2017-10-09 11:05:00

Papa Francisko na Utume wa Sala, Mwezi Oktoba 2017


Baba Mtakatifu Francisko katika nia zake za jumla kwa Mwezi Okoba, 2017 anajielekeza zaidi katika haki ya kazi kama sehemu ya utimilifu wa utu na heshima ya binadamu! Kuna mamilioni ya watu wanaotafuta fursa za ajira katika sehemu mbali mbali za kazi, ili kujihakikishia matumaini kwa siku za usoni. Haya ni matunda ya jasho, juhudi, bidii na maarifa. Si rahisi kuweza kupata kazi bila kuonesha vyeti vinavyostahili, hata ikiwa ni ile kazi ya kawaida kabisa inayoweza kufanywa na wote.

Baba Mtakatifu Francisko katika ujumbe wake kwa njia ya video kwenye mtandao wa Utume wa sala anaonesha furaha, vicheko na tabasamu; upendo, ukarimu na mshikamano; mambo msingi yanayofumbatwa katika ujumbe huu. Baba Mtakatifu anakazia haki ya wafanyakazi na haki ya watu wasiokuwa na fursa za ajira. Familia ya Mungu inakumbushwa kwamba, utu, heshima na haki msingi za wafanyakazi zinapaswa kulindwa na kudumishwa, kwani ni sehemu muhimu sana za mchakato wa maendeleo endelevu ya binadamu na jamii katika ujumla wake.

Baba Mtakatifu Francisko anawaalika waamini pamoja na watu wote wenye mapenzi mema katika mwezi huu wa Oktoba, kusali kwa ajili ya kuwaombea wafanyakazi katika ulimwengu wa kazi, ili kwamba, wafanyakazi wote waweze kuwa na uhakika wa usalama na haki zao msingi. Watu wasiokuwa na fursa za ajira, wapewe nafasi pia ya kuchangia ustawi, maendeleo na mafao ya wengi.

Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.

Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.








All the contents on this site are copyrighted ©.