2012-10-18 10:40:50

Mama Kanisa bado anachangamotishwa kutangaza Habari Njema ya Wokovu hadi miisho ya dunia! Hakuna kulala hadi kieleweke!


Maadhimisho ya Siku ya Kimissionari Duniani yanakwenda sanjari na kumbu kumbu ya Jubilee ya Miaka hamsini ya Mtaguso Mkuu wa Pili wa Vatican, Mwaka wa Imani uliotangazwa na kuzinduliwa na Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita hivi karibuni, Miaka ishirini ya Katekisimu Mpya ya Kanisa Katoliki, sanjari na maadhimisho ya Sinodi ya Maaskofu juu ya Uinjilishaji Mpya.

Mama Kanisa bado anaendelea kuhimiza umuhimu wa Uinjilishaji wa awali miongoni mwa waamini wasiomfahamu bado Mungu, kama Mababa wa Mtaguso Mkuu wa Pili wa Vatican walivyosema, "Ad Gentes". Mtaaguso Mkuu wa Pili wa Vatican, ilikuwa ni Pentekosti mpya kwa Kanisa, iliyowakusanya Maaskofu kutoka sehemu mbali mbali za dunia, ili kutoa dira na mwongozo kwa Mama Kanisa katika mapambazuko ya Millenia ya tatu ya Ukristo.

Huu ulikuwa ni Mtaguso wa Kiekukemene, uliowashirikisha pia wawakilishi kutoka dini na madhehebu mbali mbali ya Kikristo. Zaidi ya Maaskofu mia sita kutoka katika nchi za kimissionari walihudhuria. Leo hii Kanisa katika nchi hizo lina zaidi ya Majimbo elfu moja na mia moja, kwa hakika, Kanisa limekuwa na kupanuka katika kipindi cha miaka hamsini iliyopita.

Haya ni maneno yaliyomo kwenye ujumbe wa Mheshimiwa Padre Timothy Lehane Barret, Katibu mkuu wa Baraza la Kipapa la Uinjilishaji wa Watu, katika maadhimisho ya Siku ya Kimissionari Duniani, inayoadhimishwa tarehe 21 Oktoba 2012. Anasema, ari na moyo wa kimissionari unapaswa kukuza na kudumishwa hususan katika maadhimisho ya Mwaka wa Imani; kwa njia ya kutangaza Injili ya Kristo, kwa kutambua kwamba, hii kimsingi ni dhamana ya Wakristo wote, lakini Maaskofu ni wadau wa kwanza kabisa.

Uinjilishaji ni utume muhimu sana unaopaswa kugusa medani mbali mbali za maisha ya Kanisa pamoja na kuwashirikisha waamini kwa ukamilifu zaidi, kwani kwa njia ya Ubatizo waamini wamekuwa pia ni wadau wakuu wa Uinjilishaji, hasa zaidi kwa njia ya maisha yao adili.

Mwaka wa Imani uwawezeshe waamini katika Jumuiya zao za Kikristo kuwasha moto na ari ya kutangaza na kushuhudia imani yao katika uhalisia wa maisha. Mtikisiko wa imani, usiwe ni kikwazo cha Uinjilishaji Mpya, changamoto kwa Waamissionari wapya kujitokeza ili kuweza kumtangaza Kristo hadi miisho ya dunia, kwa kutumia karama na vipaji walivyokirimiwa na Mwenyezi Mungu. Kila mwamini ajibidishe kukutana na Kristo Mfufuka, ili aweze kuimarisha imani yake na hatimaye, kuishuhudia.

Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, anawashukuru na kuwapongeza Wamissionari na Mashirika yote ya Kimissionari yanayojitosa kimasomaso kwa ajili ya kutangaza Habari Njema ya Wokovu. Anawahimiza kuendelea kuonesha ushirikiano na mshikamano ili kufanikisha dhamana hii nyeti katika mapambazuko ya Millenia ya tatu katika Ukristo.

Huduma mbali mbali zinazotolewa na Wamissionari na Mashirika haya katika sekta ya elimu, afya, maendeleo endelevu; haki na amani ni kielelezo makini cha umwilishaji mbegu ya Injili katika hali halisi ya maisha ya watu. Maadhimisho ya Siku ya Kimissionari Duniani, yalete mwamko mpya katika Mwaka wa Imani.







All the contents on this site are copyrighted ©.