaka kutawaliwa.
Katiba huainisha haki na wajibu kwa kila mmoja – raia na viongozi na kuweka vyombo
vya kusimamia utekelezaji. Ni chombo kitakatifu kinachotusaidia kuishi vizuri tukiongozwa
na maadili mema na hivyo kuthihirisha maisha yenye kuonyesha upendo kwa Mungu na kwa
jirani.
Kwa nini tunahitaji mabadiliko ya Katiba?
Wananchi
wameonyesha wazi kutaka mabadiliko ambayo yataweza kujibu kero na changamoto zinazowakabili
katika maisha yao na kama Taifa. Hasa changamoto ambazo zimeonekana hazina ufumbuzi
katika mfumo wa utawala uliopo na zinaelekea kukatisha tamaa wananchi walio wengi.
Alama za nyakati zinaonyesha hasira ya jamii kwa sababu wanaona mambo mengi hayaendi
vizuri. Ni kwa hiyo tunataka Katiba itakayoweza kuleta mabadiliko hayo, kwa kujibu
kero na changamoto ambazo zimekuwa kikwazo kwa maendeleo ya watanzania wengi na pia
kuathiri tunu ya amani katika nchi yetu. Katiba inaainisha
mamlaka ya wananchi, na kwa hiyo haitoshi tu kuwa na Katiba nzuri. Ni lazima pia iwe
Katiba inayotekelezwa katika maisha ya kila siku ya raia na Taifa. Ikiwa inatokea
ukiukwaji, basi mfumo uwepo wa kulazimisha Katiba kutekelezeka.
II.
MAONI YA KUONGOZA MCHANGO WETU KATIKA KUANDIKA KATIBA Nia ya maoni haya ni kusaidia
waumini wetu kutafakari na kupata uelewa na hivyo kuweza kutoa maoni makini kwa faida
ya jamii yetu na Taifa letu. Moni haya yamejikita hasa katika changamoto zifuatayo:
Rushwa na ufisadi
Tukumbuke Rushwa nia adui wa haki sitapokea
wala kutoa rushwa. Hadi sasa miaka hamsini ya uhuru wetu tunaona rushwa inazidi kukua
na kuenea. Na imejikita pia hadi kwenye vyombo vikuu vya utawala (polisi, mahakama,
serikali na bunge) na inaelekea vigumu kuidhibiti. Tatizo hili kongwe linahusu jamii
nzima – kushiriki kwa kutoa au kupokea ama kufumbia macho. Matokeo yake rushwa na
ufisadi imetuathiri sote kama wananchi na kama Taifa. Tutoe maoni yetu kuonyesha ni
namna gani tatizo hili linaweza kutatuliwa kisheria na kijamii. Tutazame upya jinsi
ya kuimarisha vipengele vya kudhibiti ukiukwaji wa maadili kwa viongozi na pia kuona
kama TAKUKURU kama ni chombo huru na chenye meno kisheria.
Mgawanyo
wa mali na rasilimali za nchi
Hizi ni pamoja na ardhi, madini, mafuta/gesi,
misitu, mbuga za wanyama, bahari, maziwa na mito, bila kusahau mfuko wa taifa (hazina).
Utajiri huu ni majaliwa ya Mwenyezi Mungu kwa ajili ya ustawi wa Watanzania wote kwa
vizazi na vizazi. Hali ilivyo sasa ni tofauti na azma hiyo. Wachache wamejilimbikizia
na wengi wanaendelea kuishi maisha duni, kumekuwa na mgawanyo wa matabaka ya wenye
nacho na wasio nacho. Kijumla wanyonge wametupwa pembeni katika maendeleo ya kiuchumi.
Wawekezaji kutoka nje wanapewa kipaumbele dhidi ya wananchi kwa njia ya mikataba kusainiwa
katika usiri mkubwa. Mwelekeo huu unahatarisha amani na hadi sasa kumekuwa na matukio
mengi ya uvunjifu wa amani katika jitihada za wananchi kujaribu kutetea maslahi yao.
