Mama Kanisa katika maadhimisho ya Mwaka wa Imani, anaendelea kuwahimiza watoto wake
kuchuchumilia: toba, wongofu wa ndani na utakatifu wa maisha. Sala ifuatayo inaweza
kutumiwa na Familia ya Mungu kwa ajili ya kuwaombea Mapadre wao, ili waweze kuwa watu
wema na watakatifu.
Ee Bwana Yesu Kristo. Mkombozi wetu, kwa mapendo na tamaa
yako ya kutaka kulinda vema Kanisa lako, ukachagua Mapadri wawe Wachungaji na Viongozi
wa roho za watu. Nakuomba sana; ubariki nia na bidii inayowapasa Mapadri wote katika
kazi zao. Uwaongezee Utakatifu.
Uwatie moyo mzuri wenye mapendo makubwa kwako
na roho za watu. Hivyo wakiisha kupata wenyewe Utakatifu, waweze kuwaongoza vizuri
watu walio chini ya ulinzi wao, katika njia ya Utakatifu na furaha ya milele. Uwajalie
neema zote za hali ya Upadri. Uwajalie ili waonyeshe kila siku ya maisha yao mfano
wa kila fadhila ya mapendo na ya uaminifu katika Kanisa, kwa Baba Mtakatifu na kwa
Maaskofu.
Yesu mpendelevu, uangalie kwa mapendo kazi na mateso ya Mapadri
wako; ubariki na ustawishe mafundisho yao; wanapowafundisha watoto, wanapowahubiria
watu, wanapowatuliza wakosefu watubu na wanapowasaidia wagonjwa na wale wanaokaribia
mauti, Ee Yesu uwe pamoja nao. Uwakinge na hatari zote za roho na za mwili.
Mwokozi
Yesu, ulijalie Kanisa liwe na Mapadri wengi walio Watakatifu. Uwajalie watoto na vijana
wengi wasikie wito wa Upadri, uwatie furaha na Utakatifu na roho za Mapadri waliokufa
uzijalie punziko la amani.
Kwa mimi mwenyewe Ee Yesu mpendelevu, naomba unijalie
roho ya imani na utii mnyenyekevu ili niwaheshimu Mapadri kama Mawakili wa Mungu.
Niwatii katika njia zote za wokovu wa roho yangu. Amina.