Mwaka wa Masomo wazinduliwa Chuo Kikuu cha Mwenge Tanzania
Mahusiano na Mungu na watu wengine ni ya maana licha ya vyeti vyo vyote. Hayo yamesemwa
na Askofu Isaac Amani wa jimbo Katoliki la Moshi. Askofu Amani ameyasema hayo alipokuwa
akifungua rasmi mwaka mpya wa masomo katika chuo kikuu cha elimu cha Mwenge kilichoko
mjini Moshi. Ufunguzi huo umefanyika siku ya Jumatatu tarehe 24 mwezi wa Septemba
2012. Akiongea kwenye Misa Takatifu ya kufungua mwaka mpya wa masomo, Askofu Amani
aliwahimiza wanafunzi wa chuo hicho Kikuu cha Mwenge kuyazingatia mafundisho ya Yesu
Mwalimu ambaye ni Mungu anayeongea nasi katika lugha ya kibinadamu. Elimu hii ya
Yesu ni kama taa inayotusaidia kutembea duniani tukiwa na mwanga wa ufahamu wa Kimungu. Alisema
Askofu Isaac Amani kuwa Neno la Mungu, Yesu, alitwaa mwili na kukaa kati yetu ili
aweze kutufundisha sisi na kwamba sehemu kubwa ya muda wake hapa duniani aliitumia
kwa kufundisha watu juu ya kuhusiana na Mungu na watu wengine. Askofu huo wa Moshi
alisema kwamba Mungu ni uhusiano na kwamba binadamu aliyeumbwa kwa sura na mfano wake
Mungu anazo pia hadhi na heshima na utukufu wa kiMungu; na kwamba mafundisho ya Yesu
humpa mtu mbinu na upeo wa kumjua Mungu mwenye kuiongoza dunia kwa amri zake. Askofu
Amani aliongeza kusema kuwa wajibu wa Kanisa ni kumfunza mwanadamu apate kujijua yeye
mwenyewe na kuijua pia thamani ya elimu ambayo ni chombo cha ukombozi na uhuru wote.
Hivyo basi elimu ya kwanza ni ile ya kumjua Mungu, kuzishika amri zake, na kuusimamia
ukweli. Elimu ingine ni ile ya malezi katika tabia njema na maadili. Ni vyema basi
mwanadamu kunoa akili yake kwa elimu, usikivu, utafiti na ubunifu ili kuweza kuboresha
mazingira yake. Askofu Isaac Amani amewapa changamoto wanafunzi wote wa Mwenge
kujifunza kisawasawa ili kwamba kama Kristo alivyo taa ya dunia, nao pia waweze kuwa
Mwanga wa dunia kufuatana na wito wa Chuo hicho ambao ni Lux Mundi, au Mwanga wa Dunia. Chuo
Kikuu cha elimu cha Mwenge (Mwenge University College of Education) kilianzishwa mnamo
mwaka 2005 na kiko chini ya Baraza la Maaskofu Katoliki wa Tanzania. Chuo hico kinatoa
shahada katika fani mbalimbali yakiwemo masomo ya sayanso na elimu. Wanafunzi wa
Mwenge hutoka kote nchini Tanzania na nchi nyingine barani Afrika.