Wasomi kutoka Afrika msibweteke na maisha ya Ulaya, jifungeni kibwebwe kusoma kwa
juhudi na maarifa, ili mrudi kujenga Kanisa Barani Afrika!
Kardinali Polycarp Pengo, Rais wa Shirikisho la Mabaraza ya Maaskofu Afrika Mashariki
na Madagascar anayehudhuria maadhimisho ya Sinodi ya Maaskofu kuhusu Uinjilishaji
mpya anawaalika wasomi kutoka Afrika waliotumwa na Maaskofu pamoja na Wakuu wao wa
Mashirika ya Kitawa na Kazi za Kitume, kusikiliza kwa makini sauti, nia na lengo la
viongozi hao, ili wajibidishe kusoma kwa: bidii, juhudi na maarifa, ili hatimaye,
wawe tayari kurudi Barani Afrika kusaidia mchakato wa Uinjilishaji wa kina, unaopania
kugusa maisha ya mtu mzima: kiroho na kimwili.
Kardinali Pengo ameyasema hayo
Jumapili iliyopita, tarehe 14 Oktoba, 2012, baada ya Ibada ya Misa Takatifu kwa ajili
ya kumbu kumbu ya Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, muasisi wa Taifa la Tanzania,
iliyokwenda sanjari na kumpongeza Askofu mkuu Protas Rugambwa, aliyeteuliwa hivi karibuni
na Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, kuwa Katibu mkuu msaidizi wa Baraza la
Kipapa la Uinjilishaji wa watu na Rais wa Mashirika ya Kipapa ya Kimissionari. Ilikuwa
ni nafasi pia kwa ajili ya kuwapongeza Mashemasi na Mapadri wapya.
Ibada hii
iliandaliwa na Umoja wa Wanafunzi Wakatoliki wanaosoma na kuishi mjini Roma na kuhudhuriwa
na umati mkubwa wa watanzania wanaoishi hapa Roma.
Kardinali Polycarp Pengo
ambaye pia ni Askofu mkuu wa Jimbo kuu la Dar es Salaam alikuwa na haya ya kusema
kwa wanafunzi na watanzania wanaoishi na kusoma mjini Roma.