Hotuba ya Rais Jakaya Kikwete wakati wa kumbu kumbu ya Baba wa Taifa Mwl. Julius Kambarage
Nyerere
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican inapenda kukuletea hotuba ya Rais Jakaya Kikwete
wa Tanzania wakati wa kuhitimisha Mbio za Mwenge kama sehemu kumbu kumbu ya Mwl. Julius
K. Nyerere pamoja na kufunga rasmi wiki ya vijana kitaifa. Rais Kikwete pamoja na
mambo mengine amejadili kwa kina kuhusu kumbu kumbu ya Baba wa Taifa, Mwl. Nyerere,
mabadiliko ya Katiba, ugonjwa wa Ukimwi, dawa za kulevya, rushwa, kilele cha wiki
ya vijana kitaifa, maji mkoani Shinyanga pamoja na bei ya pamba. Kilele cha maadhimisho
haya kimefanyika hapo tarehe 14 Oktoba 2012, huko Mkoani Shinyanga. Ninakusihi ujitaabishe
kujipatia mahudhui yaliyomo kwa kina na mapana.
Ndugu wananchi;
Naomba
nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu, mwingi wa rehema, kwa kutujalia uzima na kutuwezesha
kukutana tena mwaka huu kuadhimisha kilele cha Mbio za Mwenge, kumkumbuka Baba yetu
wa Taifa, na Wiki ya Vijana. Naungana na viongozi waliotangulia kuwashukuru viongozi
wa Mkoa wa Shinyanga pamoja na wananchi wote wa mkoa huu kwa mambo mawili. Kwanza
kwa kukubali kuwa mwenyeji wa maadhimisho haya. Ni jukumu kubwa na zito, lakini wenzetu
mmelipokea kwa mikono miwili na kulitekeleza kwa ufanisi mkubwa. Asanteni sana. Pili,
nawashukuru kwa mapokezi mazuri. Naomba radhi kwa kushindwa kufika jana kutokana
na matukio yaliyotokea Dar es Salaam.
Namshukuru pia Mheshimiwa Dkt. Fenella
Mukangara, Waziri wa Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo na Mheshimiwa Zainabu Omari,
Waziri mwenzake kutoka Zanzibar kwa kunialika kuja kuungana nanyi na Watanzania wengine
popote walipo kushiriki kwenye maadhimisho haya adhimu kwa taifa yanayofanyika hapa
Shinyanga mwaka huu.
Ndugu Wananchi;
Nawapongeza pia Mawaziri,
Naibu Mawaziri, Wakuu wa Mikoa na Wilaya pamoja na watumishi wote wa Serikali ya Muungano
na Serikali ya Mapinduzi Zanzibar, bila kuwasahau wajumbe wote wa kamati mbalimbali,
walioshiriki katika kuratibu mbio za Mwenge wa Uhuru mwaka huu. Mipango yao mizuri
na umakini wao katika utekelezaji ndio imewezesha Mbio za Mwenge wa Uhuru mwaka huu
kufanyika nchi nzima kwa mafanikio makubwa. Hongereni sana.
Ndugu Wananchi;
Kwa
namna ya pekee nawapongeza kwa dhati vijana wetu waliokabidhiwa jukumu la kukimbiza
Mwenge wa Uhuru kitaifa mwaka huu. Wamefanya kazi kubwa na nzuri. Mwenge wameufikisha
salama, unang’ara kama walivyokabidhiwa. Pia, wamefikisha ujumbe wa Mwenge kwa ufasaha
mkubwa. Nimeambiwa mbio za mwaka huu zimefana sana. Kila mahali Mwenge wa Uhuru
ulipokelewa vizuri na wananchi walijitokeza kwa wingi kushiriki katika shughuli za
Mwenge ikiwa ni pamoja na shughuli mbalimbali za maendeleo.
Napenda kuchukua
nafasi hii pia kuwapongeza wananchi wote walioshiriki kwa namna moja au nyingine kufanikisha
Mbio za Mwenge wa Uhuru mwaka huu. Hamasa yenu inatupa nguvu na kutufanya tuongeze
bidii zaidi ya kuboresha Mbio za Mwenge miaka ijayo. Navipongeza sana vyombo vya habari
nchini kwa kuwa pamoja nasi katika kutangaza msafara wa Mwenge na kuwahimiza wananchi
washiriki kwenye za Mbio za Mwenge wa Uhuru. Wenzetu hawa wametusaidia sana kufikia
malengo yetu. Asanteni sana.
