2012-10-08 10:29:57

Hali bado ni tete kati ya wachimba migodi Afrika ya Kusini!


Askofu Kevin Dowling wa Jimbo Katoliki la Rustenburg, Afrika ya Kusini anasema kwa sasa hali ni tete sana Afrika ya Kusini kutokana na wachimba migodi wapatao elfu kumi na mbili kufukuzwa kazi na baadhi ya wachimba migodi hao kuamua kuendelea na kazi, kutokana na mgomo usio halali uliofanyika kunako tarehe 12 Septemba, 2012.

Wafanyakazi wote ambao hawakujitokeza kwenye kikao cha nidhamu, kilichoitishwa na Kampuni ya Amplats, moja ya makampuni makubwa duniani yanayojihusisha na uchimbaji wa madini ya Platinum, wamefukuzwa kazi kuanzia tarehe 5 Oktoba 2012. Wafanyakazi wanadai ongezeko kubwa la mishahara kama waliyopewa wenzao kwenye machimbo ya Marikana.

Askofu Kevin Dowling anasema kwamba, Jimbo lake limelazimika kusitisha baadhi ya huduma kutokana na kinzani na machafuko yanayoendelea kujitokeza katika maeneo mbali mbali Jimboni humo. Baadhi ya watu wanaendelea kupoteza maisha yao kutokana na mapambano na vikosi vya ulinzi na usalama katika eneo hilo.







All the contents on this site are copyrighted ©.