2017-04-14 17:19:00

Tazameni mtu! Ecce homo!


Fumbo la Pasaka la Msalaba na Ufufuko wa Kristo ni kiini cha Habari Njema ambayo Mitume na Kanisa baada yao, wanapaswa kuitangaza na kuishuhudia duniani. Mpango wa wokovu wa Mungu umetimilika mara moja tu kwa mateso, kifo na ufufuko wa Kristo Yesu! Ijumaa kuu, ni Siku ambayo Kanisa linaadhimisha  na kukumbuka  mateso na kifo  cha Bwana wetu Yesu Kristo,  katika kilima cha Kalvari nje kidogo ya mji wa Yesuslemu, kiini cha imani, matuma. Ni siku ambayo kwa mateso makali  na  ya kutisha Yesu anakufa  msalabani, ikiwa ndiyo siku ya kumi na nne ya mwezi wa Nisani. Safari hii ya mateso ilianza hivi, pale bustanini Gesthmane, bila kusema neno  Yesu alijitoa kwa watesi wake, na ndipo wakamfunga mikono yake na kiuno pia, njia ya mateso ikaanza na mara wakafika nyumbani kwa kayafa, ambako Yesu alitakiwa kupelekwa mbele ya baraza.

Wakati huu ilikuwa yapata asubuhi, lakini giza lingali bado, tena hata masaa kazaa, na ilikuwa miiko kumhukumu mtu kungali giza bado, kulingana na desturi za kiyahudi.  Pale ndipo wote walipokutanika  mbele ya Kayafa na mara Yesu akaletwa mbele yao. Na hapo wale mashahidi wakatoa ushuhuda wa uwongo kuhusu Yesu, ili tu auwawe.  Ila   sasa wote mbele ya Kayafa wakasema asulubiwe. Na sasa Yesu akapelekwa mbele ya Pilato,  na ilikuwa yapata saa sita  kamili. Hapa watu hawakuingia ndani ya Pretorio ili wasije wakanajisika   kwa kuingia katika jengo la watu wa mataifa.  kwani wakati huo pia, Pasaka ya kiyahudi ilikuwa ikikaribia. Ila katika haya yote hawakusita kumsulibisha mtu asiyekuwa na hatia yeyote.  Na ndipo Pilato akampeleka Yesu kwa Herode,  na  ndipo  Herode akafadhaika sana, kwani alijua makuu aliyotenda Yesu. Na kwa mfadhaiko huo Herode alimrudisha tena Yesu kwa   Pilato.

Hapo ndipo Pilato akamtwaa Yesu mbele ya watu, na kwa maneno haya akamtambulisha Yesu;  tazameni mtu (ecce  homo).  Maana halisi ya neno  hili Tazameni mtu,  ni rejeo la maneno  yaliyonenwa na Nabii Isaya akisema ”wengi waliomwona walishtuka, kwa vile sura yake ilikuwa imeharibiwa, hakuwa tena na umbo la kibinadamau. Is 52:14.   Tazameni   Mtu,  mtu wa masikitiko makubwa, anavyoangaika Msalabani, akiwa uchi, akitemewa mate, wakimkejeli na kumdhihaki, amedhoofika na hata mifupa yake inahesabika. Basi, Tazameni Mtu,  “ Ecce homo”, Nabii Isaya anaendelea kutuambia  “hakuwa na umbo, wala sura ya kutupendeza, wala hakuwa   na uzuri wowote wa kuvutia, alidharauliwa na kukataliwa na watu, alikuwa mtu wa huzuni na uchungu, alikuwa kama mtu kinyaa kwa watu, alidharauliwa na akaonenakana  si kitu.  Is 53:2-3.  Angalia mateso haya tafakari  tuwe na uchungu wa dhambi moyoni, tuomboleze na kulia kwa toba na wongofu wa ndani na huruma na msamaha wa Mungu utuinue tena!

Ecce homo: Tazameni mtu, Huu  ni upendo wa Yesu, upendo usiopimika , kwani leo  ametufia msalabani , amesulibiwa kwa dhambi zetu , hichi ndicho  kifo  kilichonenwa  na  manabii , pale nabii Isaya aliposema, Alidhulimiwa, akahukumiwa  na kupelekwa kuuawa, na hakuna mtu aliyejali  yaliyompata, alifukuzwa kutoka nchi ya walio hai kwa ajili ya makosa ya watu wangu. Is 53:8. Utabiri mwingine wa kinabii kuhusu Yesu kusulibiwa Msalabani  ni pale mfalme Daudi, mfalme wa Waisraeli, yapata miaka 1000 kabla ya Kristo, alipotabiri undani na ukatili wa kifo cha msalaba , ambacho yeye mwenyewe kamwe hawezi kukikabili.  Utabiri   huu tunaupata kwenye zaburi  ya 22:14 – 18, inayosema.. nimekwisha kama maji  yaliyo mwagika , mifupa yangu yote imetenguka , Moyo wangu ni kama nta unayeyuka ndani mwangu ,  koo langu limekauka kama kigae , ulimi wangu wanata kinywani mwangu, umeniacha kwenye mavumbi ya kifo. Genge la waovu limenizunguka , wamenitoboa mikono na miguu, nimebaki mifupa tupu  adui zangu wananiangalia na kunisumanaga, wanagawana nguo zangu na kulipigia kura vazi langu. Zab  22;14-18.

Maziko ya Yesu nayo pia yalikuwa yamekwisha tabiriwa kuwa yatakuwa ni maziko ya namana gani,  pale nabii isaya anapotuambia.. walinizika pamoja na wahalifu , katika kifo aliwekwa pamoja na matajiri, ingawa hakutenda ukatili  wowote, wala hakusema neno  lolote la udanganyifu. Is 53:9.   Utimilifu wa maneno haya ni kwamba Yesu amekufa kama mtu dhaifu  katika macho ya Dunia  na katikati  yake wahalifu wawili walisulibiwa naye. Mt 27:38.  Na baada kifo chake mtu tajiri Yosefu wa Arimathaya  aliomba mwili wake ili kwenda kuuzika.

Maandiko haya ya manabii yametimia leo ili tupate kuamini kuwa Yesu ni Bwana na kwa dhambi zetu amekufa mauti  tena mauti ya msalaba ili apate kutukuomboa na kutuelekeza  wote kwa Baba.  Mwimbaji mmoja  aliimba ila kwa kiingereza  ( where you there when they crucified my lord...yaani:  Je,’ ulukuwepo walipomsulibisha  Bwana wangu .. akaendelea  sometimes it does  indeed cause me to tremble....yaani  hunifanya hata mara kutetemeka ninaposikia maneno haya Msalabani  Yametimia, ndipo akainamisha kichwa akatoa roho. Yametimia maana yake, yamekamilika, kukamilishwa katika kizingiti cha juu na cha mwisho kabisa  ikichorwa milele katika mawazo na mioyo ya mwanadamu.

Na Padre Agapiti Amani ALCP/OSS.








All the contents on this site are copyrighted ©.