2012-10-15 11:35:58

Wenye heri wa kwanza katika maadhimisho ya Mwaka wa Imani watangazwa na Kanisa kwa kuthubutu kuishuhudia imani yao kwa njia ya kifodini!


Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, mara baada ya Sala ya Malaika wa Bwana, Jumapili iliyopita, 14 Oktoba 2012, alimzungumzia Mtumishi wa Mungu Federic Bachstein pamoja na Wanashirika wenzake, kumi na watatu wa Shirika la Ndugu Wadogo, waliouwawa kikatiliki kutokana na msimamo wa imani yao kunako mwaka 1611, waliotangazwa kuwa ni Wafiadini, walioshuhudia imani yao kwa Kristo na Kanisa lake, hata wakathubutu kuyamimina maisha yao. Tukio hili limefanyika huko Prag, Jamhuri ya Watu wa Czech.

Baba Mtakatifu anasema, hawa ni Mashahidi wa Kwanza kutangazwa katika Maadhimisho ya Mwaka wa Imani. Ni wafiadini wanaowakumbusha Wafuasi wengine wa Kristo kwamba, kumwamini Kristo maana yake ni kujiachilia mikononi mwake, kiasi hata cha kuyamimina maisha pamoja na kwa ajili ya Yesu.

Katika tafakari yake, Baba Mtakatifu anaendelea kuwaalika waamini katika maadhimisho ya Mwaka wa Imani, kuwa na ujasiri wa kujadiliana na Yesu, ili aweze kuwaonesha yale anayotaka wafanye zaidi, ili wapate uzima wa milele. Hii ni changamoto kwa watu walio pweke, maskini na wagonjwa, ili katika hija ya maisha yao hapa duniani waweze kuwa ni warithi wa maisha ya uzima wa milele na ahadi kutoka kwa Mwenyezi Mungu.

Amewapongeza kwa namna ya pekee, Waamini na Watu wenye mapenzi mema kutoka Poland waliomiminika kwa wingi kabisa kwa ajili ya kumbu kumbu ya maadhimisho ya Siku ya Yohane Paulo wa Pili, iliyokuwa inaongozwa na kauli mbiu "Mtumishi wa Mungu Yohane Paulo wa Pili ni Papa wa Familia". Amewapongeza kwa moyo wao wa mshikamano na umoja ndani ya Kanisa. Anawaalika waamini na watu wote wenye mapenzi mema, kuhakikisha kwamba, maadhimisho ya Mwaka wa Imani, yanakoleza imani, Injili ya Upendo na kutafuta daima mapenzi ya Mungu katika hija ya maisha yao hapa duniani.







All the contents on this site are copyrighted ©.