Tanzania na Omani kukuza na kuimarisha biashara, siasa, elimu ya juu na utunzaji wa
kumbu kumbu
Tanzania na Oman zimetiliana saini mikataba mitano itakayoziwezesha nchi hizi mbili
kufanya biashara baina yake kwa uaminifu na utaratibu ambao unaridhisha pande zote.
Mikataba hiyo imetiwa saini katika mkutano wa wafanyabiashara wa Oman tarehe 16 Oktoba,
2012 na kushuhudiwa na Rais Jakaya Mrisho Kikwete. Mikataba hiyo inahusu kuundwa kwa
Baraza la Biashara baina ya Oman na Tanzania, kukuza na kulinda biashara, majadiliano
ya kisiasa na, Elimu ya Juu na makubaliano ya utunzaji na uwekaji kumbukumbu.
Mara baada ya kutiliana saini mikataba hiyo, Rais Kikwete amewaeleza wafanyibiashara
wa Oman kuwa Tanzania iko tayari kufanya biashara na Oman na kwamba milango iko wazi,
hivyo kuwakaribisha wale wote wenye nia na uwezo wa kuwekeza katika Kilimo, Viwanda,Uvivu,
Utalii na Sekta mbalimbali ambazo Tanzania imejaliwa kuwa nazo.
Rais amesema
mbali na Tanzania kuwa na eneo kubwa ambalo linajumlisha Bara na Visiwani, "Tanzania
ni mlango mkuu kwa nchi za Afrika Mashariki na pia zile zilizopo kusini mwa Afrika
na Maziwa Makuu" amesema. Na kuwaasa wafanyibiashara wa Oman kuja kuwekeza Tanzania.
Mapema kabla ya Rais kufungua rasmi mkutano wa wafanyabiashara, Mwenyekiti
wa Chama cha wafanyabiashara na wenye Viwanda cha Oman mheshimiwa Khalil Al Khonji
ameelezea jinsi nchi mbili hizi zinavyofurahia na kuuenzi uhusiano wa kindugu baina
yake.
"Mahusiano ya karibu baina ya Oman na Tanzania yanaenziwa na serikali
pamoja na wananchi wake, na tunapoongelea kukuza biashara na uwekezaji kwa ajili
ya nchi zetu, tunategemea kupata suluhisho la kudumu la kuondokana na tatizo la
kutokuwepo kwa uwekezaji katika nchi zetu" amesisitiza.
Mapema kabla ya kufungua
mkutano wa wafanyabiashara, Rais Kikwete ametembelea makumbusho ya kijeshi Bait Al
Falaj ambapo ameelezwa historia ya nchi ya Oman. Rais pia ameweka jiwe la msingi ambapo
utajengwa ubalozi wa Tanzania nchini Oman.
Katika siku yake hii ya pili, Rais
Kikwete amealikwa kwenye chakula cha usiku na Sultani Qaboos Bin Said. Rais anaendelea
na ziara yake ambapo anatarajiwa pia kukutana na watanzania wanaoishi na kufanya kazi
Oman.