Jimbo Katoliki Mbeya katika harakati za maboresho ya huduma ya Afya Wilayani Igongwe
Askofu Evaristo Chengula wa Jimbo Katoliki Mbeya, hivi karibuni amehoji sababu inayokwamisha
Serikali ya Mkoa wa Mbeya kutoa ardhi kwa ajili ya kujenga Chuo cha Wauguzi katika
Hospitali ya Igogwe mchakato ambao umeanza tangu mwaka 1992 bila mafanikio.
Askofu
Chengula alisema katika miaka ya hivi karibuni wafadhili walio wengi wamesitisha misaada
kwa asilimia kubwa kutokana na myumbo wa uchumi kimataifa. Kumbe, ni bahati ya pekee
kupata wafadhili wenye nia ya kutaka kuwajengea Chuo ambacho kitaisaidia Serikali
ya Tanzania na wananchi kwa ujumla kwa kuongeza wataalamu wa kutoa huduma katika Zahanati
na vituo vya afya kama sehemu ya mchakato wa maboresho ya wananchi wa Tanzania
Akizungumza
katika Maadhimisho ya Jubilei ya miaka 50 tangu kufunguliwa kwa Hospitali ya Teule
ya Wilaya ya Igogwe inayomilikiwa na kuendeshwa na Kanisa Katoliki Jimbo la Mbeya
mwaka 1962, Askofu Chengula alisema, kilio chake kikubwa kwa mgeni rasmi ambaye alikuwa
ni Mkuu wa Mkoa wa Mbeya Bwana Abbas Kandoro ni kupata uwanja wa ekari nne unaohitajika
kwa ajili ya kujenga Chuo cha Uuguzi.
Alisema leo hii wafadhili wamekata mawasiliano
ya kutoa misaada na waliobakia wanaendelea kutoa kidogo walicho nacho kutokana na
mioyo yao mizuri, hivyo ni nafasi ya pekee kuwaombea wafadhili hao waliobakia kutoka
barani Ulaya ili mwenyezi mungu aendelee kuwapa afya na uzima. "Lakini tunashangaa
tumezuiliwa na watu wenye mioyo iliyoganda wasio kuwa na mapendo na wenzao wanaoumia,
kwa nini tusiwe na mshikamano wa kuwasaidia watoto wa Nchi hii. Jubilei hii iwatie
moyo tumtegemee Mungu. Serikali kwa nini tusishirikiane kuunganisha nguvu katika huduma
tunayotaka kupatiwa na watu wa mbali?,"alihoji Askofu.
Askofu Chengula alisema
Kanisa limeomba tangu muda mrefu ardhi ya kufanyia kazi kwa ajili ya kuwasaidia watanzania
wote bila kujali: imani, itikadi wala kabila kwa kuwajengea shule itakayoziba pengo
la uhaba wa wauguzi na haiombi fedha, lakini bado kumekuwa na ubabaishaji na kuzungushwa
hali ambayo inaweza kuwafanya wafadhili waliotaka kutoa misaada kukataa tamaa.
"Neema
inapita wala haisubiri, ugumu unatoka wapi? Barabara ndiyo hiyo watu hadi wavunje
miguu, kama hamtaki semeni kuliko kutuambia mara mchakato, tutaangalia…mnaumba dunia?,"aliendelea
kuhoji.
Hata hivyo Askofu Chengula aliwasihi Wauguzi na Madaktari wasikate
tamaa bali waendelee kufanyakazi kwa bidii, juhudi na maarifa, wakitambua kwamba,
wanashiriki katika utume wa Mama Kanisa unaopania kumponya mwanadamu: kiroho na kimwili.
Ameupongeza Uongozi na Wafanyakazi wa Hospitali hiyo kwa kutimiza Agizo la
Sinodi ya pili ya Afrika ambapo Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita katika Waraka
wake “Africae Munus” Dhamana ya Afrika, anakazia umuhimu wa amani, utulivu pamoja
na huduma makini kwa wagonjwa. Waguswe na mahangaiko na mateso ya wagonjwa wanaowahudumia
wakitambua kwamba, kwa kufanya hivyo, wanamhudumia Kristo anayejionesha miongoni mwa
maskini na wanyonge.
