2012-10-08 15:11:06

Utukufu wa fumbo la Msalaba katika maisha na utume wa Kanisa


Ndugu msikilizaji wa Radio Vatican, Msalaba ni ishara ya mapendo, neema, sala, msamaha na matumaini. Ni kwa sababu hii, Mama Kanisa anaona fahari juu ya Msalaba wa Bwana Yesu Kristo. Kuna baadhi ya watu hawajaelewa vema nini maana na ukuu wa msalaba katika maisha yao.
Ni vizuri kutafakari walau kwa ufupi juu ya msalaba. Utakumbuka pia mwaka jana wakati wa maadhimisho ya ishirini na sita ya siku ya vijana kimataifa, Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, pamoja na zawadi zingine, aliwagawia vijana wote Msalaba. Msalaba una maana gani kwako! Keti kwa utulivu nikupe siri ya Msalaba na ishara ya msalaba.
Msalaba ni ishara ya wokovu wa mwanadamu na wokovu wa ulimwengu mzima. Baada ya dhambi ya wazazi wetu wa kwanza, Adamu na Eva, mwanadamu na ulimwengu mzima ulitekwa katika utawala wa utumwa wa mzushi, shetani. Kristo kwa sadaka yake Msalabani anamuokoa mwanadamu kutoka katika utumwa wa dhambi, kutoka katika utumwa wa kuasi, kutoka utumwa wa kiburi. Wokovu huo unamrudishia mwanadamu na ulimwengu hadhi yake ya awali, nawe unaalikwa kuuenzi na kuuishi msalaba huo ili kushiriki katika kuikamirisha kazi ya ukombozi.
Kama unavyouona msalaba una pembe nne. Hii ni ishara kuwa msalaba umerekebisha mahusiano kati ya Mungu na mwanadamu, viumbe vyote na ulimwengu kwa ujumla. Msalaba unarudisha ule utaratibu wa awali na makusudio aliyokuwa nayo Mungu wakati akiuumba ulimwengu. Msalaba unaurudishia ulimwengu uzuri wake asilia. Lakini ukamirifu wa uzuri na utaratibu huo unategemea kushiriki kwako katika kuuishi msalaba huo wa Kristo.
Kumbe unaalikwa wewe pia kujitoa sadaka kila siku kwa ajilia ya wengine, kwa ajili ya wahitaji, kwa ajili ya kupambana na nguvu za giza, kupambana na mzushi shetani. Jitoe sadaka kama harufu nzuri ya ubani ili kufukuza mbali kila uovu unaoinyemelea dunia. Ishi ukristo wako bila aibu, bila woga. Kabla ya chakula au kabla ya shughuli yoyote anza kwa njia ya msalaba na sala ya kweli na ya rohoni, ili kuiendeleza sadaka ya Kristo na kuutukuza ukuu wa msalaba. Msalaba na ishara ya msalaba viwe ni kinga na ngao yako kupambana na mabaya.
Msalaba ni muhtasari wa historia ya mwanadamu, muhtasari wa historia ya wokovu. Ndio sababu baada ya kuja kwa Kristo wana dunia wamegeuza namna ya kuhesabu nyakati: kabla ya Kristo na baada ya Kristo. hii ni sababu Kristo ndiye kiini cha historia, ndiye mwenye historia na ndiye mwenye kuigawa historia. Kristo anaikamirisha historia ndani yake, katika msalaba wake. “Tazama ya kale yanafanywa kuwa ni mapya”. Kristo anayaweka kwa pamoja na katika mahusiano na utaratibu bora, mambo ya kale, ya sasa na yajayo. Ni katika msalaba wa Kristo tu, ndipo matukio yote duniani yanapata umaana wake.
Msalaba ni ishara ya upendo aliyonao Mungu kumtoa mwanaye wa pekee kukukomboa wewe. Ni ishara ya upendo aliyonao Kristo kukubali kuteseka msalabani kwa unyenyekevu na utii ili kukukomboa wewe. Unapoutazama msalaba, unapopiga ishara ya msalaba, kumbuka kuwa mnyenyekevu na mtii kwa mapenzi ya Mungu.
Msalaba ni kiungo cha wanadamu wote ndani ya Utatu Mtakatifu. Kristo asema “ntakapoinuliwa juu, ntawavuta watu wote waje kwangu”. Mbele ya msalaba wa Kristo umoja kati ya watu unapatikana, umoja kati ya madhehebu na dini mbalimbali unapata mhimili na nguzo thabiti. Msalaba wa kristo unakuvuta wewe na jirani zako wote kuwa pamoja na kuwa na umoja ndani ya Kristo.
Msalaba ni kiti cha enzi cha ufalme cha Kristo aliye Bwana. Ni kiti chake cha enzi maana ni katika msalaba huo ndipo anapomshinda shetani na nguvu zote za giza. Ni katika msalaba hapo ndipo linapozaliwa Kanisa kwa damu na maji. Kupitia nguvu ya msalaba Kristo anautawala ulimwengu. Mbele ya msalaba unapata hukumu yako mwenyewe, ya kuwa ni kwa dhambi zako yeye ametundikwa msalabani hapo, na ni kutoka katika kiti hicho cha msalaba wewe utapata hukumu yako ya mwisho, kwa kuzingatia jinsi ulivyoishi kufuatana na fumbo la msalaba.
Uenzi na kuutukuza ukuu wa Msalaba huo, chanzo, kiini na kilele cha historia ya mwanadamu na wokovu. Mpaka juma lijalo, ni sauti ya kinabii, Celestin Nyanda.









All the contents on this site are copyrighted ©.