2018-05-09 14:49:00

Papa Francisko: Kuzeni na kudumisha Ibada kwa Bikira Maria


Baba Mtakatifu Francisko ameuanza Mwezi Mei, ambao ni mwezi wa Rozari Takatifu kwa kusali kwenye Madhabahu ya Bikira Maria ya “Divino Amore” yaliyoko Jimbo kuu la Roma. Nia ya Sala hii ilikuwa ni kwa ajili ya kuombea amani nchini Siria pamoja na sehemu mbali mbali za dunia. Baba Mtakatifu mara baada ya Katekesi yake, Jumatano, tarehe 9 Mei 2018, ameendelea kuwaalika waamini pamoja na watu wote wenye mapenzi mema kusali kwa ajili ya kuombea amani nchini Siria na duniani kote, ili amani ya kudumu iweze kupatikana kama kikolezo cha maendeleo endelevu ya binadamu. Baba Mtakatifu amewataka waamini kukuza na kudumisha Ibada ya Kusali Rozari Takatifu, muhtasari wa historia ya huruma ya Mungu katika maisha ya mwanadamu! Baba Mtakatifu anawataka waamini kuwa kweli ni vyombo na mashuhuda wa huruma na upendo wa Mungu kwa jirani zao.

Baba Mtakatifu katika sala yake anasema, Bikira Maria, Mama wa Mungu na Malkia wa Rozari Takatifu, amebarikiwa kuliko wanawake wote, ni sura ya Kanisa iliyovishwa mwanga wa Pasaka; Yeye ni heshima ya watu wa Mungu; mshindi dhidi ya dhambi na ubaya wa moyo! Bikira Maria ni shuhuda wa unabii wa upendo wa huruma ya Mungu; mwalimu mahiri wa Habari Njema ya Mwana wa Mungu, alama ya moto wa Roho Mtakatifu. Huku bondeni kwenye furaha na machozi, Bikira Maria awafundishe watoto wake ukweli wa milele ambao Baba wa milele, anapenda kuwafunulia wadogo. Bikira Maria awaoneshe ulinzi na tunza ya mkono wenye nguvu! Moyo wake usiokuwa na doa uwe ni kimbilio la wadhambi, njia inayowaelekeza kwa Mwenyezi Mungu. Baba Mtakatifu Francisko akiwa ameungana na ndugu zake wote katika imani, matumaini na mapendo, wanajiaminisha kwa Bikira Maria na kujiweka wakfu kwa Mwenyezi Mungu, ili kumtolea Mungu utukufu, milele yote!

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.

Vatican News!

 








All the contents on this site are copyrighted ©.