Tafakari ya kina ya Neno la Mungu iwe ni msaada mkubwa katika kuuishi Mwaka wa Imani
Ni Dominika nyingine mpendwa msikilizaji wa Radio Vatican, kipindi tafakari Neno la
Mungu, tunaposhirikishana upendo usi ona mwisho. Neno la Mungu Dominika ya 28 ya mwaka
B wa Kanisa latualika kuchagua Hekima ya Kimungu, njia ya kurithi uzima wa milele.
Katika somo
la kwanza toka kitabu cha Hekima tunamwona mfalme Suleimani akiitukuza hekima ya kumjua
Mungu ambayo ni mwangaza na njia kamilifu kwa ajili ya kufika mbinguni. Mfalme Suleimani
anaona Hekima, kitu cha thamani kubwa na hivi haiwezi kulinganishwa na kitu chochote
kiwacho hapa ulimwenguni. Hivi, Hekima hiyo ni zawadi ya kumjua Mungu itolewayo na
Mungu mwenyewe pasipo madai yoyote toka kwetu.
Mwaka huu yaani, 2012-2013
Baba Mtakatifu ameutangaza kuwa mwaka wa Imani, na hivi yafaa kufahamu na kutambua
kuwa ni zawadi, ni tunu bora toka kwa Mungu kwa ajili ya zama zetu hizi. Ndiyo hekima
ambayo inatupasa kuichagua kwa unyenyekevu pasipo mashaka. Tunaalikwa katika mwaka
huu kusadiki kina mafumbo yote matakatifu na kwa njia hiyo tutaweza kuuingia mlango
wa heri wa mbinguni. Jambo la Imani ni gumu kumbe lazima liambatane na hekima ya Kimungu
ili liweze kukolea katika maisha yetu.
Katika kuchagua Hekima ya kumjua Mungu
lazima kila mmoja wetu azame kwa undani kabisa katika Neno la Mungu ambalo ni nguzo
mojawapo ya imani yetu. Kwa njia ya Neno la Mungu tutaweza kujua yaliyomo ndani ya
imani yetu na kuyaweka katika matendo. Tunasikia katika somo la pili Dominika hii
kuwa Neno la Mungu ni kali kuliko upanga wowote ule! Ni kali kwa sababu ni hai na
lina uwezo wa kupenya katika mioyo ya watu.
Kumbe, mwaliko ni kulisoma ama
kulisikia na kulisikiliza na kisha kutafakari. Ndiyo kusema katika mwaka huu wa Imani
tunaalikwa kuzama katika kutafakari Neno la Mungu. Tunaalikwa kila siku walau kujisomea
Neno la Mungu na kwa namna hiyo tutakuwa katika mlango wa kukua kiimani na katika
tumaini la kweli kwa Mungu. Neno la Mungu lililo msingi wa imani yetu lazima lizame
mioyoni na lilete mabadiliko na hivi kuzaa matunda.
Mpendwa msikilizaji, Mwinjili
Marko anatupa namna ambavyo tunatakiwa kubadilishwa na Neno la Mungu, ndiyo kusema
kuwa tayari kuacha mambo ya zamani ambayo hayaambatani na mapendo ya jirani, kuacha
kujifungamanisha na mali na utajiri binafsi na badala yake tuambatane na ushirika
wa kimungu yaani kutumia vipaji vyetu kwa sifa na utukufu kwa Mungu na kwa mafaa ya
wengine.
Anatuasa kuwa makini katika kushika amri za Mungu, yaani si kuziorodhesha
na pengine kuzikariri bali kuzitumia kama njia na mlango wa mapendo ya Mungu kwa mwanadamu
na hivi toka pale kupiga hatua katika kutimiza mapenzi ya Mungu. Lazima mmoja wetu
afikiri na kujiuliza je mali na vipaji nilivyonavyo vyanipa nafasi ya kumpenda Mungu
na kumtumikia na kisha kufika mbinguni?
Mpendwa yafaa kuwa kama mfalme Suleimani
ambaye katika kitabu cha kwanza cha Wafalme 3:4-15 yuko Gibeoni akitolea sadaka na
huko anaomba Hekima ya Mungu ili imsaidie kutenda haki na hukumu ya kweli katika kazi
yake ya kutawala taifa la Mungu. Ndivyo wewe mchungaji, Baba na Mama katika familia
unavyopaswa kusali na kuomba mbele ya Mungu. Yote haya tuyafanye kwa Imani matumaini
na mapendo na heri yake ni ya milele.
Ninakualikeni katika wasaa na wakati
huu Dominika ijayo tunaposafiri pamoja katika mwaka wa Imani. Tumsifu Yesu Kristo.
Tafakari
hii imeletwa kwako na Padre Richard Tiganya, C.PP.S.