Hatimaye, safari ya mwisho
ya aliyekuwa Katibu wa Askofu na mshauri wa Jimbo Katoliki la Mbeya, Padre Theodorus
Johannes Maria Slaats wa Shirika la Roho Mtakatifu imefikia kikomo, tarehe 9 Oktoba,
2012; majira ya saa 8.39 baada ya kumhifadhi katika nyumba yake ya milele ndani ya
Kikanisa cha Pango la Bikira Maria. Padre Slaats ambaye wengi
wa waumini na mapadre walizoea kumuita Babu, wengine Padre Silas ama Sailas alikuwa
Paroko wa Kanisa la Roho Mtakatifu, Parokia ya Ruanda, Jimbo Katoliki la Mbeya amefariki
akiwa na umri wa miaka 82 ambapo ibada ya Misa Takatifu ilianza majira ya saa 4.00
asubuhi na kuongozwa na Mhashamu Baba Askofu Evaristo Chengula wa Jimbo Katoliki la
Mbeya. Katika Misa wawakilishi mbalimbali walihudhuria
akiwemo Katibu Mkuu wa Baraza la Maaskofu Tanzania, Padre Anthony Makunde, Mkuu wa
Shirika la Roho Mtakatifu Kanda ya Tanzania, Padre Amandus Kepele, Mwakilishi wa Shirika
hilo kutoka nchini Uholanzi, Padre Harry Tullemans Mkuu wa Mkoa wa Mbeya Bwana Abbas
Kandoro, Mbunge wa Jimbo la Mbeya mjini, Mheshimiwa Joseph Mbilinyi "Sugu", wawakilishi
kutoka Majimbo ya Iringa, Njombe, Dodoma na Sumbawanga pamoja na na wakuu wa Mashirika
ya kitawa ya kike na kiume. Askofu Chengula katika mahubiri yake alisema,
hakuna cha kumpatia Padre Slaats isipokuwa ni kuyaenzi mapendo yake, kuyaendeleza
matendo mema aliyowaachia sanjari na kuendelea kumuombea na anaamini kwa imani na
matumini ndiyo yaliyowafikisha watu wote kumsindikiza katika safari yake ya mwisho
hapa duniani. Amewashukuru wawakilishi kutoka majimbo
ya Iringa, Njombe, Dodoma na Sumbawanga na kwamba wawakilishi kutoka Jimbo la Songea
na Mbinga wameshindwa kufika kutokana na ajali mbaya ya gari iliyotokea tarehe 8 Oktoba
2012 kati ya Njombe na Songea na hivyo kugharimu maisha ya Sr. Gabriel wa Mbinga ambaye
kitaaluma alikuwa ni daktari. "Padre Slaats amelala usingizi wa milele
sasa hatembei, haongei, viungo vyake vimekauka na baadaye tutamrudisha katika udongo…hili
ni fumbo lisilohitajika ambalo binadamu halifahamu kwa undani wake kwani kifo siyo
tabia wala hulka,"alisema. Alisema wakati akiugua na baadaye kuanza
kutembelea kiti cha matairi baada ya kupooza, Padre Slaats aliwahi kumtania Askofu
Chengula kuwa walikuwa na miili mikubwa lakini sasa hatembei tena na kumtaka yeye
(Askofu) naye ajiandae katika safari yake ya mwisho. Alisema
mapato yake na matendo yake mema yatabaki na kuweza kuunda tabia ya watu kwani itabakia
kumbukumbu muhimu katika maisha ya wote kwasababu imani,amani na kusameheana na kudumu
katika kristo ndiyo mwanzo wa maisha ya mbinguni na jambo la furaha uanza na magumu
na hofu ya maisha huku akielekeza kusoma kitabu cha Mwinjili Mathayo 25:34. Askofu Chengula alisema anamfahamu Padre Slaats akiwa Morogoro na baadaye kumteua
kuwa Katibu wake kutokana na matendo yake mema kwani aliishi kama Yesu Kristo kwa
kuwasaidia watu wenye ulemavu, ukoma, wasiojiweza na kila mhitaji aliyemwendea! "Ametufundisha vya kutosha, lakini, tunalishukuru Shirika kwa kutupatia heshima
Jimbo letu kukubali kumzika hapa, kwani kadiri ya katiba yenu mngeweza kutukatalia
lakini tulikubaliana na mawazo yake ya kuomba arudi jimboni baada ya kutibiwa na mkuu
wake wa Uholanzi alimruhusu. "Pili kabla hajafa ndugu zake walikuja na
kuzungumza naye walikubaliana na ombi lake la kuzikwa Tanzania, Jimboni Mbeya ni heshima
