Maadhimisho ya Siku ya Kimataifa ya Wanawake Vijijini ni changamoto ya kuwawezesha
kiuchumi ili kukabiliana na changamoto za maisha!
Ndugu msikilizaji wa Radio Vatican, leo makala ya wanawake na maendeleo inakuletea
ujumbe wa Katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa Bwana Ban Ki-Moon katika maadhimisho ya
Siku ya Wanawake Duniani.
Wanawake wa vijijini ndio huzalisha asilimia kubwa
ya chakula, ndio hutunza mazingira kusaidia katika kupunguza hatari ya majanga miongoni
mwa jamii zao. Hii ni kwa mujibu wa katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa Bwana Ban Ki-Moon,
kwenye ujumbe wake wakati wa maadhimisho ya siku ya kimataifa ya wanawake wa vijijini
inayoadhimishwa tarehe 15 Mwezi Oktoba kila Mwaka.
Katibu mkuu amesema kuwa
changamoto kubwa ambayo kwa sasa inawakabili asimilia kubwa ya wanawake walio vijijini
ni kuwa hawana umiliki wa ardhi wanayolima na mara nyingi huwa wananyimwa huduma za
kifedha zinazostahili kuwainua kutoka kwenye umaskini, ili wapate kuishi bila ya usumbufu
wa kupata huduma zikwemo za afya, maji safi na salama. Katibu mkuu wa Umoja wa
Mataifa Bwana Ban Ki-Moon amesema kwamba, anaunga mkono hoja kuhusu wanawake wa vijijini
kuwezeshwa zaidi ilikupambanana na baa la umaskini na njaa, ili kuwajengea watoto
wao maisha yenye matumaini bora kwa siku za usoni. Katibu mkuu ameongeza kuwa, wakati
usalama wa lishe na chakula vinapoimarishwa wanawake wa vijijini huwa na fursa za
kupata ajira na kuwawezesha kukidhi mahitaji ya familia zao.