Kumbukumbu ya Baba wa Taifa
Ndugu
wananchi;
Kama nilivyosema awali, pamoja na kuwa ni Kilele cha Mbio za Mwenge
wa Uhuru, siku ya leo pia tunaadhimisha miaka kumi na tatu tangu Baba wa Taifa Mwalimu
Julius Kambarage Nyerere alipotangulia mbele ya haki. Miaka hiyo ni mingi kwa mwanadamu
kusahaulika baada ya kufariki, lakini siyo hivyo kwa Baba wa Taifa, Mwalimu Julius
Kambarage Nyerere.
Hasahauliki na kamwe hatasahaulika kwa sababu ya mema
mengi aliyoifanyia nchi yetu na watu wake. Ameongoza harakati za kudai uhuru wa nchi
yetu kwa njia ya amani mpaka ukapatikana. Kwa miaka 23 ameongoza juhudi za kujenga
taifa jipya la Tanganyika na baadaye la Tanzania. Ametuachia nchi nzuri ya watu wenye
umoja, upendo, mshikamano, amani na utulivu licha ya watu wake kuwa na tofauti za
rangi, kabila, dini, hali zao za kiuchumi na maeneo watokayo.Na licha ya kuwa nchi
yetu imetokana na nchi mbili kuungana.
Ndugu Wananchi;
Tofauti hizo
miongoni mwa raia wa nchi hii ni sababu tosha ya watu kuwa na migawanyiko, uhasama
baina yao na ukosefu wa amani na utulivu. Bahati nzuri, na kwa mshangano wa wengi,
nchi yetu imekuwa kisiwa cha amani na utulivu. Wahenga walisema “usione vinaelea
vimeundwa”. Hakuna mtu mwingine wa kushukuriwa na kutambuliwa kwa kuifanya hali hiyo
iwe, zaidi ya Baba wa Taifa hayati Mwalimu Julius Kambarage Nyerere.
Alibuni
na kutekeleza Sera nzuri zilizowajumuisha Watanzania wote katika shughuli muhimu zihusuzo
nchi yao bila ya ubaguzi. Sera nzuri zilizohakikisha raia wote wanapata haki zao
za msingi kwa usawa bila ya kubaguliwa kwa sababu ya rangi zao, makabila yao, dini
zao au maeneo watokayo. Sera nzuri zilizopinga na kuzuia dhuluma, unyanyasaji, ukandamizaji
na uonevu dhidi ya raia. Hiyo ndiyo siri ya utulivu na amani ya Tanzania.
Ndugu
Zangu, Watanzania Wenzangu;
Hakuna jambo kubwa na la heshima kubwa tunayoweza
kumfanyia katika kumkumbuka Baba wa Taifa siku ya leo zaidi ya kuzingatia sera hizo
za msingi zilizojenga umoja, amani na utulivu wa nchi yetu na watu wake. Tanzania
ni miongoni mwa nchi chache Barani Afrika ambazo hazizalishi wakimbizi bali tumekuwa
tunapokea wakimbizi. Hivyo basi lazima tuzienzi na kuzidumisha sera hizo kama tunataka
amani na utulivu vidumu. Tusiwape nafasi watu wanaotaka au kufanya vitendo vya kutuvurugia
sera hizo nzuri, wawe ni watu binafsi, kikundi cha watu au vyama vya siasa. Watu
hao hawaitakii mema nchi yetu na watu wake. Tukiwapa nafasi na tukawaendekeza tutaingia
kwenye maangamizi sisi wenyewe.
Nafarijika sana kuona Watanzania wakiendelea
kukataa ushawishi wa kugawanywa kwa rangi, makabila na dini bali wamekuwa wanasisitiza
kuwa wamoja na wenye mshikamano licha ya tofauti zao hizo. Na huo ndiyo ujumbe mkuu
wa Mwenge tangu kuasisiwa kwa wazo la kuwasha Mwenge kabla ya uhuru na kuwepo kwa
Mbio za Mwenge baada ya Uhuru.
Ndugu Wananchi;
Jana kule Dar es Salaam
nilitembelea makanisa yaliyovunjwa na wanaharakati wa Kiislamu kufuatia tukio la kusikitisha
la kijana mmoja kukojolea kitabu kitakatifu cha Waislamu, yaani “Quran Tukufu”. Kijana
huyu alifanya kosa kubwa pamoja na mazingira ya utoto wake na mwenzake. Waislamu
wanayo haki ya kukasirika. Lakini pamoja na kukasirishwa kwao, na wao kuvamia makanisa
matano kuyabomoa, kuharibu vifaa pamoja na magari, haikuwa sahihi hata kidogo. Kijana
huyo hakutumwa na Kanisa wala na mtu yeyote. Ni matokeo ya ubishani wake na mtoto
mwenzake. Isitoshe tayari alikuwa mikoni mwa Polisi kwa hatua zipasazo za kisheria.
