2012-10-22 08:36:52

Fadhila ya Uaminifu, Upatanisho na Msamaha ni vigezo muhimu vinavyodumisha maisha ya ndoa na familia


Ndugu msikilizaji wa Radio Vatican, karibu tena tuendelee na tafakari yetu ya maisha ya Ndoa na Familia leo tukazie zaidi umuhimu wa uaminifu na msamaha kama nguvu za lazima kati ya wanandoa. RealAudioMP3
Mojawapo ya ahadi wanazopeana wana-ndoa ni ahadi ya uaminifu na upendo katika hali zote za maisha, katika raha na taabu siku zote za maisha yao. Ahadi hizo huwapa nguvu wana-ndoa kuanza safari yao hata kama baadaye haiko wazi lakini kwasababu wako kwenye umoja basi hupeana matumaini wakati wote wa safari yao. Uaminifu huenda sambamba na fadhila za matumaini, ujasiri na upendo. Uaminifu ni lazima utawaliwe pia na kujikatalia pale ambapo yanajitokeza mazingira yanayopingana na uaminifu.
Ndugu msikilizaji kama tulivyotaja hapo mwanzoni uaminifu wa wanandoa ni ule wanaojifunza kwa Kristo. Aliyebaki mwaminifu mpaka juu ya msalaba na hivyo akatulea wokovu.
Ndugu msikilizaji Waswahili husema: “Chupa zinapokaa pamoja hugongana, lakini pia ili miti inyoke vizuri msituni ni lazima ikwaruzane.” Hali kadhalika wana-ndoa wanapokaa pamoja katika utofauti wa tabia zao hutofautiana na utofauti huu ni muhimu katika ujumuiya wao. Lakini pia mapungufu hutokea na yanapotokea dawa pekee katika mapungufu haya ni ni msamaha.
Mwenyeheri Yohane Paulo II katika mafundisho yake kwa wanandoa mwaka 1996 aliwaambia “Upendo wa kindoa ni lazima utawaliwe na msamaha. Hakuna mapendo yasiyojua msamaha. Kila anayesamehe anafungua mlango wa kusamehewa. Na kwa Wakristo hujifunza msamaha toka kwa Kristo aliyewasamehe sio tu marafiki zake ila hata maadui wake pia. Tujifunze kusamehe na kusahau, kwani kukosa na kukoseana ni sehemu ya ubinadamu, kusamehe na kusahau ni kuanza hija ya utakatifu wa maisha.
Ndugu msikilizaji kila mmoja wetu anajua jinsi ambavyo familia nyingi kila mahali zipo kwenye magomvi ya kudumu. Msamaha na uaminifu huhitaji sadaka kubwa lakini faida zake ni nyingi kwa faida ya wanandoa na familia zao,kwa faida ya jamii zima. Kwa uhakika ni dawa nzuri katika maisha ya ndoa na familia.
Kutoka Studio za Radio Vatican ni mimi Padre Raphel Mwanga, wa Jimbo Katoliki la Same, Taasisi ya Ndoa na Familia, Chuo Kikuu cha Kipapa cha Laterano- Roma.








All the contents on this site are copyrighted ©.