2017-05-19 13:16:00

TBS uchumi wa kati Tanzania unawezekana kupitia uchumi wa viwanda


Shirika la Viwango Nchini Tanzania (TBS) liimejipanga kuzalisha bidhaa zenye ubora wa kumudu ushindani wa masoko ya ndani na nje ya nchi ya Tanzania ili kutimiza malengo ya Serikali ya kufikia uchumi wa kati kupitia uchumi wa viwanda.Hayo yamesemwa Alhamisi, tarehe 18 Mei 2017 na Mkurugenzi wa Shirika hilo Prof. Egid Mubofu wakati wa mahojiano maalumu katika kipindi cha TUNATEKELEZA kinachoandaliwa na Idara ya Habari (MAELEZO) na kurushwa hewani na Kituo cha Televisheni ya Taifa (TBC).

Prof. Mubofu alisema kuwa, jukumu la nchi kuingia kwenye uchumi wa viwanda si la TBS pekee bali la watanzania wote hivyo suala la kudhibiti viwango vya ubora wa bidhaa ni la watanzania wote kwa faida ya jamii na taifa kwa ujumla. “TBS imekuwa na majukumu mbalimbali ikiwemo kuandaa viwango vya kitaifa, kikanda na kimataifa, kutoa elimu kwa wazalishaji wa viwandani ili kusaidia kuzalisha viwango vinavyohitajika na kuhakikisha bidhaa hizo zinakidhi viwango” alifafanua Prof. Mubofu.

Prof. Mubofu amewataka Watanzania kuhakikisha bidhaa zinazoingia au kuzalishwa nchini zinakidhi viwango kwani suala hilo si la TBS pekee bali ni la watanzania wote.  Katika kutekeleza malengo hayo, TBS ina mkakati wa kutengeneza ‘Electronic Signature’ itakayowezesha walaji kuhakiki bidhaa iwapo zimekaguliwa kwa kutumia simu ya mkononi kwa lengo la kurahisisha utendaji kazi. Vilevile alisema kuwa, ifikapo mwezi Agosti mwaka huu TBS itaanza kutoa nembo kwa bidhaa za nje zinazoingizwa nchini baada ya kuzikagua ambapo kwa sasa nembo za TBS zitatolewa kwa bidhaa zinazozalishwa nchini Tanzania. “Kwa sampuli ambazo zinatoka nje ya nchi kuingia nchini hasa kwa bidhaa hatarishi ikiwemo chakula,TBS itazichukua na kuzipeleka katika maabara zetu ili kupima kama zinakidhi kiwango kinachostahili” alisema Mkurugenzi huyo.

Akifafanua zaidi Prof. Mubofu alisema katika kipindi cha mwaka wa fedha 2016/17 takribani sampuli 11,600 za bidhaa mbalimbali zimepimwa kupitia TBS na kutengeneza viwango 174 ikiwa ni pungufu ya lengo kufikisha viwango 200 ifikapo mwisho wa mwaka wa fedha.

Na Beatrice Lyimo,  

MAELEZO, DAR ES SALAAM.








All the contents on this site are copyrighted ©.