Watu kwenda Kituo cha Polisi kutaka wakabidhiwe mtoto yule wamuadhibu wao
haikuwa sawa. Nchi yetu inaongozwa kwa kuzingatia na kuheshimu sheria, tuache sheria
ichukue mkondo wake. Na baada ya hapo watu kuvamia makanisa na kufanya uharibifu
niliouona nalo lilikuwa ni kosa la kusikitisha na lisilokuwa na maelezo yanayotosheleza.
Nilisema jana, na napenda kurudia tena leo kuwa ndugu zangu tujiepushe na matendo
ya namna ile. Hayajengi bali yanabomoa. Hayatoi jawabu kwa matatizo yanayotukabili
bali yanakwaza wahusika, waathirika na jamii kwa ujumla.
Yanaleta ugumu
katika kupata ufumbuzi wa matatizo yenyewe. Isitoshe yanaleta wasiwasi usiostahili
kuwepo katika jamii na nchi kwa jumla. Niliwasihi viongozi wa dini wa pande zote
mbili kujiepusha na jazba na kulipiza kisasi. Niliwaomba Waache vyombo vya sheria
vifanye kazi yake. Yule kijana yuko mikononi mwa Polisi, halikadhalika na wanaharakati
122 wa Kiislamu nao hivyo hivyo.
Kauli Mbiu ya Mbio za Mwenge wa Uhuru
Mwaka 2012
Ndugu wananchi;
Kama tulivyomsikia Mheshimiwa
Waziri akitueleza muda mfupi uliopita, kila mwaka Mbio za Mwenye huwa na ujumbe maalum.
Mwaka huu ujumbe ulikuwa “Sensa ni Msingi wa Mipango ya Maendeleo Yetu, Shiriki Kuhesabiwa
Tarehe 26 Agosti 2012”. Kauli mbiu hii ilikuwa muafaka kabisa kwani kama mtakavyokumbuka
kuwa tarehe 26 Agosti hadi 1 Septemba, 2012 katika nchi yetu kulifanyika zoezi la
Sensa ya Watu na Makazi. Zoezi hilo lilifanyika kwa mafanikio makubwa pamoja na kuwapo
kwa changamoto ndogo na kubwa. Bila ya shaka, Mbio za Mwenge wa Uhuru mwaka huu na
Kauli mbiu yake hiyo imechangia katika mafanikio haya.
Ndugu Wananchi;
Pamoja
na ujumbe huu wa jumla, Mwenge wa Uhuru uliendelea kuwahimiza wananchi kushiriki katika
mambo muhimu kwa mustakabali mwema wa taifa letu na jamii. Miongoni mwa mambo hayo
ni pamoja na wananchi kushiriki katika mchakato wa mabadiliko ya Katiba na kuendeleza
mapambano dhidi ya ugonjwa wa UKIMWI, dawa za kulevya na rushwa. Masuala haya yote
yalielezwa vizuri na viongozi wa msafara wa Mbio za Mwenge na ujumbe uliwafikia walengwa.
Mabadiliko ya Katiba
Ndugu wananchi;
Mwenyekiti
wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba, Mheshimiwa Jaji Joseph Sinde Warioba ametoa taarifa
hivi majuzi kuwa zoezi la kukusanya maoni kutoka kwa wananchi na makundi mbalimbali
linaendelea vizuri. Katika awamu ya kwanza na ya pili, Tume imefanya mikutano 842
katika mikoa 15; miwili ya Zanzibar na 13 ya Tanzania Bara. Katika mikutano hiyo,
watu 517,427 walihudhuria na waliotoa maoni yao moja kwa moja ni watu 29,514 na waliotoa
kwa njia ya maandishi ni 102,404.
Katika awamu ya tatu inayoendelea sasa,
Wajumbe wa Tume wanakusanya maoni katika mikoa tisa yaani miwili ya Visiwani na saba
ya Bara. Kama mambo yataenda vizuri kama ilivyo sasa, huenda Tume ikamaliza kazi
ya kukusanya maoni mwezi Disemba, 2012. Baada ya hapo itafuata hatua nyingine ya kuandaa
rasimu ya Katiba. Dhamira yetu ni kuona kuwa katika uchaguzi ujao nchi yetu itakuwa
na Katiba mpya inayokidhi mahitaji ya sasa na miaka mingi ijayo.
