Tarehe 23 Novemba 2017 saa 11 na nusu jioni masaa ya Ulaya, katika Kanisa Kuu la Mtakatifu Petro, Baba Mtakatifu Francisko ataongoza maadhimisho ya sala ya Amani kwa ajili ya nchi ya Sudan ya Kusini na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo.Mwaliko ni kwa watu wote hapatakuwapo na tiketi za kuingilia.
wakati huo huo Baba Mtakatifu Francisko ametoa msaada wa fedha kwa familia 5,000 ambamo wanaishi zaidi ya watu 30,000, wenye kukabiliwa na hali ngumu ya njaa katika eneo la Yei , kanda ya Equatoria, Sudan Kusini. Msaada huo unalenga kurudisha ari ya uzalishaji mazao ya kilimo kwa familia hizo, zinazokabiliwa na upungufu mkubwa wa chakula katika kipidi cha miezi kadhaa ijayo.
Habari imebaini msaada huo wa Baba Mtakatifu Francisko,ambao ni zaidi ya Euro 25,000, kupitia Shirika la Umoja wa Mataifa la Chakula na Kilimo(FAO), ni kwa ajili ya upatikanaji wa pembejeo na zana za kilimo katika kanda hiyo ambako mashamba mengi yaliharibiwa wakati wa mapigano na vurugu za kivita. Mwalikishi wa FAO Sudan Kusini , Serge Tissot, akizungumzia msaada huo, ameonyesha kufurahia kwamba , msaada unaleta matumaini mapya ya maisha kwa wakulima wengi waliomezwa na hofu za kifo cha njaa. Kwa msaada huo wakulima wa Yei wataweza rudi tena mashambani mwao, kufanikisha shughuli za kilimo, hivyo kujiweka mbali na kifo cha njaa.
Vivyo hiyo baadhi ya wakulima katika kanda hiyo ya Equatoria Kati wakihojiwa na wanahabari juu ya msaada huu, wametoa shukurani zao za dhati kwa Papa Francisko wakisema , utawawezesha wengi kurudi katika maeneo yao waliyokuwa wameyakimbia. Vivyo hivyo, Askofu Jeremia Taban wa Jimbo la Yei , amemshukuru Papa Francisko kwa msaada wake , utakaowawezesha watu karibia elfu tano , kupambana vyema na njaa kali inayowakabili na hasa familia maskini zaidi.
Thabita Janeth Mhella
Idhaa ya Kiswahili ya Radio vatican
All the contents on this site are copyrighted ©. |