Upendo wa Yesu hauna kipimo na wala siyo kama upendo wa kiulimwengu unaotafuta
madaraka na ubatili mtupu.Ni maneno kutoka katika mahubiri ya Baba Mtakatifu Francisko
wakati wa Misa Takatifu tarehe 18 Mei 2017 katika Kikanisa cha Mtakatifu Marta mjini
Vatican. Baba Mtakatifu amebainisha kwamba utume wa kikristo ni kutoa furaha kwa
watu , na kwamba upendo wa Mungu ni kiini cha maisha ya Kikristo.
Kama Baba alivyonipenda mimi hata mimi nawapenda ninyi. Baba Mtakatifu amechambua
maneno hayo ya Yesu yanayosisitiza upendo usio na kikomo kutoka Injili ya siku iliyosomwa.
Bwana Mungu natutaka tubaki katika upendo wake kwasababu ni upendo wa Bwana na kuzishika
amri zake. Amri kumi za Mungu ndiyo msingi wa kufuata mambo yote aliyotufundisha
Yesu mwenyewe na ndiyo amri za kuishi kila siku katika maisha yetu kwa maana zinawakilisha
namna ya kuishi kikristo.
Aidha Baba Mtakatifu anasema kuna mlolongo mpana wa amri za Yesu, lakini msingi ni mmoja tu wa upendo wa Baba na yeye na upendo wake kwetu sisi. Hata hivyo kuna aina nyingi za upendo; kwasababu hata ulimwengu huu unatengeneza aina zake za upendo: kama vile upendo wa fedha, upendo wa kibatili, upendo wa kiburi, upendo wa madaraka, hata kudiriki kufanya mambo yasiyo ya haki ilimradi kuwa madarakani; huo ni upendo wa aina nyingine, siyo upendo wa Yesu na wala upendo wa Baba yake. Yesu mwenyewe anaomba tubaki katika upendo wake na katika upendo wa Baba. Tufikirie hata upendo wa aina nyingine ambao unatupeleka mbali na upendo wa Yesu kama vile aina za vipimo vya kupenda, na hivyo ni kama kupenda nusu lakini hiyo siyo upendo. Pia kuna jambo la jema la kutakiana mema ambalo ni upendo hata kama haujafikia upendo kamili. Anafafanua akisema kuwa; kupenda ni zaidi ya kutakiana mema. Anaongeza je ni kipimo gani cha upendo ? Kipimo cha upendo ni kupenda bila kipimo. Kwa njia hiyo ni lazima kufanya kama alivyo tuagiza Yesu ili tubaki katika upendo wa Yesu na Upendo wa Baba mwenyewe , tupende bila kikomo wala ubaridi na hata kwa manufaa yetu sisi.
Swali lake Baba Mtakatifu anauliza kwa nini Bwana amekumbusha hilo?, anasema, tunaweza kumjibu kwamba ili furaha yangu katika ninyi iwe kamilifu. Kama upendo unatoka kwa Baba kwa njia ya Yesu, hivyo Yesu anatufundisha njia ya upendo, ambayo ni mwoyo ulio wazi na kupenda bila kikomo kwa kutupilia mbali upendo upendo wa malimwengu. Upendo mkubwa wa Yesu, Baba Mtakatifu anaongeza, ni ule wa kubaki katika upendo na furaha hiyo; upendo na furaha ni zawadi ambavyo tunalazimika kumuomba Bwana. Ametoa mfano kuwa, siku za hivi karibuni, Padre mmoja amateuliwa kuwa askofu. Huyo Padre alikwenda kwa baba yake mzee na kumpatia habari hii. Baba huyo mzee ambaye yuko tayari pensheni , mtu mnyenyekevu , aliyefanya kazi katika maisha yake yote lakini hakwenda hata chuo kikuu lakini alikuwa mwenye hekima ya maisha. Huyo baba alimshauri mtoto wake mambo mawili tu, yaani kutii na kuwapa furaha watu.
Kwa maana hiyo Baba Mtakatifu amesema kwamba, mzee huyo alitambua kwamba ni kutii upendo wa Baba bila kuwa na upendo mwingine, kutii zawadi hiyo na baadaye kuwapa furaha watu .Kwa njia hiyo wakristo wote, walei, mapadre watawa na maaskofu tunalazimika kutoa furaha kwa watu. Je ni kwasababu gani? Ndiyo njia ya maisha ya upendo bila kuwa na mafaa mengine zaidi hiyo ndiyo njia tu ya kupenda . Utume wetu wa kikristo ni kutoa furaha kwa watu. Baba Mtakatifu Francisko amemalizia kwa matashi mema ya kuweza kubaki katika upendo wa Yesu ili kuweza kutoa furaha kwa watu.
Sr Angela Rwezaula
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican
All the contents on this site are copyrighted ©. |