Ndugu Wananchi; Naomba
nichukue nafasi hii kumpongeza kwa dhati Mwenyekiti wa Tume Mheshimiwa Jaji Joseph
Warioba, Makamu wa Rais na Waziri Mkuu Mstaafu, Makamu Mwenyekiti Jaji Agustino Ramadhani,
Jaji Mkuu Mstaafu, Wajumbe wote wa Tume pamoja na Maofisa wa Tume kwa kazi nzuri wanayoendelea
kuifanya. Nawaomba waendelee na moyo huo wa kuchapa kazi mpaka watakapokamilisha jukumu
lao kubwa na la kihistoria kwa nchi yetu.
Nawaomba wananchi wa Mikoa iliyosalia
waendelee kujitokeza kwa wingi kama wanavyojitokeza sasa wenzao kutoa maoni yao pindi
wajumbe wa Tume watakapotembelea katika maeneo yao. Watoe maoni yao kwa uhuru bila
woga wala vitisho. Msikubali kutishwa wala kulishwa maneno ya kusema na mtu yeyote.
Msikubali kugeuzwa radio kaseti au santuri ya mtu. Toeni maoni yenu mpendavyo nyie.
Ugonjwa wa UKIMWI
Ndugu wananchi;
Kuhimiza
Watanzania kuendeleza mapambano dhidi ya ugonjwa wa UKIMWI umekuwa ni ujumbe wa kudumu
kwenye Mbio za Mwenge wa Uhuru tangu mwaka 2007. Tumeamua iwe hivyo kwa sababu ya
ukubwa wa tatizo na haja ya kuzidisha mapambano hayo. Huu ni mwaka wa 29 tangu maradhi
ya UKIMWI yalipogunduliwa kuwepo nchini kwa mara ya kwanza. Tangu wakati huyo mpaka
sasa watu wengi wameambukizwa na wanaendelea kuambukizwa. Watu wengi wamepoteza maisha
na wengi wanaugua hivi sasa.
Maradhi haya yamekuwa na gharama kubwa kwa taifa
kwa maana ya tiba, kupoteza nguvu kazi na mzigo wa kulea yatima. Jitihada kubwa
zimekuwa zinafanywa kupambana na maradhi haya na mafanikio makubwa yamepatikana.
Bado jitihada zaidi zinahitajika.
Ndugu Wananchi;
Kuzuia maambukizi
mapya ndilo hasa lengo kuu la mkakati wa kupambana na maradhi haya nchini. Tunataka
walioambukizwa wabaki hao hao tuwashughulikie lakini wale ambao walio salama wabakie
salama. Kwa ajili hiyo, kazi kubwa imekuwa inafanyika kuelimisha umma kuhusu UKIMWI.
Hivi sasa, karibu kila Mtanzania anajua kuwepo kwa ugonjwa wa UKIMWI, jinsi unavyoambukiza
na namna ya kujikinga. Elimu ya kujikinga na UKIMWI tumeielekeza pia kwa watoto wetu
mashuleni ili wapate ufahamu mapema na kujinga. Hivi sasa, inawafikia asilimia 65
ya wanafunzi wa Shule za Msingi na asilimia 80 ya Shule za Sekondari. Elimu kwa vijana
wetu ndiyo matumaini makubwa ya kutokomeza janga hili siku za usoni.
Ndugu
Wananchi,
Pamoja na hayo, tumeelekeza nguvu zetu katika kuwahamasisha Watanzania
kupima afya zao ili kujua kama wako salama au wana maambukizi. Nafurahi kwamba tangu
tuzindue kampeni ya kitaifa ya upimaji UKIMWI kwa hiari, Julai 2007 zaidi ya watu
milioni 14.2 wamejitokeza kupimwa na kuifanya Tanzania kuwa miongoni mwa nchi zinazoongoza
duniani kwa upimaji wa hiari. Kutokana na zoezi hilo, imethibitika kuwa kiwango cha
maambukizi nchini kimeshuka kutoka zaidi ya asilimia 15 miaka ya tisini hadi asilimia
5.7 hivi sasa.
Haya ni mafanikio makubwa sana. Hata hivyo bado watu watano
katika kila watu 100 kuwa wameambukizwa ni wengi mno. Tunataka tufikie siku ambapo
hakuna hata mtu mmoja mwenye maradhi haya. Inaleta faraja kuona kuwa, maambukizi
mapya yamepungua kwa asilimia 25.
