Baba Mtakatifu Benedikto XV1, Alhamis amefanya hija katika madhabahu ya Mama Bikira
Maria ya Loreto Italia. Lengo la ziara hii ni kwenda kuomba msaada wa Mama Maria,
ili waamini wa Kanisa wapate ufahamu na mwanga zaidi,katika maana ya uwepo matukio
matatu muhimu ya Kanisa. Matukio hayo ni : Mkutano wa Sinodi ya Maaskofu ya kawaida
ya 13, kwa ajili ya uinjilishaji mpya. Sinodi inayofanyika chini ya Mada: Uinjilishaji
Mpya: Uenezaji wa Imani ya Kikristu, inayoanza 7-28 0ctoba 2012, Kuanza kwa mwaka
wa Imani Oktoba 11, hadi 24 Novemba 2013 na adhimisho la kutimia miaka 50 ya Mtaguso
Mkuu wa Pili wa Vatican dira ya utendaji wa Kanisa. Aidha Papa Benedikto XV1,
amefanya hija hii kwa heshima na kumbukumbu ya miaka 50 kupita, tangu Mwenye Heri
Yohane XXIII, alipofanya hija katika madhabahu ya Loreto 4 Octoba 1962, ambaye nae,
alikwenda kuomba msaada wa Mama Maria na Mtakatifu Francis, ili Mkutano Mkuu wa Vatican
uwe wa mafanikio. Baba Mtakatifu Benedikto XV1, amefanya hija hii kwa njia
ya Helkoputa hadi Loreto tokea Vatican, na mara baada ya kuwasili, majira ya saa nne
, alipokelewa na bahari ya waumini , wakiongozwa na Meya wa mji wa Loreto, Mstahiki
Paolo Niccoletti na pia AskofuMkuu Giovanni Tonucci wa Jimbo Kuu la Prelato. Na
mara baada ya salaam, Papa alikwenda moja kwa moja katika madhabahu, ambako alipokelewa
Jumuiya ya Ndugu Wadogo wa Mtakatifu Francis “Wakapuchini” wakiongozwa na Mkuu wa
Jumuiya, Padre Mauro Johri. Ndani ya Madhabahu hayo, Papa alipiga magoti kusali
na kuabudu Sakramenti Kuu Takatifu Sana na kutolea sala zake kwa Mama Bikira Maria
wa Loreto. Kunako majira ya saa nne na nusu za Asubuhi, aliongoza Ibada ya Misa
katika Uwanja wa Mama Maria wa Loreto. Baada ya Misa aliyoiongoza katika Uwanja
wa Maria wa Loreto, Papa amepata chakula chake cha mchana katika Kituo cha Vijana
cha Yohane Paulo 11, ambako pia amepata nafasi ya kusalimiana na waandaaji wa hija
hii.