2012-10-17 09:41:40

Katekesi makini na kina; ushuhuda wa Injili ya Upendo na Majadiliano na ulimwengu mamboleo ni kati ya vipaumbele katika dhamana ya Uinjilishaji Mpya


Mababa wa Sinodi ya Maaskofu juu ya Uinjilishaji mpya wanaendelea kuhimiza waamini kufanya maandalizi ya kutosha: kiroho na kimwili wanapopania kufanya hija kwenye maeneo matakatifu yanayobeba viashiria vya imani ya Kanisa. Nchi Takatifu ni kati ya maeneo yanayobeba kwa kiasi kikubwa historia ya maisha na utume wa Yesu aliyeteswa, akafa na kufufuka kutoka katika wafu. Lakini kwa bahati mbaya, maeneo haya yamekuwa pia yakijuhujimiwa.

Uwepo wa mahujaji kutoka sehemu mbali mbali za dunia ni kielelezo cha imani hai, kinachoweza pia kukoleza na kuimarisha imani ya wafuasi wa Kristo katika maeneo matakatifu. Ni mwaliko wa kuendelea kuombea imani na amani inayokabiliwa na changamoto kubwa huko Mashariki ya kati.

Waamini wanapaswa kutambua kwamba, imani yao si jambo binafsi, wala urithi wa kijamii na kihistoria, bali ni dhamana nyeti wanayochangamotishwa kuitolea ushuhuda amini miongoni mwa watu wanaoishi nao.

Mababa wa Sinodi wanasema, kuna haja ya kuendelea kuimarisha Katekesi kwa njia ya tafakari ya kina, inayowashirikisha pia wasomi na wanasayansi wa Kanisa Katoliki ili imani hiyo iweze pia kumwilishwa katika maisha na tamaduni za watu, kama njia ya kuendeleza mchakato wa utamadunisho. Wakristo wanapaswa kutolea ushuhuda makini wa imani yao kwa Kristo na Kanisa lake, na kamwe wasijisikie wanyonge, kwani wana haki ya kuwa jinsi walivyo. Katekesi iwe ni muhtasari makini wa kile ambacho Mama Kanisa anaamini, anaadhimisha, anaishi katika uadilifu wake na kusali kama njia ya majadiliano na Mwenyezi Mungu, ili kujenga na kudumisha uhusiano mwema na Mungu pamoja na jirani.

Ili mchakato wa Uinjilishaji Mpya uweze kuchukua kasi inayokusudiwa na Mama Kanisa katika mapambazuko ya Millenia ya tatu ya Ukristo, kuna umuhimu wa kuwa na Wainjilishaji Wapya, wenye mwono mpana, mang'amuzi na ufahamu mpana wa imani yao kama ilivyokuwa kwa watakatifu, wafia dini, waanzilishi wa Mashirika, Mababa wa Kanisa, Wamissionari na wadau wengine wa Uinjilishaji kadiri ya Mapokeo ya Mama Kanisa.

Hawa ni mihimili na mfano wa kuigwa hata kwa Kanisa la nyakati hizi. Mababa wa Sinodi wanakazia umuhimu wa kumwilisha tunu msingi za maisha ya Kikristo katika uhalisia wa maisha, kwa njia ya ushuhuda makini, maombezi ya watakatifu na hija katika maeneo yenye mguso na mvuto wa kiimani. Mambo yote haya ni msaada mkubwa katika azma ya Uinjilishaji Mpya ndani ya Kanisa.

Maendeleo ya sayansi na teknolojia, kuyumba kwa uchumi wa kimataifa pamoja na kuporomoka kwa misingi ya maadili na utu wema, kumepelekea mahangaiko makubwa kwa watu wengi duniani, kiasi cha kujikuta watu wanaogelea katika dimbwi la umaskini wa kipato kutokana na ukosefu wa fursa za ajira. Hii ni changamoto kwa Mama Kanisa katika azma ya Uinjilishaji Mpya kuendeleza majadiliano ya kitamaduni na kiuchumi, kwa kuzingatia maadili, utu wema, haki msingi za binadamu pamoja na kupania kutafuta na kulinda mafao ya wengi ndani ya Jamii.

Maendeleo ya sayansi na teknolojia yasiwe ni chanzo cha kinzani za kijamii, kutokana na kuongezeka kwa idadi kubwa ya maskini. Kanisa daima lijitahidi kuonesha mshikamano wa dhati na waathirika wa matukio kama haya, ili hata katika ugumu wa maisha yao, waweze kuonja huruma na upendo wa Kristo.

Katika mapambazuko ya Millenia ya tatu ya Ukristo, Kanisa kwa namna ya pekee, linaalikwa kuutangaza na kumwilisha: haki, amani, upendo na mshikamano wa Kristo kwa waja wake kwa njia ya maendeleo endelevu yanayogusa mahitaji ya mtu mzima: kiroho na kimwili. Wainjilishaji watambue na kuthamini utajiri mkubwa unaofumbatwa katika Mafundisho Jamii ya Kanisa kama nyenzo msingi wa Uinjilishaji Mpya unaopania kuyatakatifuza malimwengu kwa njia ya ushuhuda makini wa imani ya Kikristo.