Ndugu Wananchi;
Katika zoezi la upimaji
wa hiari linaloendelea, tumeweza kupata sura ya kuaminika zaidi ya watu wenye maambukizi
ya virusi vya UKIMWI nchini. Kati ya hao, asilimia 57 tayari wanapatiwa dawa za kurefusha
maisha na asilimia 43 waliosalia watahudumiwa hali zao za ugonjwa itakapofikia hatua
ya kuhitaji dawa. Jitihada zinaendelea kufanywa kuhakikisha kuwa mahitaji muhimu yakiwepo
ya dawa na fedha yanapatikana.
Napenda kutumia nafasi hii kuwahimiza wananchi
kuendelea kujitokeza kupima kwa hiari. Inasaidia kujua kama uko salama ili ujihadhari
na kama umeambukizwa ujue namna ya kuishi kwa matumaini na kuepuka kuambukiza wenza
wao. Aidha, napenda kuwahakikishia kuwa tumejipanga vizuri, wale wote walioathirika
watapata dawa.
Ndugu Wananchi;
Narudia kuwakumbusha Watanzania wenzangu
kufanya kila wawezalo kujiepusha kupata maambukizi ya UKIMWI. Hili ni jambo linalowezekana
iwapo watu watazingatia masharti yake. Wahenga wamesema penye nia pana njia, haya
shime tuazimie kwa dhati kukataa kuambukizwa virusi vya UKIMWI. Ziko njia kadhaa
za kuambukizwa lakini kubwa zaidi ni ile tunayoijua sote. Kila moja wetu aamue kushinda
udhaifu wa moyo wake, jambo ambalo hatuwezi kusema haliwezekani. Linawezekana. Ndiyo
maana bado sina shaka Tanzania bila UKIMWI inawezekana. Sisi serikalini tutaendelea
kuimarisha jitihada zetu ili kupunguza maambukizi mapya na kuwahudumia vizuri zaidi
walioathirika. Pia naomba tuache tabia ya kuwabagua na kuwanyanyapaa wenzetu walioathirika.
Dawa za Kulevya
Ndugu wananchi;
Taifa letu
liko katika mapambano makubwa na magumu dhidi ya biashara na matumizi ya dawa za kulevya.
Biashara imekuwa kubwa na idadi ya watumiaji imeongezeka sana na maeneo yenye tatizo
hili hapa nchini nayo yameongezeka. Zaidi ya bangi na mirungi, watu sasa wanatumia
dawa za kulevya ngeni kutoka nje kama vile heroin, cocaine, na nyinginezo.
Matumizi
ya dawa za kulevya huambatana na athari mbaya za kiafya, kijamii na kiuchumi. Baadhi
ya athari hizo ni magonjwa mbalimbali yakiwemo magonjwa ya akili, moyo, figo, kifua
kikuu na UKIMWI. Vilevile matumizi ya dawa za kulevya yanasababisha uhalifu kuongezeka,
nguvu kazi muhimu ya taifa kupotea, watoto wa mitaani kuongezeka na vifo vinavyoweza
kuepukika. Kinachosikitisha zaidi ni ule ukweli kwamba waathirika wengi wa dawa za
kulevya ni vijana wakiwemo pia wanafunzi katika shule na vyuo.
Ndugu Wananchi;
Serikali,
kupitia kwa Tume ya Kuratibu Udhibiti wa Dawa za Kulevya, Kikosi Kazi na vyombo vingine
vya dola inaendelea kukabiliana na tatizo hili. Mafanikio ya kutia moyo yameendelea
kupatikana japokuwa bado changamoto zipo nyingi. Kwa mwaka huu 2012 hadi kufikia Agosti,
Tume kwa kushirikiana na Kikosi Kazi na vyombo vingine vya dola imefanikiwa kukamata
kilo 250 za heroin, kilo 150 za cocaine, kilo 45,458 za bangi kavu, kilo 6,215 za
mirungi na kuteketeza ekari 184 za mashamba ya bangi. Aidha, kati ya Januari hadi
Agosti, 2012, watu 44 wakiwemo Watanzania na raia wa kigeni wamekamatwa na dawa za
kulevya za cocaine, heroin na kadhalika na kesi zao zipo Mahakamani.
Napenda
kuwahakikishia Watanzania wenzangu kuwa tutaendeleza mapambano dhidi ya biashara na
matumizi ya dawa za kulevya nchini bila kuchoka. Hatutakubali kushindwa. Hatuwezi
kuacha taifa letu liangamie na kuwa na vijana wengi mazezeta. Hata hivyo ili tufanikiwe
kwenye vita hii, tunahitaji sana ushirikiano wa wananchi wote. Wananchi mnawafahamu
vizuri waagizaji, wauzaji na watumiaji wa dawa za kulevya. Wengine mnaishi nao, marafiki,
jirani, ndugu na hata watoto wenu. Tafadhali pelekeni taarifa mzijuazo kwenye taasisi
na vyombo vinavyohusika ili zifanyiwe kazi na hatua stahili zichukuliwe dhidi ya wahalifu
hao. Tusiwaonee muhali, ni hatari kwa taifa na hasara kwa jamii na familia.
