2012-10-20 15:47:22

Wasomi waliojikita katika majadiliano ya kidini na kiekumene wapewa Tuzo la Ratzinger!


Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, amewashukuru na kuwapongeza viongozi mbali mbali waliofanikisha maandalizi ya Tuzo la Ratzinger, ambalo limeingia katika awamu ya pili, linalopania kuwazawadi wasomi wanaofanya tafiti za kisayansi kuhusu kazi mbali mbali zilizowahi kutungwa na Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita.

Kwa namna ya pekee, amewashukuru Padre Daley na Professa Brague walionesha umahiri mkubwa katika tafiti na ufundishaji, kiasi cha kushiriki maisha na utume wa Kanisa kama Padre na Mlei, katika ulimwengu mamboleo. Wasomi hawa wawili wanaendelea kutoa mchango mkubwa katika mchakato wa majadiliano ya kiekumene na kidini, kwa njia ya tafiti za kina kuhusu Mababa wa Kanisa, ili kuwajengea watu ari na moyo wa kulipenda Kanisa, sanjari na kukuza moyo wa upendo na mshikamano na waamini wa Kanisa la Kiorthodox.

Baba Mtakatifu anasema Profesa Brague ni msomi na mtaalam katika masuala ya filosofia za dini, hususan dini ya Kiyahudi na Kiislam Nyakati za Kati. Katika maadhimisho ya Jubilee ya miaka hamsini ya Mtaguso Mkuu wa Pili wa Vatican, Baba Mtakatifu anapenda kushiriki pamoja nao Tamko la Mababa wa Mtaguso Mkuu wa Pili wa Vatican kuhusu umuhimu wa majadiliano ya kidini na kiekumene, utu wa mwanadamu na uhuru wa kuabudu vikipewa kipaumbele cha kwanza.

Baba Mtakatifu anawahimiza Wasomi hawa waliobahatika kujinyakulia Tuzo la Ratzinger kuendelea kushirikisha mang'amuzi yao katika nyanja hizi, ili kukuza na kuendeleza majadiliano kati ya Kanisa na Ulimwengu mamboleo. Anawashukuru kwa majitoleo yao yanayojionesha katika kutafuta ukweli wa mambo kwenye lugha mbali mbali, changamoto kwa Mama Kanisa kuendeleza ari na moyo wa kufanya tafiti za kina katika sekta ya elimu na utamaduni.

Baba Mtakatifu anawaalika wanafunzi na wasomi mbali mbali kujihusisha na tafiti hizi, kama ilivyojionesha nchini Poland na semina maalum itakayofanyika hivi karibuni huko Rio de Janeiro, nchini Brazil. Washindi wa tuzo hii wameonesha umahiri wa kuunganisha sayansi na hekima, daima mwanadamu akipewa msukumo wa pekee, ili aweze kugundua sanaa ya kuishi vyema, kwa njia ya imani angavu inayotolewa ushuhuda wa kweli kwa kuonesha uwepo wa Mungu katika maisha ya mwanadamu.

Ni vyema ikiwa kama watu watatambua kwamba Yesu ni njia ya maisha na kwamba kwa njia ya mwanga kutoka kwa Mwenyezi Mungu, wasomi wanapata fursa ya kugusa akili na nyoyo za watu, changamoto kutoka kwa Mababa wa Mtaguso Mkuu wa Pili wa Vatican na dhamana ya Uinjilishaji Mpya.







All the contents on this site are copyrighted ©.