Katiba iweke namna ya kuhakikisha wananchi wote wanashiriki katika kutumia rasilimali
zetu kwa maendeleo ya wote na kuzitunza kwa ajili ya vizazi vijavyo.
Uwajibikaji : raia na viongozi kwa ngazi na makundi yote
Kadiri
siku zinavyokwenda moyo wa uwajibikaji unaendelea kufifia tangu ngazi ya familia.
Jamii inakosa kushikamana katika kujiletea maendeleo na ustawi na hata huharibu miundombinu
iliyowekwa kwa ajili yao. Viongozi wanakiuka maadili na kuliingizia Taifa hasara kubwa
na bado hakuna kuwajibika ama kuwajibishwa. Kwa hiyo tunaona mfumo wa uwajibikaji
kijumla sio mzuri. Katiba iweke taratibu wa kung’olewa madarakani kwa sababu ya kutowajibika,
iimarishe njia za kudhibiti madaraka (checks and balance), bunge liwe kweli mwakilishi
wa wananchi na mijadala yake iongozwe katika hali ya kuruhusu maoni mbadala na kuyaheshimu.
Raia wasibaki katika kulalamika tu, bali waonyeshe mamlaka yao na nguvu yao katika
suala zima la uwajibilkaji.
Vyombo vya kusimamia na kutoa haki
Hapa tulenge mahakama na polisi. Vyombo hivi vimeshindwa kufikia matarajio
ya wananchi. Zaidi vimekuwa upande wa wenye fedha na madaraka na kwa wananchi wa kawaida
na hasa wanyonge imekuwa ni vigumu mno kupata haki zao. Kwa upande mwingine wananchi
nao wanashiriki kuvifanya vyombo hivi vishindwe kutimiza majukumu ya uwepo wake mfano
kwa njia ya kushiriki rushwa, wakati mwingine ikiambatana na kubambikiza kesi, polisi
kutesa na kudhalilisha, kuchelewesha mno kesi na pengine hukumu ikitoka kuonyesha
kuwa mhabusu hakuwa na kosa nk. Katiba iwezeshe vyombo hivi kuwa huru na hivyo kutenda
haki sawa kwa wote badala ya kuegemea upande fulani.
Uteuzi
wa viongozi
Kwa mujibu wa Katiba ya sasa Rais ana madaraka makubwa mno.
Vigezo vinavyotumika haviko wazi na mara kadhaa imeonekana wanashindwa kutimiza majukumu
yao kwa sababu wamepewa kazi ambayo hawana uwezo nayo. Hata inapodhihirika hivyo bado
imekuwa vigumu mno kuwaondoa madarakani. Vigezo vya kidini na kinasaba pia vimekuwa
vikilalamikiwa kuwa vinatumika. Kwa mteuliwa husukumwa kutumikia matakwa ya aliyemteua
badala ya kuwa mtumishi wa wananchi. Katiba ijibu changamoto hii kwa kuweka sifa na
vigezo kadiri ya mahitaji ya nafasi husika na pia njia ya kuwajibisha. Uteuzi usibaki
kwa mtu mmoja bali ufanyike kwa njia shirikishi kupitia Tume huru.
Huduma
bora za jamii na haki za binadamu
Haki hizi ni pamoja na huduma za afya,
elimu, maji, miundombinu nk. Haki hizi zaweza kulenga mtu mmoja mmoja , makundi maalum
kama vile walemavu, wazee na maskini ama jamii nzima. Kutimiza haki hizi serikali
na wananchi wote wanawajibika kila mmoja kwa nafasi na kiwango chake. Haki hizi ziainishwe
katika Katiba na Katiba ihakikishe zinatekelezeka kisheria.
