2012-09-15 09:56:18

Papa safarini Lebanon- Salaam kwa wakuu wa Nchi , na ajibu maswali ya wanahabari


Ijumaa Baba Mtakatifu Benedikto XV1, akipita katika anga za mataifa mbalimbali , alipeleka salaam zake za matashi mema kwa wakuu wa nchi alimopita. Kwa Rais wa Italia, , Mheshimiwa Giorgio Napolitano alisema, ”Mheshimiwa Rais, ninapita katika taifa lako, nikielekea Lebanon kama mhujaji wa amani na umoja. Ambako pia nitawasilisha waraka wangu wa Kitume , juu ya maoni yaliyolewa wakati wa Sinodi ya Maaskofu niliyoiitisha maalum kwa ajili ya kutazama kwa makini , hali ya maisha ya Wakristu katika mkoa wa Mashariki ya Kati na msaada unaohitajika kujenga amani, umoja na matumaini katika mkoa huo.
Papa aliendelea kusema, ataendelea kutolea sala zake, kwa watu wa Italia ili waweze, katika hali ya utulivu na amani, kupambana na changamoto zinazo wakabili nyakati hizi.
Vivyo hivyo, Papa alitoa salaam kama hizo, alipopita katika anga la Ugriki , kwa Rais Enerico na kwa Rais Demetris Christofias wa Cyprus.
Mkutano na wanahabari
Baba Mtakatifu pia akiwa bado safarini alijibu maswali ya wanahabari, mengi yakilenga katika hali za ubabe wa kidini na ghasia zinazo onekana nyakati hizi, Mashariki ya Kati. Wanahabri hao, walitaka kujua kama alikuwa na nia ya kufuta ziara yake baada ya kusikia habari za ghasia hizi mara kwa mara.
Papa alijibu kwamba, hakuna hata mmoja aliye mshauri kufuta ziara yake na wala hakuwa na wazo hilo, katika fikira zake , sababu alijua kwamba, kwa kadri hali inavyozidi kuwa ngumu , ndivyo kunavyokuwa na umuhimu wa kutiana moyo, kujenga umoja na mshikamano wa kidugu na wale walio katika hali za mahangaiko na mashaka.
Na ndiyo maana aliitikia mwaliko wa ziara hii, kwenda kujadiliana na kuzungumzia amani, kukataa ghasia na fujo, na kutafuta jawabu la pamoja katika kukabiliana na matatizo yanayojitokeza.
Papa pia alijibu swali juu ya ongezeko la watu wenye imani kali isiyo vumilia wengine, akisema kwamba utendaji huo ni kuihaini dini, kwa kuwa dini ni mwaliko wa watu kushirikishana kupendana na kuishi kwa amani duniani kote.
Alifafanua , kila binadamu ameumbwa kwa sura na mfano wa Mungu na hivyo ni lazima wote, mmoja kumheshimu mwingine . Na ujumbe mkuu wa dini ni lazima ukemee aina zote za ghasia, hasa zinazo fanyika kwa jina la dini. Kila dini inapaswa kuwa elimisha waumini, kuangaziwa na kutakatifusha dhamiri , kwa ajili ya ukuzaji wa majadiliano, mapatano na amani.
Na alipoulizwa maoni yake juu ya kile kinachoitwa mapambazuko ya nyakati , katika nchi za Kiarabu na udumishaji wa Ukristu katika mkoa huo ambako idadi ya Wakristu ni dogo, alisema, ”katika mtazamo wenyewe, hamu ya demokrasia, uhuru na utambulisho mpya wa Mwarabu, ni mambo mema katika juhudi hizo. Lakini haya yasiwafanye kusahau kipengere cha kuvumiliana mmoja kwa mwingine”. Papa amesisitiza ule ukweli kwamba, uhuru wa binadamu daima ni kushirikishana , na tu, huweza kufanikishwa, kupitia kutembea pamoja katika njia thabiti ya umoja, kushirikishana , kugawa, na kuishi pamoja. Na hivyo watu wote wanapaswa kufanya kila linalowezekana kuikubali dhana ya uhuru na hamu ya uhuru huenda sanjari na uhuru wa kweli bila ya kupuuza uvumilivu na mapatano, vipengere viwili muhimu katika kuwa na uhuru kamili.
Na kwa upande wa Wakristu kuikimbia Mashariki ya Kati, na hasa Syria na Iraki, Papa amesema, ni lazima kufanya kila linalowezekana kusaidia Wakristu hawa kubaki katika nchi yao ya kuzaliwa. Na cha msingi zaidi ni kusaidia kusitisha ghasia zinazoendelea, ambazo katika ukweli, si kwamba ni madhulumu kwa Wakristu tu lakini pia kwa Waislamu na watu wengine wenye mapenzi mema katika mkoa huo. Na hivyo inakuwa muhimu, kueneza ujumbe wa amani na maelewano kati ya watu wa tamaduni mbalimbali kwa kuwa wote ni wana wa Mungu.
Papa pia alitoa wito wa kusitishwa kwa upelekaji wa silaha katika maeneo yenye machafuko. Aliuita upelekaji wa silaha huo, kuwa ni dhambi kubwa. Ni lazima kukubali kuishi na wengine licha ya tofauti za kitamaduni na kidini.
Papa alifunga mkutano huo na wanahabari kwa kutoa wito kwa wanasiasa kupata ufumbuzi wa kusitisha ghasia Mashariki ya Kati . Na pia alitoa ombi kwa mashirika ya misaada ya ubinadamu, yaendelee kusaidia kwa ukarimu, wote wanaoteswa na hali hizi za ghasia na madhulumu.
Pia alikumbusha umuhimu wa watu kuzama katika sala kwa uaminifu na uchaji , maana sala ya umma inaweza kuwa na kishindo katika utoaji wa maoni ya umma. Sala inayotolewa kwa Mungu kwa uaminifu, inaweza kutenda maajabu mengi.








All the contents on this site are copyrighted ©.