Mkazo utolewe kwa Majandokasisi, Watawa na Waamini walei, ili waweze kuyafahamu Mafundisho Jamii ya Kanisa. Lengo ni kujenga na kukuza utakatifu wa kijamii, katika ulimwengu unaoendelea kuogelea katika dhana ya ukanimungu. Mwalimu Julius Kambarage Nyerere ni kati ya mifano bora ya kuigwa kwenye medani za siasa.

Uinjilishaji Mpya ujikite katika kulisoma, kulifafafanua na kulimwilisha Neno la Mungu kuanzia katika ngazi ya mtu mmoja mmoja, familia, Jumuiya ndogo ndogo za Kikristo na Kanisa katika ujumla wake, ili kuzima kiu na njaa ya uwepo wa Mungu katika maisha ya watu. Ikumbukwe kwamba, kutangaza Habari Njema, ni dhamana ya kila Mkristo na wala si kwa Makleri na Watawa peke yao. Waamini walei wanaalikwa kuitangaza Injili ya Kristo kwa njia ya ushuhuda wa maisha, kama sehemu ya mchakato wa kuyatakatifuza malimwengu.

Uinjilishaji Mpya uimarishe umoja na mshikamano miongoni mwa wafuasi wa Kristo, kwa kukuza na kuendeleza ari na mwamko wa kimissionari, daima waamini wakiwa tayari kujitoa bila ya kujibakiza kwa ajili ya kumtangaza Kristo hadi miisho ya dunia. Umoja na mshikamano ni changamoto kubwa kutoka katika Mtaguso Mkuu wa Pili wa Vatican. Maneno yaendane na vitendo vinavyoleta mvuto na mguso katika maisha ya watu, kwa kujikita katika wongofu wa ndani na utakatifu wa maisha.

Ulimwengu mamboleo unatawaliwa kwa kiasi kikubwa sana na maendeleo ya sayansi na teknolojia ya habari, hii ni fursa kubwa inayopania kuufanya ulimwengu kuwa kama kijiji. Njia hizi za mawasiliano zinaweza pia kutumiwa na Mama Kanisa kwa ukamilifu zaidi katika dhamana ya Uinjilishaji Mpya. Jambo la msingi ni kuhakikisha kwamba, Kanisa linawaandaa watu kutekeleza utume huu nyeti kwa kuzingatia Mafundisho Tanzu na Mapokeo ya Kanisa.

Yesu ni kiini cha Uinjilishaji na Habari Njema ya Wokovu inayopaswa kutangazwa hadi miisho ya dunia. Familia za Kikristo ziwe ni vitovu vya Uinjilishaji Mpya, kwa kukazia pia majiundo makini na endelevu kwa wanandoa watarajiwa. Waamini wajenge utamaduni wa majadiliano ya kiekumene katika maisha ya sala, huduma na mshikamano ili dunia iweze kumwamini Kristo aliyeteswa, akafa na kufufuka kutoka katika wafu.

Mababa wa Sinodi wanasema, kuna haja ya kuangalia tatizo la vijana wengi wanaokimbilia mijini wakitafuta nafuu ya maisha, kwani hawa pia wanahitaji kuinjilishwa na wakisha injilishwa, basi wawe pia ni vyombo vya uinjilishaji miongoni mwa vijana wenzao katika hija ya maisha yao. Vijana wakumbuke kwamba, kwa sasa wanakabiliwa na dhana ya ubinafsi, athari za maendeleo ya sayansi na teknolojia ya habari; athari za utandawazi, mawazo mepesi mepesi pamoja na kukosa mifano bora ya kuigwa katika imani. Watambue kwamba, hakuna njia ya mkato katika maisha, bali wanapaswa kwanza kabisa kujifunza kwa juhudi, bidii na maarifa.

Wachungaji na waamini kwa ujumla wao, wawasaidie vijana kukua na kukomaa katika misingi ya imani, matumaini na mapendo kamili. Waamini watambue kwamba, Mungu ni upendo, unaopaswa kumwilishwa katika uhalisia wa maisha.

Huu ndio ushuhuda wa Injili ya Upendo uliotolewa na Mama Teresa wa Calcutta pamoja na umati mkubwa wa waamini wanaoendelea kutoa huduma kwa wagonjwa, wakimbizi, watu wasiokuwa na makazi pamoja na huduma mbali mbali za matendo ya huruma. Lengo ni kuwawezesha watu wote hawa kupata utimilifu wa maisha kama Kristo mwenyewe alivyoahidi. Huu ndio utume unaoendelezwa na Kanisa katika mapambazuko ya Millenia ya tatu ya Ukristo.







All the contents on this site are copyrighted ©.