Rushwa
Ndugu
wananchi;
Changamoto nyingine inayolikabili taifa letu ambayo Mwenge wa Uhuru
umekuwa unaimulika ni rushwa. Sote tunafahamu kuwa taifa lolote lile duniani haliwezi
kuendelea bila kudhibiti vitendo vya rushwa na ubadhirifu wa mali ya umma. Rushwa
ni kikwazo kikubwa cha maendeleo ya taifa na utoaji wa haki. Hivyo hatuna budi kupambana
kwa dhati na vitendo vya kutoa na kupokea rushwa nchini mwetu.
Taasisi ya Kuzuia
na Kupambana na Rushwa ndicho chombo cha mstari wa mbele katika mapambano haya. Serikali
inaendelea kuweka mazingira mazuri na kujenga uwezo wa kiutendaji wa TAKUKURU ili
iweze kutimiza ipasavyo wajibu wake. Nafurahi kuwa kazi inakwenda vizuri na mafanikio
yanazidi kupatikana. Idadi ya kesi za rushwa kubwa na ndogo zinazopelekwa mahakamani
imeongezeka.
Pamoja na mafanikio hayo bado tatizo la rushwa lipo hivyo hatuna
budi kuendeleza mapambano kwa nguvu zaidi. Napenda kutumia nafasi hii kukumbushana
kuwa vita hii sio ya Serikali na TAKUKURU peke yake. Ni vita ya kila mtu hapa nchini,
walio raia na wasiokuwa raia wa Tanzania. Narudia kuwasihi watu wote kushirikiana
na Serikali na TAKUKURU kupiga vita rushwa. Uhakika wa mafanikio katika vita hii
utapatikana pale watu watakapokuwa jasiri kukataa kutoa rushwa au kukataa kupokea
rushwa wanapoombwa kufanya hivyo. Mafanikio yatakuwa makubwa zaidi pale watu watakapotoa
taarifa kwa TAKUKURU au vyombo vya dola husika kwa hatua zipasazo kuchukuliwa dhidi
ya wahalifu. Kulalamikia rushwa imezidi bila ya kuwasema waombaji, watoaji na wapokeaji
rushwa haitoshi. Haitasaidia kumaliza tatizo hili ambalo sote tunalolichukia sana.
Wiki
ya Vijana Kitaifa
Ndugu wananchi;
Siku ya leo pia ni
kilele cha Wiki ya Vijana Kitaifa iliyoanza tarehe 8 Oktoba, 2012. Mbio za Mwenge,
ni shughuli ya vijana. Tangu zilipoanzishwa na Baba wa Taifa aliwakabidhi vijana
kukimbiza Mwenge, na kwenye wiki kabla ya kumalizika kwa mbio hizo vijana hupata fursa
ya kufanya na kuonyesha shughuli mbalimbali wazifanyazo. Nafurahi kwamba utaratibu
huu umedumishwa na naomba tuendelee kuudumisha. Hapa Shinyanga programu mbalimbali
za vijana ziliandaliwa ikiwa ni pamoja na maonesho na midahalo, kama sehemu ya kuadhimisha
Wiki ya Vijana. Kabla ya kuja hapa nimepata fursa ya kutembelea maonesho ya vijana
pamoja na ya wadau wengineo katika Viwanja vya Sabasaba mjini hapa. Nimejionea mwenyewe
jinsi vijana wanavyofanya kazi kwa bidii na maarifa kuinua hali zao za maisha na
kuchangia maendeleo ya nchi yao. Maonesho haya yamebainisha wazi kuwa vijana wanao
uwezo wa kulifanya taifa letu kupiga hatua kubwa ya maendeleo katika nyanja mbalimbali
za uchumi na utoaji wa huduma.
Ndugu Wananchi;
Kinachotakiwa kutoka
kwetu, yaani wazazi, Serikali na jamii ni kuwajengea vijana wetu mazingira mazuri
ya kufanya shughuli zao.
Kwa kutambua ukweli huo Serikali imewekeza katika
kuwapatia vijana fursa za elimu na mafunzo ya stadi za kazi. Kadhalika, kuna mifuko
ya kuwasaidia vijana kupata mikopo kutoka Serikalini, taasisi za fedha na kupitia
mashirika yasiyokuwa ya Kiserikali. Natambua kuwa mahitaji ni makubwa kuliko rasilimali
zilizopo. Ahadi yangu kwenu tutaendelea kuongeza mafungu kwa ajili hiyo. Aidha,
tutaendelea kuhimiza vijana kupewa kipaumbele katika fursa mbalimbali zitakazojitokeza.