Ukubwa
wa serikali
Tunaweza kuwa na serikali ndogo ambayo inafanya kazi kwa
ufanisi. Hapa tuangalie idadi ya wizara na mawaziri, na hata mgawanyo wa mikoa na
wilaya. Tunaweza kupunguza gharama za uendeshaji kwa kupunguza maeneo haya na hivyo
kuweza kuongeza fungu katika bajeti ya maendeleo na mahitaji mengine muhimu ambayo
tunakwama kuyagharamia. Katiba iainishe hayo isiwe ni matakwa ya kila awamu ya uongozi.
Ukubwa wa bunge
Kwa nia hiyo hiyo ya kupunguza
gharama inafaa kuangalia upya nafasi za ubunge wa kuteuliwa na wa viti maalum. Kimsingi
mbunge ni mwakilishi wa wananchi ambao wanaweza kumwajibisha, na aelewe anabeba dhamana
kubwa na anapaswa kuchapa kazi kwa umahiri na weledi.
Mgawanyo
wa madaraka
Hii ni kanuni msingi ya demokrasia na utawala bora. Kibinadamu
ni jambo msingi kwa sababu inatoa nafasi ya kusahihishana na hivyo kukabiliana na
madhaifu ya kimaumbile. Mihimili mikuu ya dola – bunge, mahakama na serikali yapasa
vifanye kazi kwa uwajibikaji na kuwajibishana na sio katika mwingiliano. Kwa hali
ilivyo sasa tunaona kuna mwingiliano mkubwa na hata tunaona serikali hukimbilia mahakama
(isiyo huru) kama kichaka kuficha udhaifu katika utendaji wa majukumu yake, hasa
kukwepa kutimiza haki za watu. Kwa namna hii utawala wa sheria unakuwa mgumu kudhihirika.
Katiba iimarishe kanuni hii kwa kutoruhusu wabunge kuwa mawaziri, majaji kutoteuliwa
na Rais nk. Wananchi wapewe uwezo wa kudhibiti mihimili ya dola kwa kuweka Mahakama
ya Katiba kupeleka mashauri yao pale wanapoona kuna ukiukwaji wa Katiba katika utekelezaji
wa majukumu yao.
Madaraka ya Rais
Madaraka ya uteuzi
wa viongozi wa juu yana wigo mpana mno unaoingilia mihimili mingine ya dola - jaji
mkuu na majaji na wabunge wa kuteuliwa. Vile vile huteua mkuu wa Jeshi la polisi,
wakuu wa mikoa na wilaya nk. Pia ana mamlaka ya kusamehe wafungwa, kuvunja bunge
na baraza la mawaziri nk. Madaraka haya yanaweza kutumiwa vibaya, na pia uwajibikaji
kwa wateuliwa hao kwa wananchi unakuwa mdogo. Madaraka haya yapunguzwe na/ama yadhibitiwe.
Vigezo viwe wazi na uamuzi ufikiwe kwa njia shirikishi.
Tume
huru ya uchaguzi na Tume nyinginezo
Kwa sababu inaundwa kwa njia ya uteuzi
bila vigezo kuwekwa wazi, wananchi wengi wamekosa imani nayo, na malalamiko yamekuwa
mengi. Uundwaji wa Tume zetu ufanyike kwa uwazi na iliyo shirikishi.
Dhana
ya kuwa Serikali haina dini (Secularity of the State)
Msingi huu ndio
nguzo ya umoja na amani katika nchi yetu. Ifafanuliwe na kusimamiwa kikatiba ikiwa
ni pamoja na kuweka mipaka katika uhuru wa kuabudu kwa kuwa tumeshaona unatumika vibaya
kama vile kuleta mgawanyiko na mtikisiko katika familia, kufanya mihadhara ya kukashifu
dini nyingine, kuharibu mali za wengine na kusababisha uvunjifu wa amani. Vile vile
msukumo wa kuanzisha mahakama ya kadhi ndani ya mfumo wa mahakama za nchi siyo haki
kwa hiyo isiwemo katika Katiba kwa kuwa ni mambo ya kidini na huenda ni njia ya kuifikisha
nchi yetu katika kukiuka dhana ya kuwa serikali yetu haina dini.
