2017-04-11 14:28:00

Askofu Inacio Saure ateuliwa kuwa Askofu mkuu wa Jimbo kuu la Nampula


Baba Mtakatifu Francisko amemteua Askofu Inacio Saure wa Jimbo Katoliki Tete, Msumbiji kuwa Askofu mkuu wa Jimbo Kuu la Nampula Msumbiji. Wakati huo huo, Baba Mtakatifu amemteua Mheshimiwa Padre Sandro Faedi, kuwa Msimamizi wa Kitume Jimbo Katoliki la Tete, Msumbiji. Itakumbukwa kwamba, Askofu mkuu mteule Saure alizaliwa kunako tarehe 2 Machi 1960 huko Balama. Baada ya masomo na majiundo yake ya kitawa kunako tarehe 15 Mei 1998 akaweka nadhiri zake za daima kwenye Shirika la Wamissionari wa Consolata na kupadrishwa tarehe 8 Desemba 1998.

Baba Mtakatifu Mstaafu Benedikto XVI, tarehe 12 Aprili 2011 akamteua kuwa Askofu wa Jimbo Katoliki Tete, Msumbiji na kukwekwa wakfu tarehe 22 Mei 2011 na akasimikwa rasmi kama Askofu wa Jimbo Katoliki la TeteĀ  tarehe 5 Juni 2011. Tarehe 11 Aprili 2017 ameteuliwa na Baba Mtakatifu Francisko kuwa Askofu mkuu wa Jimbo kuu la Nampula, Msumbiji.

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.

Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.








All the contents on this site are copyrighted ©.