Napenda kuwahimiza vijana wote nchini wachangamkie fursa zitakapojitokeza na wafanye
kazi kwa bidii na maarifa. Waache uvivu na uzembe, waache kushinda vijiweni na kulalamika
bali wajitume. Mifano ya wenzao wanaojituma ipo hata leo tumeona. Waige mifano hiyo.
Serikali ipo nao bega kwa bega, ipo tayari kuwasaidia.
Maji Mkoani
Shinyanga
Ndugu wananchi;
Niruhusuni nimalizie yangu
hotuba yangu kuzungumzia mambo mawili: Jambo la kwanza ni tatizo la uhaba wa maji
safi na salama Mkoani Shinyanga na Simiyu. Serikali, kwa kutambua hilo, iliamua kuchukua
maji ya Ziwa Victoria na kuyafikisha miji ya Kahama na Shinyanga. Katika mradi huo
uliokamilika mwezi Desemba, 2008 pamoja na kuhudumia Manispaa ya Shinyanga na mji
wa Kahama, vijiji 45 vya mkoa huu na Mwanza vimenufaika. Kazi ya upanuzi wa mradi
inaendelea ili kupeleka huduma ya maji safi kwenye vijiji 104 vilivyosalia.
Katika
mwaka wa fedha 2012/2013 vijiji vinne vya Nyangomango, Isesa, Igenge na Mbalika vimefanyiwa
usanifu na ujenzi wa miundombinu unatarajiwa kuanza hivi karibuni. Vile vile, vijiji
vya Chibuji, Ndambi na Nyang’ohonge vilivyoko wilayani Kwimba viko katika hatua ya
mwisho za kuunganishwa katika mtandao ili viweze kupata huduma hiyo.
Ndugu
Wananchi;
Nyaraka za zabuni zimekamilika kwa ajili ya kupata Mkandarasi wa
kupeleka maji kwenye mji wa Muhunze ambao ni makao makuu ya wilaya ya Kishapu. Hivi
sasa taratibu za kupata fedha za kutekeleza mradi huo zinaendelea. Vile vile, maandalizi
yanaendelea ya kupata Mhandisi Mshauri wa kufanya usanifu wa mradi wa kupeleka maji
kutoka Kahama kwenda Kagongwa hadi Tinde kupitia Isaka na vijiji vya njiani. Mambo
yakienda kama ilivyopangwa kazi inategemewa kuanza mwezi Januari, 2013.
Ndugu
Wananchi;
Serikali imebuni mradi mpya wa kutumia maji ya Ziwa Victoria kutoka
kijiji cha Nasa na kuyasambaza kwenda Miji ya Bariadi, Maswa mpaka Mwanhuzi. Tathmini
ya kumpata Mhandisi Mshauri atakayefanya kazi hiyo imekamilika. Mhandisi Mshauri
anatarajia kuanza kazi hiyo mwezi Januari, 2013. Baada ya hapo tutatafuta fedha za
kutekeleza mradi huo. Hivyo ndugu zangu wa Shinyanga na Simiyu vuteni subira, Serikali
inatambua kilio chenu cha miaka mingi na jitihada za kutafuta ufumbuzi zinaendelea
vizuri. Subira yavuta heri.
Bei ya Pamba
Ndugu
wananchi;
Jambo la pili, ninalotaka kulizungumzia ni tatizo la bei ya zao la
pamba katika msimu wa mwaka huu ulioanza tarehe 2 Julai, 2012 ambao sasa unaelekea
ukingoni. Haukuwa msimu mzuri sana pamoja na mafanikio yaliyopatikana mpaka sasa ya
ununuzi wa pamba. Mpaka sasa jumla ya makampuni 37 yanaendelea kununua na kuchambua
pamba mbegu. Aidha, zaidi ya tani 309,560 za pamba-mbegu zimenunuliwa kutoka Kanda
ya Magharibi. Na zaidi ya tani 1,700 zimenunuliwa Kanda ya Mashariki. Ununuzi bado
unaendelea katika Wilaya mbali mbali ambapo inakadiriwa kiasi cha tani 30,000 za pamba
bado hazijanunuliwa toka kwa wakulima katika Wilaya za Bariadi, Maswa na Meatu.