Katika Maadhimisho ya Jubilee hii, Wakristo mia mbili
waliimarishwa kwa Sakramenti ya Kipaimara, wakiwemo: watoto, vijana na wazee na amewataka
kuendelea kudumu katika imani na kufuata maadili ya Kanisa badala ya kutanga tanga
toka dhehebu moja hadi jingine, dalili za myumbo wa imani.
Mkuu wa Wilaya ya
Rungwe, Chrispin Meela akizungumza kwa niaba ya mgeni rasmi Mkuu wa Mkoa wa Mbeya,
Kandoro amemwambia Askofu Chengula kulala usingizi na kuwa na amani katika suala la
eneo la ukubwa wa ekari nne za uwanja kwani kuanzia jumatatu tarehe 22 Oktoba 2012
linaanza kushughulikiwa na kulikamilishwa muda siyo mrefu. Meela alisema utafiti unaonesha
kuna kundi la watu katika Kijiji hicho wanaotaka kuleta siasa katika masuala ya maendeleo,
lakini “washindwe na walegee” kwani Serikali haitalivumilia suala hilo linalotaka
kukwamisha maendeleo ya wengi.
"Kwa mujibu wa sheria za ardhi, ardhi yote ipo
chini ya Rais na kwa wilaya msimamizi ni Mkurugenzi wa wilaya na kama ardhi ya umma
inatumika kwa manufaa ya umma kwa nini kuwe na kigugumizi? Serikali ina mpango wa
kuweka Zahanati kila Kijiji na Vituo vya afya kila Kata, Wauguzi watatoka wapi kama
siyo katika Vyuo hivyo vinavyotakwa kujengwa?," alihoji.
Amelishukuru Kanisa
Katoliki kwa juhudi zake kwa kushirikiana na Serikali bega kwa bega na kwamba, hawawezi
kupoteza msaada huo kwa ajili ya watu wachache wasiopenda maendeleo, na kuwa suala
la barabara litaingizwa katika mpango. Tayari zaidi ya Sh.mil.60 zimetengwa kwa Wilaya
ya Rungwe kwa ajili ya kuzishughulikia barabara.
"Pia nimesikia kuna tatizo
la uhaba wa maji lakini niwahakikishie Serikali imeshatenga Sh.Mil.120 kwa ajili ya
Mradi wa Maji Rungwe, lakini tutaendelea kuwaleta wauguzi na madaktari kuboresha huduma
za Hospitali na kwa mwaka wa fedha awamu ya tatu dawa hazitapitia MSD zitakuja moja
kwa moja Wilayani tutapata mgao wa dawa,"alisema.
Hata hivyo Mkuu huyo wa Wilaya
amewaonya watu wanaochoma moto ovyo misitu na hatimaye, kuharibu mazingira na vyanzo
vya maji kuwa waache mara moja kwani watachukuliwa hatua kali za kisheria. Alitoa
kiasi cha sh.500,000 katika mchango wa kukisaidia Kituo cha Watoto Yatima cha Igogwe
ili kiweze kuendelea kutoa huduma nzuri.
Wafadhili kutoka nchini Uholanzi wanaoendelea
kuisadia Hospitali hiyo na kutaka kujenga Chuo cha Wauguzi Yan Veltmann na Hans Berendsen
kutoka katika Hospitali ya Medisch Spectrum Twente enshede wataendelea kutoa misaada
ya vifaa na madawa. Walisema wanaelewa kwamba kuna uhitaji mkubwa wa msaada kwa ajili
ya kuwasaiidia ndugu zao wa afrika kutokana na uhitaji kuongezeka siku hadi siku na
wao watazidi kuongeza pale inapowezekana.