2017-08-16 09:54:00

Baraza la Makanisa Ulimwenguni kuiombea amani nchi ya Korea


Tarehe 13 Agosti 2017 ilikuwa ni Siku ya Sala  katika Peninsula ya Korea, siku iliyo andaliwa na Baraza la Makanisa Ulimwenguni ambapo kwa mwaka huu wametoa kipaumbele zaidi katika nchi ya Korea kutokana na hali ya mvutano wa kisiasa na kijeshi.
Shirika la habari la Osservatore Romano linaeleza kuwa, siku ya maombi imewekwa rasmi Jumapili inayoekelea  tarehe 15 ya mwezi Agosti , siku ambayo inakumbusha uhuru wa nchi ya Korea kutoka Ukoloni wa Kijapani mwaka 1945, vilevile inakumbusha hata mgawanyiko wa visiwa vya Korea  katika sehemu mbili tofauti. Siku ya maombi ya sala ilikuwa imegawanyika katika sehemu tofauti kwa mantiki ya hija ya haki na amani iliyoandaliwa na Baraza hilo la Makanisa Duniani, ikiwa na kauli mbiu kutoka Barua ya Mtakatifu Paulo kwa Waroma isemaayo “ kwa hiyo tuyazingatie daima mambo yenye kuleta amani na yanayotusaidia kujengana” (Waroma 14, 19).

Katika suala  la nchi ya Korea, pia upo wito wa Katibu Mkuu wa Baraza la Makanisa duniani Olav Fykse Tveit ambaye anaona umuhimu wa kutafuta suluhisho la haraka ili hatari ya migogoro hiyo iweze kupungua badala ya kuongezeka. Kwa namna hiyo anasisitizia Jumuiya ya Kimataifa kuwa makini katika kuingilia kati ili kuweza kutoa ufumbuzi wa mgogoro huo.
Ni zaidi sasa ya miaka 30 Baraza la Makanisa ulimwenguni imejikita katika kuongoza mazungumzo na mikutano kati ya wakristo wa sehemu mbili za Korea. Mara kwa mara wamekuwa na ugomvi wa maneno mengi ambayo yamezidisha mivutano na kusababisha hatari na migogoro ya silaha na nguvu za nyuklia.

Sr Angela Rwezaula
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican

 








All the contents on this site are copyrighted ©.