kubwa na shukrani kwa walio mlea nchini Uholanzi…Padre Slaats Mkaribie mungu na usisahau
wenzako tupo nyuma yako tunakuja usije ukafunga komeo la mlango huko mbinguni,"alihitimisha
Askofu Chengula kwa majonzi makubwa. UJUMBE BARAZA LA MAASKOFU
TANZANIA (TEC). Akitoa salamu za pole kwa Askofu Chengula,
Katibu Mkuu wa Baraza la Maaskofu Tanzania, Padre Anthony Makunde alisema kwa niaba
ya Rais wa Baraza la Maaskofu, Askofu Ngalekumtwa na Askofu mkuu wa Jimbo kuu la Songea,
Norbert Mtega wamempa pole sana na kwamba kutokana na majukumu ya kuzika masalia ya
mwadhama Kardinali Lugambwa Bukoba wameshindwa kufika vivyo hivyo kwa Askofu Mtega
kutokana na ajali iliyochukuwa maisha ya Mkuu wa Shirika la watawa wa kike Jimbo la
Mbinga. Padre Makunde alisema Padre Slaats alikuwa
hazina kubwa ya Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania (TEC), kwani angeweza kusema
alikuwa ni maktaba ya TEC na hasa pale zilipokuwa zikihitajika kumbukumbu za Kanisa
Katoliki za miaka ya 1912 hadi 1972 aliweza kuzipata katika maktaba yake. "Katika kukamilisha historia na kuadhimisha miaka 40 ya AMECEA sisi kama Baraza
hatukufaulu kupata historia yake lakini Baba Slaats alikamilisha kila kitu na sasa
tunapoelekea miaka 100 ya Baraza historia yote tangu mwaka 1912 hadi 1972 ni kazi
ya mikono yake…tuliipata toka kwake na sasa ametuachia kazi ya kuanzia mwaka 1972
hadi sasa tunaendelea kukamilisha,’alisema. UJUMBE KUTOKA UHOLANZI Padre Harry Tullemans kutoka Shirika la Roho Mtakatifu parokia
ya Oeffelt nchini uholanzi alisema alikuja nchini Tanzania katika Jimbo la Mbeya ikiwa
ni miezi minne imepita tangu amlete Padre Slaats aliyekataa kubakia ulaya na kuamua
kuja kufia Afrika, Tanzania, Jimboni Mbeya. "Daktari wake alimshauri
akiwa Ulaya kuwa hasirudi Afrika hataweza kufika na badala yake atafia ndani ya ndege
lakini ‘ujeuri’ wake alikataa akasema nitaenda kwa sababu hapa (Uholanzi)ni nyumbani
nilipozaliwa lakini hata huko ni nyumbani kuna ndugu, wazazi, watoto na marafiki pia
kwa hiyo aliamua kurudi nami nilitumwa kumsindikiza na leo nimerudi akiwa ameshakufa,’alisema
Padre Harry. Alisema ametumwa kuwakilisha Shirika kutokana
na mapadre walio wengi kuwa wazee kama alivyokuwa marehemu lakini wanamsubiri siku
ya jumamosi ijayo katika ibada ya misaa takatifu maalum kwa ajili ya kumuombea Padre
Slaats ambayo itakuwa ni misa ya kipekee. "Wananisubiri mimi na
porojo zangu na jicho kubwa (akimuelekeza video shooter),tutakwenda kuonyesha kila
kitu kilichotokea hapa leo na wiki ya kesho wataona mambo makubwa na watashangaa imani
yenu kubwa na mlivyojitokeza kumsindikiza mpendwa wenu." UJUMBE
KUTOKA SHIRIKA LA ROHO MTAKATIFU KANDA YA TANZANIA Mkuu wa shirika la roho mtakatifu Tanzania Padre Amandus Kapele alisema marehemu
padre Slaats aliishi kwa upendo na mapadre wenzake na watawa na hivyo hakuweza kufahamika
kuwa ni wa kutoka shirika gani na atakumbwa kwa mambo yake mema mengi ikiwemo mwaka
1958 ni miongoni mwa mapadre vijana waliounga mkono jitihada za ukombozi wa Taifa
zilizofanywa na Mwalimu Julius Kambarage Nyerere za kupigania uhuru wa Tanzania enzi
za chama kimoja cha TANU. Alisema Padre Slaats pia alikuwa miongoni
mwa mapadre waliounga mkono ‘Africanization’ kuwataka mapadre waafrika kupewa nafasi