Muungano
Kwa
mujibu wa Katiba ya sasa ya Zanzibar, Katiba ya Muungano imevunjwa, wakati huo huo
msukumo wa watu kutaka Muungano uangaliwe upya una hoja zenye nguvu. Tutoe maoni
yetu tukizingatia sababu za waasisi wa muungano, na pia faida na hasara za muungano
kwa wakati huu. Mapendekezo ya kutambua Tanganyika kama nchi yametambuliwa na Katiba
ya sasa ya Zanzibar, kwa hiyo wazo la kuwa na Muungano wenye Serikali tatu ni hoja
ambayo tunaweza kutolea maoni yetu.
Haki ya kuishi
Kwetu
sisi Wakatoliki ni jambo la kupigania kwa nguvu zote Katiba iweze kulinda uhai tangu
kutungwa mimba. Vile vile tunaweza kutoa maoni yetu juu ya adhabu ya kifo. Hapa tuna
wajibu wa pekee kabisa kutoka imani yetu inayotufundisha kwamba mwenye mamlaka ya
kutoa uhai na kuutwaa ni Mungu Mwenyewe.
Umiliki ardhi
Haki
ya watu wa Tanzania Visiwani kumiliki ardhi ya Bara ifutwe kama ilivyo kwa watu
kutoka Tanzania Bara kutoweza kumiliki ardhi huko Visiwani.
Kubadilisha
Katiba
Iwe wazi kutoruhusu Bunge kurekebisha Katiba kadiri ya matakwa
yao. Mabadiliko yafanyike kwa ridhaa ya wananchi. Hapa tunaweza kubainisha na kuainisha
mambo ambayo hayawezi kuguswa kabisa na Bunge. Vipengele hivyo msingi katika Katiba
vibadilishwe tu na wananchi kwa kura ya maoni. Vipengele vingine ambavyo siyo vya
msingi viruhusiwe kubadilishwa na bunge kwa kura si chini ya theluthi mbili. (Ila
hii itawezekana tu kama Katiba itawapa wananchi uwezo wa kuwawajibisha wabunge wao
kwa kuwaondosha au “recall” wasiporidhika na uwakilishi wao).
Mgombea
huru/ binafsi
Ni vema kuruhusu ili kuwezesha wale ambao hawapendi kujiunga
na vyama waweze kuwa na haki ya kugombea nafasi za urais, ubunge na udiwani. Hii itasaidia
pia viongozi hawa kuwajibika zaidi na kwa wananchi badala ya kujali zaidi maslahi
ya chama kama ambavyo imeonekana. Itazuia chuki na uhasama ndani ya vyama kumwondoa
mbunge ambaye ni chaguo la wananchi na wanampenda.
Vyama vya
siasa
Ni muhimu sheria ya kuanzisha na kuendesha vyama vya siasa ishinikize
vyama vyenye kukubalika na kuwakilisha wananchi kwa kuzingatia umoja wa Taifa na kupiga
vita ubaguzi wa ukabila, dini au makundi mangine yoyote. Vilevile kuwe na vigezo vya
vyama kukubalika na wananchi kwa kiasi cha upeo utakaokubalika. Na pia kuwe na mwongozo
kuhusu matumizi na vyanzo vya mapato ya vyama vya siasa kwa ajili ya kudhibiti rushwa
na kutekwa na matajiri.