Ndugu
Wananchi;
Kwa ujumla, ununuzi wa pamba msimu huu ulikabiliwa na changamoto
kubwa ya bei kwa mkulima kuwa ndogo tofauti na mwaka wa jana. Kiini cha tatizo hilo
ni kuporomoka kwa bei ya pamba katika soko la dunia. Mwaka wa jana bei ya pamba katika
soko la dunia ilikuwa Dola ya Marekani 1.45 sawa na shilingi 2,276 kwa ratili wakati
mwaka huu ilianzia senti 83 ya dola ya Marekani sawa na shilingi 1,303 kwa ratili
na iliendelea kushuka. Kwa sababu hiyo bei ya mkulima mwaka wa jana ilikuwa shilingi
1,100 kwa kilo wakati mwaka huu ilikuwa shilingi 660 kwa kilo. Tena, bei hiyo ilifikiwa
baada ya juhudi kubwa iliyofanywa na Serikali ikishirikiana na Chama cha Wanunuzi
wa Wachambuaji wa Pamba, Chama cha Wakulima wa Pamba (TACOTA) pamoja na viongozi wa
siasa hususan Wabunge. Wanunuzi wa pamba walitaka kununua kwa shilingi 525 kwa kilo.
Katika jitihada za kutaka bei iongezeke njia mbalimbali zilifikiriwa. Mojawapo
ilikuwa ile ya Serikali kufidia tofauti ya bei. Njia hiyo ilishindikana kwani ilikuwa
inaibebesha bajeti ya nchi mzigo mkubwa mno ambao haingeumudu. Iwapo ingeamuliwa
iwe hivyo mipango mingi ya maendeleo iliyopangwa ingebidi isimame. Baada ya njia
hiyo kushindikana, ikaonekana tuangalie uwezekano wa kupunguza baadhi ya tozo zilizokuwa
kwenye zao la pamba. Tulikubaliana kupunguza ushuru wa Halmashauri kutoka asilimia
5 hadi 2, faida ya wachambuaji kutoka asilimia 10 hadi 2. Pia, tuliondoa Kodi ya Ongezeko
la Thamani (VAT) ya asilimia 18 kwenye viwanda vya nguo. Hatua hizo ndizo zilizopandisha
bei kutoka shilingi 525 kwa kilo hadi shilingi 660 kwa kilo. Bado bei hiyo ni nafuu
kidogo, lakini ni chini mno ukilinganisha na ile ya mwaka wa jana. Hata hivyo, ni
vigumu kumlazimisha mnunuzi kulipa bei kubwa kuliko ile atakayouzia katika soko la
dunia.
Ndugu zangu, Watanzania wenzangu;
Ni vyema tukatambua kuwa
hatuna uwezo wa kudhibiti bei katika soko la dunia. Kuna miaka huwa nzuri kama mwaka
jana na mingine huwa mbaya kama mwaka huu. Lakini tatizo la bei safari hii limetufundisha
mengi. Kwanza inatupasa tuanze kuchuna bongo kutafuta mfumo mzuri wa kuleta utulivu
wa bei kwa wakulima wakati wa misukosuko mbalimbali ya kiuchumi ndani na nje ya nchi.
Nimeshatoa maelekezo kwa Wizara husika kuanza kufanya kazi hiyo. Pili, kwamba tupunguze
kutegemea mno soko la nje kuuza pamba ghafi na tuanze safari ya kuuza pamba iliyoongezwa
thamani au bidhaa zitokanazo na pamba. Hii ina maana ya kuwa tuwe na viwanda vingi
vya nyuzi, nguo na mavazi hapa nchini vinavyotumia pamba yetu. Jambo hilo litawezesha
wakulima kupata bei nzuri kwa pamba yao bila ya wanunuzi kuathirika vibaya.
Hitimisho
Ndugu
Wananchi;
Kabla ya kuhitimisha Mbio za Mwenge wa Uhuru mwaka huu wa 2012 napenda
kuwapongeza vijana walioshiriki kwenye halaiki. Nawapongeza pia walimu wao. Narudia
pia kuwashukuru wote walioshiriki kwa namna mbalimbali kufanikisha sherehe hizi ambazo
zimefana mno. Kwenu nyote nasema asanteni sana.
Baada ya kusema hayo sasa
natamka rasmi kwamba shughuli za Mbio za Mwenge wa Uhuru, Kumbukumbu ya Baba wa Taifa
Mwalimu Julius Kambarage Nyerere na Wiki ya Vijana Kitaifa kwa Mwaka 2012 zimefikia
kilele chake.
Mungu Ibariki Afrika Mungu Ibariki Tanzania Asanteni sana