ya kuongoza, hivyo atakumbukwa kwa mengi aliyoyafanya kwa taifa la Tanzania,watanzania,waumini
na watawa wenzake ikiwemo na kutunza kumbukumbu na vifaa vya makumbusho. UJUMBE WA SERIKALI Mkuu
wa Mkoa wa Mbeya, Abbas kandoro amemuelezea Padre Slaats kuwa alikuwa ni kiongozi
mwenzao aliyekuwa na sifa nyingi za uongozi kwani aliipenda injili na watu wote waliwaongoza
kwa kulitumikia kanisa kwa moyo wake wote. Alisema watamkumbuka padre huyo
kwa mchango wake mkubwa katika kuiongoza jamii ya mkoa wa Mbeya kwani hakuwaunganisha
waumini pekee bali wananchi wote kwa sababu alijuwa kanisa ni jamii iliyo pana na
hivyo kila mmoja kwa nafasi yake amtendee haki kwa kuwayaendeleza aliyoitendea jamii. Alisema kama serikali anatoa pole kwa Askofu,mapadre,watawa wa kike na kiume,waumini
na wanambeya kwa ujumla kwa kuondokewa na kiongozi,hodari,shupavu,mpenda watu. MBUNGE WA JIMBO LA MBEYA MJINI Mbunge
wa jimbo la Mbeya mjini kupitia tiketi ya Chama kikuu cha upinzani cha Demokrasia
na Maendeleo (CHADEMA), Joseph Mbilinyi ‘Sugu’ ambaye pia ni mwanamuziki wa miziki
ya kizazi kipya yeye kama mtoto aliyekulia Parokia ya Ruanda walizoea kumuita Padre
Slaats: babu na rafiki. Mimi nimempoteza rafiki yangu kwa sababu
nilikuwa ninampotembelea hata nilipopata ubunge alikuwa akinikosoa na kuniambia hapa
Chama chenu kimekosea na hapa mmefanya vyema na hakuwa akiniita mbunge bali aliniita
‘MCHADEMA’…Jumapili ya tarehe 16 Septemba 2012 nilimtembelea kumtakia hali na tulizungumza
naye kwa kweli ni pigo kwa Jimbo ni pigo kwa watanzania wote,"alisema. Mbunge sugu ambaye pia alishiriki katika mkesha wa kumuombea Padre Slaats uliofanyika
katika Kanisa la Roho Mtakatifu, Parokia ya Ruanda, alitoa rambi rambi mifuko 20 ya
Saruji kwa ajili ya kujengea kaburi la Padre Slaats. Katika
safari hiyo ya mwisho maelfu ya watu walijitokeza kumzika kutoka maeneo mbalimbali
ndani na nje ya Mkoa wa Mbeya huku kwaya zikiimba nyimbo za kabila la kiswafwa ambazo
inadaiwa alipenda sana kuzisikiliza na kuziimba huku wao wakimwita mwene(chifu). Hivyo ndivyo nyota ya Padre Slaats ilivyozima ghafla katika uso wa dunia bali
tunaamini kiroho yupo nasi daima.raha ya milele umpe ee! bwana na mwanga wa milele
umwangazie apumzike kwa amani padre Slaats amina. HITIMISHO LA ASKOFU
CHENGULA Hata hivyo Askofu Chengula amehitimisha
kwa kumshukuru Mkuu wa Mkoa wa Mbeya,Abbas kandoro na Mbunge wa Jimbo la Mbeya mjini
Joseph Mbilinyi ‘Sugu’ambaye ni mwamini wa Kanisa la Ruanda kwa kushiriki katika maziko
hayo na amewataka viongozi wa chama na serikali kushirikiana na kanisa siyo katika
shida tu bali hata katika mazuri. "Ninawashukuru Mkuu wa
Mkoa na Mbunge na viongozi wa madhehebumbali mbali, ninakumbuka Mkuu wa Mkoa ulinisaidia
sana katika kuhakikisha shule ya sekondari ya St.Francis haifungwi wakati wa mgogoro
na leo umefika katika kifo, tushikamane mikono hata wakati wa raha pia, Mbunge tuombeane
muongoze vizuri,msitusahau wapiga kura wenu mtukumbuke katika kutuletea maendeleo,"alisema. Askofu Chengula alisema Mapadre na Masista ni jukumu lao kuongea na viongozi
wa vyama na serikali katika kuwasaidia na kuwaunganisha na wananchi bila kujali imani
za kidini wala itikadi za kisiasa,rangi wala kabila,"nanyi wa madhehebu asante sana,msiwe
na wasi wasi Padre Slaats amekwenda kwa mungu." |
All the contents on this site are copyrighted ©. |