2012-10-08 12:48:29

Wanandoa wenye ugumba, kubalini kuupokea mpango wa Mungu katika maisha yenu!


Ndugu msikilizaji wa Radio Vatican, napenda kukualika tuendelee tena na tafakari yetu ya juma lililopita kuhusu matatizo yatokanayo na ugumba, ila leo tukazie zaidi ushauri tunaoweza kuwapatia wanandoa wagumba. RealAudioMP3
Kanisa linaposikitika na wale wanandoa wagumba, linawasihi wapokee mipango ya Mungu kwa matumaini kama katika hali ya kawaida haiwezi kutibika bila kuvuruga muungano wa tendo la ndoa na uzazi. Hili liwasaidie wazazi kukumbuka daima kuwa mtoto ni zawadi toka kwa Mungu. Wao ni washiriki katika mpango huu lakini hawana madaraka ya mwisho kuhusu mtoto. Ni katika misingi hii Kanisa halitabadilisha uamuzi wake kuhusu kuhusu uharamu watoto wa kutengeneza ndani ya maabara.
Kanisa linawaalika wanandoa wagumba wajifunze kuasili (adopt) watoto hasa wale wasio na wazazi rasmi wa kuwalea kama wanaoishi katika mazingira hatarishi. Wapo watoto wengi waliopo kwenye mazingira magumu ya kiuchumi, kijamii na kiroho wakati huo huo, wapo wazazi wagumba wenye hali nzuri za kiuchumi na kijamii ambao wangeweza kuwaasili. Hata hivyo kuasili watoto kunapaswa kuendana na taratibu za kisheria zilizokubaliwa na jamii ili kuondoa ukatili unaweza kujitokeza kwa watoto hawa na kujenga mahusiano mazuri kati ya waliokuwa wazazi wao na wale wazazi wao wapya.
Wana-ndoa wagumba wanaalikwa pale inapowezekana wajiingize zaidi katika huduma za upendo kwa kuanzisha: vyama vya kitume kwa ajili ya malezi kwa watoto wanaoishi katika mazingira hatarishi; vikundi au asasi za kuwahudumia wenye shida mbalimbali hasa watoto, wagonjwa, wazee na wenye shida mbalimbali. Hii itawafanya wasijisikie wapekwe sana pia wawekeze nguvu zao za malezi kwenye makundi mengine kama wanavyofanya baadhi ya makasisi na watawa wanaojitoa kwa njia mbalimbali kuhudumia wahitaji zaidi ndani ya Jamii.
Daima, tukumbe kuwa japo uzazi ni moja ya malengo muhimu ya ndoa lakini pia wanandoa wanaalikwa kutimiza malengo mengine kama umoja na uaminifu katika maisha ya ndoa. Hivyo ugumba usiwe sababu ya kuvuruga umoja na uaminifu huu unaowanufaisha wanandoa. Usiwe sababu za talaka, na mahusiano mengi mabaya kati ya wanandoa kama jamii nyingi duniani zimefanya.
Kutoka Studio za Radio Vatican ni mimi Padre Raphel Mwanga, wa Jimbo Katoliki la Same, Taasisi ya Ndoa na Familia, Chuo Kikuu cha Kipapa cha Laterano- Roma.








All the contents on this site are copyrighted ©.