Watu zaidi ya 700 tayari wamepoteza maisha kutokana na ugonjwa wa malaria nchini
Burundi mwaka huu, ikiwa ni sawa na watu kumi kufa kila siku, na tayari serikali imetangaza
kuwa malaria ni janga la kitaifa.Waziri wa Afya Daktari Josiane Nijimbere ametangaza
Jumatatu 13 Mchi 2017 kuwa kiwango cha dola za Kimarekani milioni 31 zinahitajika
ili kukabiliana na ugonjwa huo.Waziri huyo ametangaza kuwa ugonjwa wa malaria umekuwa
ni janga la kitaifa.Kulingana na takwimu kutoka wizara hiyo wananchi milioni mbili
waliuguwa homa ya malaria tangu mwanzoni mwa mwaka 2016, hadi hivi sasa.
Waziri wa afya amelinganisha maambukizi ya mwaka huu na yale ya mwaka jana akisema
kati ya wakazi milioni kumi nchini, watu milioni nane sawa na robo tatu ya wananchi
waliumwa malaria mwaka jana. Maambukizi yaliongezeka kwa asilimia 13 mwaka huu ukilinganisha
na mwaka jana ambapo katika miezi miwili ya mwanzo, waliofariki dunia kutokana na
malaria walikuwa theluthi moja ya waliofariki kwa kipindi cha mwaka mzima.
Mikoa inayoathiriwa zaidi ni pamoja na Muyinga Kirundo na Karusi kaskazini Ngozi na Kayanza kaskazini mwa Burundi, pamoja na mkoa wa Ruyigi mashariki na karusi kati kati. Sababu za ugonjwa huo kuongezeka, ni mabadiliko ya hali ya hewa, amesema waziri.Ameongeza kuwa kutokana na madiliko ya tabia nchi, sasa mbu wanao ambukiza ugonjwa huo wanaweza kupatikana katika nchi nzima. katika mikoa hiyo joto limepanda sana. Kuna pia kilimo cha mpunga na kama mnavyojuwa vyote hivyo vinahitaji maji mengi. Waziri amesema ni vuzuri kuendeleza kilimo hicho lakini tuna wakumbusha watu wasiache maji yakitiririka karibu na makazi yao ili mbu wasipate mahali pa kuzaliana na watu waendelee kutumia vizuri vyandarua.Sasa mkakati umeandaliwa kwa ushirikiano na wahisani ili kukabiliana na ujonjwa huo na kiwango cha fedha kinachohitajika ni dola milioni 31 za kimarekani.
Waziri wa afya imesema dawa za dharura zimekwisha nunuliwa na kwamba wako tayari kuwatibu raia pasipo kulipa gharama yoyote.Wizara imesema waganga wa ziada walipelekwa kusaidia katika maeneo yalioathiriwa zaidi kukiwa na mpango pia wa kuwahudumia wananchi ambao wanaishi katika vijiji vilivyoko mbali na vituo vya afya. Kwa mara ya mwisho ulikuwa ni mwaka 2002 ambapo ugonjwa huo wa malaria ulitangazwa nchini Burundi kuwa ni janga la kitaifa.Ikumbukwe kwamba Burundi tangu 2015 inapitia kipindi kigumu cha vurugu na machafuko, wakati huo huo inakabiliwa na ukosefu wa chakula na maji ya kunywa, mambo yanayozidi kuwasababishia maisha ya maelfu ya watu kuwa hatarini.
Sr Angwela Rwezaula
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.
All the contents on this site are copyrighted ©. |