2017-12-30 08:33:00

Ibada za kufunga mwaka 2017 na kufungua Mwaka 2018 mjini Vatican


Baba Mtakatifu Francisko katika mchakato wa kukunja jamvi la Mwaka 2017, tayari kuanza mwaka 2018, anatarajiwa, Jumapili, tarehe 31 Desemba 2017 saa 11 Kamili za jioni kuongoza Ibada ya Masifu ya kwanza ya Jioni kwa ajili ya maadhimisho ya Sherehe ya Bikira Maria, Mama wa Mungu. Ibada hii itapambwa kwa “Te Deum” yaani “Utenzi wa Sifa na shukrani kwa Mwenyezi Mungu” kwa kuumaliza Mwaka salama pamoja na Ibada ya Kuabudu Ekaristi Takatifu. Mara baada ya Masifu ya jioni, Baba Mtakatifu atatembelea Pango la Noeli lililojengwa kwenye Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican.

Jumatatu, tarehe Mosi, Januari 2018, majira ya saa 4:00 kwa saa za Ulaya, Baba Mtakatifu Francisko atauanza Mwaka 2018 kwa Ibada ya Misa Takatifu kwenye Kanisa kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican kwa heshima ya Bikira Maria Mama wa Mungu sanjari na Maadhimisho ya Siku ya 51ya Kuombea Amani Duniani inayoongozwa na kauli mbiu “Wahamiaji na wakimbizi ni watu wanaotafuta amani”. Baadaye wakati wa mchana, Baba Mtakatifu atawaongoza waamini kwa Sala ya Malaika wa Bwana. Vatican News, itaendelea kuwa nawe mubashara ili kukujuza yale yanayojiri katika maadhimisho haya!

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.

Vatican News!








All the contents on this site are copyrighted ©.