2017-01-26 13:59:00

Mazao ya kilimo kuongezewa thamani kabla ya kuuzwa nje ya Tanzania


Waziri Mkuu wa Tanzania Kassim M. Majaliwa amesema Serikali imejipanga katika kuhakikisha inaongeza thamani ya mazao yake kabla ya kuyauza nje ya nchi. Amesema kwa muda mrefu Serikali ilikuwa inapata hasara kwa kusafirisha malighafi nje nchi lakini kwa sasa inajenga viwanda ili iweze kuuza bidhaa. Waziri Mkuu ametoa kauli hiyo Jumatano, Januari 25, 2017 wakati alikizungumza na wakulima wa chai katika kijiji cha Lwangu wilayani Njombe. “Miaka mingi Serikali imekuwa ikipata hasara kwa kuuza mazao nje ya nchi, tumeamua kujenga viwanda vitakavyoweza kuyachakata na kuuza bidhaa badala ya malighafi,”.

“Ujenzi wa viwanda ni moja kati ya mikakati dhati ya Serikali ya kuhakikisha mazao mnayolima yanakuwa na thamani kubwa hivyo kuwaongezea tija,” alisema. Kutokana na mkakati huo Waziri Mkuu amewataka wananchi kuongeza juhudi katika kilimo.“Kuna anayetaka hela hapa? Kama mnataka mali mtazipata shambani. Limeni,”. Waziri Mkuu alisema mazao hayo ndiyo yatakayoweza kuleta tija kwa wakulima, hivyo aliwashauri waendelee kushirikiana katika vikundi ili wapate misaada ya kitaalam kwa urahisi. Aidha, alimuagiza mkuu wa wilaya hiyo, Ruth Msafiri na Maafisa kilimo kuwatembelea wakulima hao kwa lengo la kuwaelekeza namna bora ya kuendeleza mazao yao. Waziri Mkuu alisema hatua hiyo itawawezesha wakulima kupata mbinu bora za kilimo na hatimaye kuvuna mazao mengi yenye viwango vya ubora vinavyotakiwa kimataifa.

Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu aliiagiza halmashauri ya wilaya ya Njombe kuwaunga mkono wakulima hao kwa kuimarisha barabara zinazoingia kwenye mashamba yao. “Tuwaunge wakulima wetu kwa kuwaimarishia miundombinu ya barabara ili kuwawezesha kupeleka chai yao kiwandani kwa gharama nafuu,” alisema. Naye Mbunge wa jimbo la Lupembe Mheshimiwa Joram Hongoli alisema kilimo cha chai ndio mkombozi kwa wananchi hao, hivyo aliwaomba waongeze juhudi.

Awali Meneja Mkuu wa Kampuni ya Kutoa Huduma kwa Wakulima Wadogo Njombe (NOSC), Bw. Filber Kavia alisema kampuni inatoa huduma za kitaalam kwa wakulima. Alisema wanalenga kuendeleza kilimo cha chai kwa kuongeza kuongeza uzalishaji kwa hao kutoka kilo 500 hadi kilo 2,000 za majani makavu ya chai kwa hekta kwa mwaka.  Meneja huyo alisema kampuni inakusudia kuongeza mashamba mapya ya chai hadi kufikia hekta 3,800 kutoka hekta 614 ifikapo mwaka 2025.

Bw, Kavia alisema huduma nyingine inayotolewa na kampuni hiyo ni utoaji wa mikopo nafuu ya pembejeo bila ya riba na mkulima hulipa muda mrefu kupitia mauzo ya chai. Pia kampuni hiyo inatoa huduma ya usimamizi wa mashamba makubwa ya chai ya vijiji na watu binafsi kwa mkataba maalumu ili kuongeza uzalishaji na tija. Awali Waziri Mkuu alikagua eneo litakalojengwa kiwanda cha kisasa cha kuchakata chai cha kampuni ya Unilever.

IMETOLEWA NA:

OFISI YA WAZIRI MKUU.








All the contents on this site are copyrighted ©.