2012-10-18 14:14:03

UJUMBE WA BABA MTAKATIFU BENEDIKTO XVI KWA SIKU YA KIMISSIONARI DUNIANI, 2012



Ujumbe wa Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, kwa maadhimisho ya Siku ya Kimissionari Duniani, itakayoadhimishwa hapo tarehe 21 Oktoba, 2012, unaongozwa na kauli mbiu “Mwaliko wa kusambaza Neno la Ukweli”.Kutujuvya zaidi kutoka Studio za Radio Vatican ni Padre Agapito Mhando. RealAudioMP3

Hili ni jukumu la kila Mkristo. Maadhimisho ya Siku ya Kimissionari kwa mwaka huu yana umuhimu wa pekee sana, kwani yanakwenda sanjari na kumbu kumbu ya miaka hamsini tangu Mababa wa Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican walipoandika hati kuhusu Uinjilishaji wa Awali, kwa lugha ya Kilatini, “Ad Gentes”. Ni wakati wa maadhimisho ya Sinodi ya Maaskofu kuhusu Uinjilishaji Mpya. Matukio yote haya yanapania kwa namna ya pekee, kuimaarisha ari ya utangazaji wa Habari Njema ya Wokovu hadi miisho ya dunia.

Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican uliokuwa na ushiriki mkubwa wa Maaskofu kutoka sehemu mbali mbali za dunia, ulikuwa ni kielelezo makini cha Kanisa la Kiulimwengu, kwani uliwakutanisha Maaskofu wanaotekeleza utume wao katika nchi za kimissionari, Maaskofu katika Majimbo ya Makanisa yao mahalia; wachungaji wa Jumuiya za waamini na wasiokuwa waamini. Kila kikundi kilijitahidi kutoa mchango wake kwa kuonesha umuhimu wa azma ya Uinjilishaji wa awali pamoja na kutambua kwamba, umissionari ni kiini na uelewa wa Kanisa.

Changamoto hii ni kubwa katika mapambazuko ya Millenia ya tatu ya Ukristo kwani kuna idadi kubwa ya watu wasiomfahamu bado Kristo. Hapa wakristo hawana budi kuamsha ari na moyo wa utangazaji wa Habari Njema ya Wokovu kama ilivyokuwa kwa Kanisa la Mwanzo; Lilikuwa ni Kanisa dogo na lisiokuwa na ulinzi wa kutosha, lakini bado liliweza kusimama kidete kutangaza Injili ya Kristo na kutolea ushuhuda wa tunu msingi za maisha ya Kikristo katika ulimwengu uliokuwa unafahamika kwao.

Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, anasema, si jambo la kushangaza kuona kwamba, Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican na baadaye viongozi mbali mbali wa Kanisa walianza kutoa kipaumbele cha kwanza kwa ari na moyo wa kimissionari ndani ya Kanisa, kama sehemu ya mwendelezo wa amri ya Kristo aliyoitoa kwa Mitume, ikatekelezwa na waandamizi wao na sasa huu ni wajibu shirikishi wa Watu wa Mungu. Kutangaza Injili ya Kristo hadi miisho ya dunia ni wajibu msingi wa Maaskofu, ambao wanayo dhamana nyeti ya kuuinjilisha ulimwengu.

Amri ya kutangaza Injili ya Kristo inagusa kwa namna ya pekee, mikakati ya kichungaji na maisha ya Kanisa mahalia. Mababa wa Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican wamelitilia wazo hili mkazo mkubwa. Huu ni mwaliko kwa Kanisa mahalia daima kujitahidi kusoma alama za nyakati, ili kuangalia kama mtindo wake wa maisha na mikakati yake ya kichungaji inakwenda sanjari na agizo hili la Kristo katika ulimwengu mamboleo unaobadilika kwa kasi ya ajabu. Kila Mkristo anapaswa kutambua kwamba, anawajibishwa na Amri ya Kristo ya kutangaza Habari Njema ya Wokovu hadi miisho ya dunia.

Makleri, watawa na waamini walei, wote kwa pamoja hawana budi kufuata nyayo za Mtakatifu Paulo, Mtume na Mwalimu wa Mataifa, aliyefanya kazi hii kwa ustadi mkubwa, akateswa na kujitaabisha ili kuhakikisha kwamba, Injili inawafikia hata wale waliokuwa bado hawajamwamini Mungu; kamwe hakujihurumia, kila chembe ya muda wake aliitumia kikamilifu, ili kuhakikisha kwamba, Injili ya Kristo inafahamika na wengi.

Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, katika ujumbe wake kwa Siku ya Kimissionari duniani anakazia kwa namna ya pekee, ushirikiano wa kimissionari, unaojumuisha mifumo mipya si tu katika masuala ya kiuchumi, bali wakristo wanapaswa kujimwaga barabara uwanjani ili waweze kushiriki kikamilifu. Maadhimisho ya Mwaka wa Imani sanjari na Maadhimisho ya Sinodi ya Maaskofu kwa ajili ya Uinjilishaji mpya ni matukio muhimu ambayo Mama Kanisa anapenda kuyatumia kuzindua ari na mwelekeo mpya wa ushirikiano wa kimissionari, unaowahusisha wakristo wengi zaidi.

Kupanuka na kuenea kwa utume wa Mama Kanisa katika ulimwengu mamboleo, kunahitaji kuwa na njia makini zinazoweza kutumika kwa ajili ya kutangaza Neno la Mungu. Jambo la msingi ni kuhakikisha kwamba, kila mwamini anaimarisha imani yake kwa Injili ya Kristo, hasa nyakati hizi za mabadiliko makubwa yanayoendelea kujitokeza sehemu mbali mbali za dunia.

Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita anasema, moja ya kizingiti kikubwa cha Uinjilishaji mpya ni kinzani za kiimani, si tu katika nchi za Magharibi, bali sehemu kubwa ya ulimwengu unaoonesha kwa namna ya ajabu kiu ya kutaka kumfahamu Mwenyezi Mungu; watu hawa hawana budi kualikwa ili waweze kupata lishe ya chakula kilichoshuka kutoka mbinguni na kuzima kiu ya maisha yao kwa Kristo chemchemi ya maji ya uzima.

Kuna haja ya kuwa na ari na mwamko mpya wa kutangaza na kushuhudia imani kwa Kristo na Kanisa lake, ili kuendeleza azma ya Uinjilishaji mpya kwa waamini waliokuwa na bahati ya kusikia kwa miaka mingi Injili ya Kristo ikihubiriwa katika viunga vyao, lakini kwa bahati mbaya sasa wamekengeuka. Ni wajibu wa Mama Kanisa kuwasaidia tena waamini kama hawa kuonja ile furaha ya kuamini.

Baba Mtakatifu anakumbusha kwamba, hii ni dhamana kwa Wakristo wote na wala si kwa ajili ya Makleri peke yao; kila mwamini anapaswa kufaidika na mchakato huu wa Uinjilishaji mpya sanjari na ushiriki wake makini. Kiini cha Ujumbe wa Injili ni Upendo mkamilifu wa Mungu unaojionesha kwa namna ya pekee, kwa Mwenyezi Mungu kumtuma Mwanaye wa pekee, Yesu Kristo aliyejitwalia hali ya umaskini wa binadamu, akawapenda na kuwakomboa kutoka katika utumwa wa dhambi na mauti kwa kumwaga Damu yake Azizi pale juu Msalabani kama sadaka safi inayompendeza Mwenyezi Mungu.

Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, anasema kwamba imani ni zawadi kutoka kwa Mwenyezi Mungu, changamoto kwa waamini kushirikishana na jirani zao hazina hii muhimu kwani kamwe hawapaswi kuibinafsisha! Kuna makundi makubwa ya Makleri, Watawa na Waamini walei wanaotoka katika nchi zao, Jumuiya zao na kwenda kwenye Makanisa mengine kutoa ushuhuda wa kweli za maisha ya Kikristo sanjari na kutangaza Habari Njema ya Wokovu kwa jina la Yesu Kristo. Hiki ni kielelezo makini kabisa cha umoja, ushirikishwaji na upendo miongoni mwa Makanisa.

Hapa mwamini anaweza kuona jinsi ambavyo imani ilivyonyanyuliwa juu kabisa na kugeuzwa kuwa ni sehemu ya upendo. Kwa namna ya pekee, Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, anachukua fursa hii kuyashukuru Mashirika ya Kipapa ya Kazi za Kimissionari, ambayo kwa hakika, yamekuwa ni vyombo vya vya ushirikiano na Kanisa la Kiulimwengu.

Kwa njia ya utume na kazi zao mbali mbali Injili inageuzwa kuwa ni msaada kwa wengine; haki kwa maskini; elimu kwa watoto wanaoishi vijijini; huduma ya afya kwa wote wanaohitaji, lakini kwa namna ya pekee, wanaoishi vijijini; huu ni ukombozi unaopania kuzima kiu ya mahitaji ya mtu; kuthaminiwa yule ambaye amesukumizwa pembezoni mwa Jamii; kuchangia maendeleo endelevu sanjari na kuvunjilia mbali kuta za utengano wa kikabila pamoja na kuheshimu zawadi ya maisha katika hatua zake zote.

Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, anahitimisha ujumbe wake kwa maadhimisho ya Siku ya Kimissionari duniani, kwa kutoa baraka zake za kichungaji kwa wadau wote wa Uinjilishaji wa awali, ili kwa njia ya Roho Mtakatifu na neema za Mwenyezi Mungu, utume huu uweze kuwa na nguvu zaidi katika historia ya ulimwengu.











All the contents on this site are copyrighted ©.