Muundo wa maeneo ya uwakilishi
Maeneo
haya – mikoa, wilaya na majimbo yagawanywe kwa kuzingatia vigezo wazi – idadi ya watu,
ukubwa wa eneo na hata rasilimali zilizopo. Ugawaji wa bajeti uwe wa kuwezesha pia
kuleta maendeleo kiuwiano kwa maeneo mbalimbali ya nchi ili kusiwe na tofauti kubwa
ya maendeleo baina ya kanda au maeneo mbalimbali ya nchi. Wazo hili linakuwa wazi
zaidi tunapoangalia mgawanyo baina ya Bara na Visiwani.
Kumwondoa
mbunge madarakani kabla ya muda kuisha
Ili kuhimiza uwajibikaji kwa wananchi,
Katiba iwape wananchi uwezo na utaratibu wa kumwondoa mbunge wao madarakani ikiwa
wamethibitisha kuwa hawafai (kwa mfano kulingana na michango yake na kura zake bungeni
kama zina tija kwa wananchi anaowawakilisha).
Elimu na ukomo
wa ubunge
Kipindi cha ubunge kiwe na ukomo wa vipindi viwili, na pia nafasi
hiyo igombewe na wenye elimu isiyopungua kidato cha sita. Kazi hiyo ina majukumu makubwa
yanayohitaji upeo na uelewa na uwezo wa kusoma na kutafiti masuala mengi.
Kuhoji matokeo ya uchaguzi wa Rais, kinga ya Rais kushtakiwa
Fursa
hii iwekwe ili kumsaidia mtu kujibidisha katika uadilifu na uwajibikaji tangu aingiapo
madarakani hadi anapotoka. Kuhoji matokeo inasaidia kuondoa manung’uniko ya wale walioshindwa
na kurejeshea wananchi imani kwa aliyeshinda.
Baraza la Wazee
Kuwe
na Baraza la Wazee lenye uwakilishi wa Kanda za kimila (cultural zones) na Taasisi
mbali mbali zinazosimamia maadili (kama za dini). Baraza liwe pia na uwakilishi wa
sehemu za jamii kama wanaume na wanawake na liwe la kushauri na kuamua au kuafiki
kuhusu mambo muhimu yanayohusu maadili, mila na uhai wa Taifa. (Vilevile ikiwa nchi
imeingia vitani liweze kuafiki kama iendelee na vita au la).
III. NAMNA YA
KUSHIRIKI MCHAKATO Lazima kujiandaa vizuri kwa kusoma nyaraka muhimu, kuzitafakari
kwa muktadha wa maisha yetu kama Watanzania ili tuweze kutoa maoni yenye hoja nzito.
Tuongeze mwamko wetu na tujitokeze kwa wingi na kutoa maoni yetu. Mpango Tume una
hatua hizi: Kuundwa Tume Utoaji wa elimu kwa umma Kukusanya maoni
Kazi
hii imekwishaanza. Katika kila mkoa vinawekwa vituo vya mikutano hiyo. Tunaweza kutoa
maoni kwa kujieleza ama kwa kuandika. Ikiwa unashindwa kufika mkutanoni, basi andika
na kupeleka Tume au kutuma kwa njia ya posta au barua pepe. Maoni yanaweza kuwa ya
mtu mmoja ama ya kikundi. Kufanya majumuisho na uchambuzi
Tume
itaweka maoni ya watu pamoja. Maoni yaliyotajwa na kuelezewa vizuri na wengi yatapewa
uzito Uandikaji wa Rasimu ya Katiba Rasimu kujadiliwa katika Mabaraza
ya Katiba. Kurudisha majumulisho kwa watu kupitia Mabaraza ya Katiba Urutubishaji
/ uboreshaji wa Rasimu baada ya michango ya Mabaraza ya Katiba
Bunge la Katiba kuijadili Rasimu Kura ya maoni Kuanza kutumika kwa
Katiba mpya
Mwisho : Ikiwa itakosa kupitishwa kwa 50% mara ya kwanza
kura itarudiwa. 50% ikikosekana tena, basi tutaendelea kutumia Katiba ya sasa hadi
mchakato mwingine utakapoandaliwa.