2012-10-17 14:23:38

Katekesi za Baba Mtakatifu katika Mwaka wa Imani zinalenga kufahamu kweli za Imani kuhusu Mungu, Binadamu, Kanisa na Ulimwengu mintarafu Kanuni ya Imani


Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, Jumatano tarehe 17 Oktoba, 2012 ameanza mzunguko mpya wa katekesi unaolenga kutoa tafakari ya kina kuhusu maadhimisho ya Mwaka wa Imani, kwa kukazia umuhimu wa shule ya sala, ili kuleta mwamko na ari mpya ya kumwamini Kristo, Mkombozi pekee wa dunia, ili hatimaye, waamini waweze kufuata nyayo zake kwa kutolea ushuhuda wa nguvu ya imani inayoleta mabadiliko.

Maadhimisho ya Jubilee ya Miaka hamsini ya Mtaguso Mkuu wa Pili wa Vatican ni fursa nyingine ya kumrudia Mwenyezi Mungu pamoja na kujitahidi kuimwilisha imani kwa Kristo na Kanisa lake ambaye ameendelea kuwa kweli ni mwalimu wa binadamu kwa njia ya: Utangazaji wa Neno la Mungu, Maadhimisho ya Sakramenti za Kanisa pamoja na Matendo ya Huruma kama mwongozo wa kukutana na hatimaye, kumfahamu Kristo: Mungu kweli na mtu kweli.

Lengo ni kumwezesha mwamini kufanya mabadiliko ya ndani kwa kurekebisha mahusiano yake yote pamoja na kuanza kujenga mwelekeo mpya mintarafu wito wao katika historia, maana ya maisha na kwamba, wao daima ni mahujaji kuelekea Yerusalem ya mbinguni.

Baba Mtakatifu anasema, Katekesi zake katika maadhimisho ya Mwaka wa Imani, zinapania kwa namna ya pekee kuimarisha hija ya waamini wanaotafuta furaha katika imani, ili waweze kuifahamu na kuimwilisha. Hii ni imani kwa Mungu ambaye ni upendo, aliyejishusha na kumkaribia mwanadamu, kiasi cha kuyamimina maisha yake pale juu Msalabani kama njia ya kumkomboa binadamu huyu kutoka katika lindi la dhambi na mauti; hatimaye, aweze kuonja upendo na utimilifu wa maisha.

Imani hii kuliko wakati mwingine wowote katika historia inapaswa kutolewa ushuhuda makini, watu waonje na kuguswa na upendo wa Mungu na huduma kwa wahitaji ili kuondokana na ubinafsi na umaskini wa binadamu kutokana na uchoyo wake. Imani ya Kikristo inajidhihirisha kwa njia ya matendo ya huruma, ina nguvu katika matumaini na humwezesha mwanadamu kupata utimilifu wa maisha.

Imani inafumbata ujumbe huu na hivyo kumletea mwanadamu mabadiliko ya ndani yanayomwezesha kumfahamu Mungu na mipango yake katika maisha ya mwanadamu. Mungu anavuka mipaka ya akili ya binadamu, ibada na sala. Kwa njia ya Maandiko Matakatifu, waamini wanaweza kuufahamu ukweli kwa njia ya Roho Mtakatifu. Yesu ni Neno wa Mungu aliyefanyika mwili, akateswa, akafa na kufufuka kutoka katika wafu. Huyu ndiye aliyejifunua kwa njia ya vinywa vya manabii, lakini, kwa njia ya Neno lake amejionesha kwa wote hadi miisho ya dunia.

Kanisa ambalo limezaliwa kutoka katika ubavu wa Kristo, pale alipochomwa mkuki mara ikatoka damu na maji, alama za Sakramenti za Kanisa, ni kielelezo makini cha matumaini kwa Yesu Kristo Mkombozi wa dunia. Yesu aliteswa, akafa na kufufuka, amekaa kuume kwa Baba, ni hakimu wa wazima na wafu ndicho kiini cha imani ya Kanisa, changamoto kwa wafuasi wa Kristo anasema Baba Mtakatifu kuwa waaminifu kwa imani hiyo.

Kanuni ya Imani ni muhtasari ambao unaonesha kweli za kiimani zilizopokelewa kwa mara ya kwanza na Mitume wa Yesu. Baba Mtakatifu anawaalika waamini kwa namna ya pekee, kujibidisha kufahamu mahudhui yaliyomo kwenye Kanuni ya Imani kwani hii ni dira na mwanga katika hija ya maisha ya waamini hapa duniani, ili kuvuka vikwazo vya ukame na jangwa na maisha ya kiroho katika ulimwengu mamboleo. Kanuni ya Imani ni chimbuko la maisha adili miongoni mwa Wafuasi wa Kristo.

Huu ndio mchango mkubwa na endelevu kutoka kwa Mwenyeheri Yohane Paulo wa Pili, Kanisa linapoadhimisha kumbu kumbu ya Miaka ishirini tangu alipochapa Katekisimu Mpya ya Kanisa Katoliki. Kanisa lina dhamana ya kuitangaza Imani na Injili, ili mwanga wa Injili ya Kristo uweze kuleta mabadiliko katika maisha ya Kijamii, kwa kuwashirikisha wengine matumaini yaliyoko ndani mwao. Waamini wajitahidi kujifunza imani yao ili kukabiliana na changamoto mbali mbali zinazojitokeza katika Ulimwengu mamboleo. Ujumbe wa Injili uwasaidie waamini kumrudia Mungu kwa njia ya Yesu Kristo.

Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, anasema, hili ndilo lengo lake la Katekesi atakazotoa katika maadhimisho ya Mwaka wa Imani; ili kufahamu kwa kina na mapana kuhusu kweli za Imani kwa Mungu, Binadamu, Kanisa, Maisha Jamii na Ulimwengu, mintarafu Kanuni ya Imani. Ni matumaini ya Baba Mtakatifu kwamba, imani hii itaweza kumwilishwa katika maisha; kwa kukazia wongofu wa ndani unaotoa mwono mpya wa kumwamini, kumfahamu na hatimaye kukutana naye.







All the contents on this site are copyrighted ©.