2012-10-11 10:37:56

Chuo Kikuu cha Wasalesiani kufungua Mwaka wa Masomo 2012- 2013: kwa kutafakari juu ya ushirikiano wa kimataifa!


Mheshimiwa Professa Andrea Riccard, Waziri wa Ushirikiano wa Kimataifa nchini Italia, anatarajiwa kuwa mgeni rasmi katika maadhimisho ya ufunguzi wa Mwaka wa Masomo, kwa mwaka 2012- 2013, Chuo Kikuu cha Kipapa cha Wasalesiani, kilichoko mjini Roma, hapo tarehe 16 Oktoba 2012 majira ya asubuhi. Tukio hili pia litahudhuriwa na Mheshimiwa Padre Pascual Chaves Villanueva, Mkuu wa Shirika la Wasalesiani wa Don Bosco.

Professa Andrea Riccard anatarajiwa pia kutoa hotuba ya kufungua mwaka wa masomo pamoja na medali kwa majaalimu na wanafunzi waliopeta katika nyanja mbali mbali za masomo na taaluma katika mwaka wa masomo uliopita. Itakumbukwa kwamba, Professa Riccard, kunako mwaka 1968 alianzisha Jumuiya ya Mtakatifu Egidio, ambayo kwa sasa imeenea katika nchi sabini duniani. Ni Jumuiya inayopania kudumisha na kuendeleza ushirikiano wa kimataifa hasa zaidi katika mchakato unaopania kudumisha misingi ya haki, amani na upatanisho wa kitaifa.

Professa Andrea Riccard amechangia kwa namna ya pekee katika harakati za kupatanisha mataifa mbali mbali yaliyojikuta yakiingia katika kinzani na migogoro yakivita. Anakumbukwa sana kutokana na mchango wake uliosaidia kufanikisha utiaji wa sahihi wa mkataba wa amani nchini Msumbiji, ambao kwa sasa unasherehekea miaka ishirini, changamoto ya kukuza na kudumisha misingi ya uhuru na demokrasia kama wanavyohimiza Maaskofu Katoliki kutoka Msumbiji. Amesaidia harakati za amani huko Guatemala, Pwani ya Pembe na Guinea.

Ni mwandishi maarufu wa vitabu na kati ya vitabu vyake ni kile cha Wasifu wa Mwenyeheri Yohane Paulo wa Pili, kilichochapishwa katika lugha nane za kimataifa nchini Italia, kunako mwaka 2011.







All the contents on this site are copyrighted ©.