2012-10-13 09:44:28

Askofu Chengula asema: tumethubutu, tumeweza kukusanya kiasi cha sh. mill. 89, sasa tusonge mbele kulitegemeza Kanisa!


Jimbo Katoliki la Mbeya, Tanzania limefanikiwa kuchangisha zaidi ya Sh.Mil.89 katika harambee iliyoendeshwa na kuongozwa na Askofu Evaristo Chengula wa Jimbo Katoliki Mbeya, ikiwa ni sehemu ya mikakati ya kulitegemeza Jimbo, katika miradi mbalimbali ya maendeleo badala ya kutegemea sadaka.

Akizungumza katika ibada ya misa takatifu ya harambee iliyofanyika katika Kanisa kuu la Mtakatifu Anthony wa Padua, Parokia ya Mbeya mjini, Askofu Chengula amewashukuru wote waliojitoa kulichangia kanisa ili liweze kusimama lenye we bila kutegemea misaada,michango na sadaka.

Akizungumza katika hafla fupi ya chakula cha mchana iliyoandaliwa baada ya misa katika ukumbi wa Parokia ya Mbeya mjini hivi karibuni, Askofu Chengula alisema hiyo ni mikakati ya awali ambayo wameiweka na kutokana na mafanikio hayo inaonesha dhahiri kwamba, Kanisa limethubutu na limeweza hivyo kinachotakiwa ni kuendelea kuweka utaratibu huo kwa mwakani, ili kuhakikisha kwamba, Kanisa linajitegemea, ili kuendeleza utume na mchakato wa Uinjilishaji wa kina, unaogusa mahitaji ya mtu mzima: kiroho na kimwili.

Askofu Chengula alisema ni vema kamati hiyo ikaweka utaratibu mzuri wa kuzitumia fedha hizo kwa ajili ya miradi mbalimbali itakayojenga na kuliimarisha Jimbo. Kamati inapaswa pia kutoa taarifa za mapato na matumizi mwakani ili waamini na watu wenye mapenzi mema waweze kupata moyo wa kuchangia zaidi.

"Kumbe tunaweza kama tumethubutu na huu ni utaratibu ambao tumeuanza sasa,kwa hiyo tunaweza kuendelea na tukasonga mbele bila kutegemea mahali popote nje ya kanisa,tulipanga kupata zaidi ya Sh.mil.89 lakini, tunaweza kupata zaidi,"alisema.

Akizungumza kwa niaba ya kamati ya harambee Padre Gabriel Mwakasita alisema kuwa michango hiyo iligawanyika katika ngazi tofauti na kwamba wamefanikiwa kukusanya fedha taslimu kiasi cha Sh.Mil.66.3 na ahadi ambazo zitakamilishwa kuwasilishwa ni kiasi cha Sh.Mil.22.9.

Ametaja kundi lililopo katika daraja la A ni Parokia za Mbeya mjini ambazo zilipangiwa kutoa kila moja kiasi cha Sh.mil.3 na hivyo kupata jumla ya Sh.Mil.18, daraja B ni Parokia za Tukuyu, Vwawa, Kyela, Chunya, Itaka na Chunya waliopangiwa kutoa Mil.2 na hivyo kukusanya jumla ya Sh.mil.10.

Padre Mwakasita ambaye pia ni Paroko wa Parokia ya Mwanjelwa alisema zaidi ya Sh.Mil.13.5 zilipangwa kukusanywa katika Parokia za Mwamabani, Igoma, Itumba, Mlowo, Pinda, Inyala, Igurus, Simike na Kisa ambazo zilipangiwa kutoa kila mmoja zaidi ya Sh.Mil.1.5 na kundi D lilitarajiwa kukusanya zaidi ya Sh.Mil.11.2 kwa kutoa kila mmoja Sh.laki nane.


Mwenyekiti huyo alikuwa akisaidiwa na Katibu wake Edgar Mangasila alisema, Kundi E lilitarajiwa kukusanya zaidi ya Sh.Mil.2.4 kwa kila mmoja kutoa shilingi Laki nne ambalo ni Parokia za Ngawala, Kapalala, Gua Sange, Ipoka, Kambikatoto pamoja na Parokia mpya ya Idiwili.

Aidha alisema Taasisi za elimu na sekondari zilipangiwa kila mmoja kutoa Sh.Mil.5 na hivyo kukamilisha Sh.Mil.14.5,Mashirika ya kitawa yalipangiwa kutoa laki tano kila moja na hivyo kukamilisha kiasi cha Sh.Mil.3.8,vituo vya afya Sh.mil.2.6, mashamba ya jimbo Shilingi laki mbili, Vyama vya Kitume na Jumuiya za Jimbo vilitoa Shilingi laki tano na kukamilisha Sh.mil.9.3.

Hata hivyo, Mwenyekiti huyo alisema kamati iligawa jumla ya kadi 40 kwa waamini na watu maarufu kuomba kuchangia na hivyo wanatarajia wanaweza kuvuka lengo endapo wote watajitoa kulichangia juhudi za Jimbo Katoliki Mbeya kujitegema ili kuwaletea watu wake maendeleo ya kweli.

Baadhi ya waamini walionesha kufurahishwa na mafanikio ya harambee hiyo iliyohusisha Jimbo pekee na kudai kuwa kuna uwezekano mkubwa wa kupata mamilioni ya fedha endapo lingeshirikisha watu mbalimbali wakiwemo viongozi wa vyama na serikali na jamii wakiwemo watu maarufu na mashuihuri, wafanyabiashara na taasisi za dini na binafsi.








All the contents on this site are copyrighted ©.