Jubilee ya miaka 50 ya uhuru wa Uganda na changamoto zake!
Askofu mkuu Cyprian Kizito Lwanga wa Jimbo kuu la Kampala Uganda, ameiomba Serikali
ya Uganda wakati huu inapoadhimisha Jubilee ya miaka 50 tangu ilipojinyakulia uhuru
wake kutoka kwa Waingereza, kuwaachia huru wafungwa wote wa kisiasa bila masharti.
Askofu mkuu Lwanga ameyasema hayo, Jumapili iliyopita wakati wa mahubiri yake
kwenye Kanisa kuu la Rubaga. Anasema, tukio hili linaweza kuonesha kwa namna ya pekee
mchakato unaopania kujenga na kuimarisha amani ya kweli, upatanisho wa kitaifa sanjari
na haki.
Kuna baadhi ya wafungwa wa kisiasa ambao wanaendelea kutumikia vifungo
vyao kinyume cha haki msingi za binadamu. Kwa sasa Serikali ya Uganda inakabiliwa
na changamoto kubwa kutokana na matumizi mabaya ya madaraka walioyokabidhiwa na umma;
uvunjifu wa haki msingi za binadamu, kuporomoka kwa sekta ya elimu hali inayopelekea
ongezeko kubwa la idadi ya watu wasiojua kusoma wala kuandika; rushwa na ufisadi.
Askofu
mkuu Lwanga anaichangamotisha Serikali ya Uganda kuhakikisha kwamba, inaipatia ufumbuzi
wa kudumu migogoro yote ya ardhi inayoendelea kufuka moshi nchini humo kwa sasa. Kanisa
Katoliki pia limejikuta likijitwalia maeneo makubwa ya ardhi, wakati ambapo kuna umati
mkubwa wa Wananchi wa Uganda wanaoendelea kuogelea katika dimbwi la umaskini, ujinga
na maradhi.
Anasema, mustakabali wa wananchi wa Uganda bado uko mikononi mwa
Waganda wenyewe, changamoto na mwaliko wa kusahau ya kale na kuanza kuganga yaliyopo
na yale yajayo mbele yao, kwa imani na matumaini makubwa zaidi. Kilele cha maadhimisho
ya Jubilee ya miaka 50 ya uhuru wa Uganda ni tarehe 9 Oktoba 2012.
Sherehe
hizi zimehudhuriwa na viongozi wa Serikali kutoka nchi mbali mbali Barani Afrika.