2012-10-16 11:14:55

Dini zina wajibu wa kukumbusha sheria maadili katika kukuza na kudumisha misingi ya haki ndani ya Jamii


Mheshimiwa Padre Miguel Angel Ayuso Guixot, Katibu mkuu wa Baraza la Kipapa la Majadiliano ya Kidini, akishiriki katika mkutano wa majadiliano ya kidini, uliofanyika hivi karibuni huko Istanbul, Uturuki, uliokuwa unaongozwa na mada "haki na ujenzi wa mfumo mpya wa ulimwengu" alikazia umuhimu wa Jamii kuendelea kujikita katika mchakato wa kumwilisha haki jamii sanjari na uhuru wa kidini kama njia ya kujenga na kuimarisha misingi ya haki, amani na utulivu na kwamba, dini mbali mbali duniani zinayo dhamana kubwa ya kusimamia ujenzi wa haki na amani.

Padre Miguel anabainisha kwamba, dini zinao mchango mkubwa katika kukuza na kudumisha majadiliano katika Jamii ya watu, ili kwa pamoja, waweze kukabiliana na changamoto zinazoendelea kujitokeza katika ulimwengu wa sayansi na teknolojia. Dhana ya amani na jamii ni tema zinazofumbatwa katika maisha ya kiroho ndani ya dini mbali mbali. Kanisa Katoliki kwa kadiri ya Mapokeo yake, linatambua na kuthamini umuhimu wa haki kama sehemu ya mchakato wa mwanadamu kufikiri, kwa waamini, wasioamini na watu wote wenye mapenzi mema.

Hii ni dhana inayoenzi na kudumisha msingi wa utu wa mwanadamu na kwamba, uwezo wake wa kufikiri ni haki msingi ambayo inapaswa kutetewa na kuheshimiwa na wote, ili kweli haki iweze kutendeka. Serikali zina wajibu wa kutoa haki kwa raia wake na kwamba, kiwango hiki kinapimwa kwa umakini mkubwa kwa njia ya utendaji wake. Serikali zinaposhindwa kutoa haki kwa raia wake, hapo zinapoteza dhamana yake ya kimaadili.

Dhana hii inaonesha kwamba, Serikali, kimsingi zinaweza pia kuwajibishwa kwa kushindwa kutekeleza wajibu wake ndani ya Jamii mintarafu sheria maadili na wala huu si uchaguzi wa kisiasa. Ni changamoto kwa Serikali na Jamii kuhakikisha kwamba, zinatekeleza wajibu wake msingi pamoja na kutoa fursa kwa dini na viongozi wake kuchangia katika ustawi na maendeleo ya watu wao. Dini zina dhamana ya kuendelea kuwa ni sauti ya kinabii kwa wanyonge na wote wasiokuwa na sauti wala uwezo wa kujitetea na wote wanaodhulumiwa katika hali mbali mbali za maisha.

Hii ni sauti ya kinabii, inayohamasisha suluhu ya amani ili haki iweze kupatikana. Ni changamoto pevu kwa Jamii kutafuta daima mafao ya wengi. Kutokana na mantiki hii, dini zinao mchango mkubwa hata katika masuala ya kisiasa, kwa kukazia umuhimu wa sheria maadili kama njia kudumisha haki ujenzi wa Jamii inayosimikwa katika misingi ya haki.







All the contents on this site are copyrighted ©.