2016-11-19 15:31:00

Papa Francisko: Kesi ziendeshwe haraka kupunguza gharama, lengo si talaka!


Katika mahakama kuu ya ndoa ya Kanisa Katoliki, yaani Rota Romana, kumefanyika warsha kwa maaskofu, kuhusu taratibu mpya za uendeshaji wa kesi za ndoa. Warsha hiyo imefanyika tangu tarehe 17 mpaka 19 Novemba 2016. Taratibu hizo mpya zinalenga kuharakisha kesi za ndoa na kwa gharama nafuu, ili kuwasaidia waamini walei ambao ndoa zao ni batili waweze kushughulikiwa kwa wakati na kupatiwa ufumbuzi kadiri ya misingi ya mafundisho ya Kanisa.

Wakati warsha hiyo ikiendelea, Baba Mtakatifu Francisko, aliwatembelea maaskofu washiriki hao jioni ya siku ya Ijumaa, tarehe 18 Novemba, na kuwakumbusha kwamba, ingawa wao ni walimu wa imani kutokana na hadhi waliyonayo ya uaskofu, ni muhimu kujinoa mara kwa mara, ili kujibu mahitaji ya wana wa Mungu, wanaotafuta majibu katika Neno la Mungu, katika kweli ya imani.

Kama ambavyo Mwenyeheri Paulo VI anafundisha katika Barua yake ya Kitume, Evangelii nuntiandi, yaani Utangazaji wa Injili, ni lazima kuihubiri Injili kwa namna ambayo ni halisi kadiri ya hali na mahitaji ya watu. Uinjilishaji usiwe wa kupambapamba au kulembalemba, bali uingie katika kina cha maisha ya watu, mpaka kwenye mizizi ya kila wanachofanya, na uinjilishaji huo uanze kwa kumlenga mwanadamu na kuhitimisha katika mahusiano kati ya wanadamau, na kati ya wanadamu na Mungu (Rej., Evangelii nuntiandi, 20). Kwa misingi hiyo hiyo ya kumuweka mwanadamu kuwa kiini cha uinjilishaji, ndiyo sababu warsha hiyo imeendeshwa katika mahakama hiyo kuu ya ndoa, ili kutafuta wokovu wa roho za waamini.

Mtume Petro anafundisha juu ya huduma msingi ya Askofu katika Kanisa: Mlichunge lile kundi la Mungu mlilokabidhiwa, mlitunze sio kwa kulazimika, bali kwa hiari kama atakavyo Mungu. Fanyeni kazi hiyo sio kwa tamaa ya fedha, bali kwa moyo wenu wote. Msiwatawale kwa mabavu hao waliowekwa chini ya ulinzi wenu, bali muwe mfano kwa hilo kundi.  (Rej., IPetro 5: 2-3). Wosia huo unaangaza utume mzima wa Askofu, ukiwasilisha mamlaka ya kiroho kuwa huduma kwa ajili ya wokovu wa watu. Kwa mtazamo huo, anahimiza Baba Mtakatifu Francisko, ni lazima kuondoa vikwazo vyote vinavyozuia  waamini wengi kuhudumiwa katika mahakama za Kanisa. Vikwazo mfano vya kiuchumi au kimikakati na utendaji. Kufuatia mahusiano yaliyopo kati ya haki na ukarimu, Sheria za Kanisa haziwezi kukwepa  Kanuni yake msingi, yaani wokovu wa roho za watu. Mahakama za Kanisa ni watumishi wa lengo hilo la mwisho, lengo linaloakisi Huruma ya Mungu. Kanisa linasafiri katika hija kama mama anayependa na kukumbatia wote, kama msamaria mwema.

Kanisa linajimwilisha katika kila hali ya kila mtu, wakiwemo maskini na wanaowekwa pembezoni mwa jamii, hata ndani ya Kanisa, mfano waliotengana katika ndoa na kujikuta katika mahusiano na mwenza mwingine tena. Ndani ya Kristu wanamkuta Mchungaji Mwema na Hakimu wa haki. Hivyo wachungaji makuhani wanapaswa kujituma kuwajali kwa mafundisho na upendo waamini wote. Taratibu hizo mpya za uendeshaji kesi za ndoa majimboni, zilitolewa tarehe 15 Agosti 2015, na Baba Mtakatifu Francisko, katika Barua binafsi, yaani motu proprio, Mitis Iudex Dominus Iesus, maana yake Bwana Yesu Hakimu wa Haki, akielekeza kupunguza baadhi ya taratibu zilizokuwa zinapelekea kesi za ndoa kuchukua muda mrefu, na kutumia gharama kubwa. Kwa taratibu za sasa, Askofu jimbo anayo haki ya kuwa na mahakama ya ndoa yenye mahakimu watatu wanaoshughulikia kesi moja kwa pamoja wakisaidiana ili kuhakikisha kwamba ukweli wala mafundisho ya Kanisa havipotoshwi wala kupindishwa wakati wa kesi. Lakini pia kwa baadhi ya kesi zenye ushahidi dhahiri usioleta mashaka, uwezekano wa kuwa na hakimu mmoja Padre.

Katika taratibu hizo, ingawa maandalizi na uendeshaji wa kesi za ndoa utafanywa na maafisa wa mahakama, Askofu jimbo mwenyewe ni hakimu kisheria, katika kuthibitisha hukumu ya mwisho juu ya ubatili wa ndoa husika. Taratibu hizo mpya, bado zinadai kuzingatia mafundisho msingi ya Kanisa kwamba, ndoa iliyo halali haivunjwi, bali zinatangazwa batili zilizo batili, tofauti na upotofu uliotolewa na baadhi ya watu kwamba talaka zimeruhusiwa katika Kanisa Katoliki. Kwa baadhi ya kesi, Askofu jimbo atazame uhalisia wa maisha ya kiroho ya wahusika baada ya kutengana, na kuamua inavyofaa ili kuokoa roho zao.

Maafisa wa mahakama za majimbo wawe wameandaliwa vema kisheria, yaani wawe na utaalamu wa kutosha, na kwa kila kesi wahakikishe wanafikia uhakika na ukweli kimaadili wanapotoa hukumu. Mahakama ya Askofu Mkuu itabaki kuwa Mahakama ya Rufaa kwa majimbo yaliyo chini yake, kadiri ya sheria ya zamani. Mahakama kuu ya ndoa Rota Romana, inabaki kuwa Mahakama kuu ya rufaa na pia Mahakama ya kesi ya awali iwapo mwamini ataomba hivyo kwa baadhi ya kesi.

Baraza la Maaskofu Katoliki kwa kila nchi, lione uwezekano wa kuchangia gharama za mahakama hizo, pale inapowezekana, ili kupunguza mzigo kwa waamini wasioweza kugharamikia kesi zao. Hata hivyo Askofu jimbo, aweke utaratibu utakaowezesha waamini kuchangia gharama za mahakama ya jimbo. Taratibu hizi tangu zimetolewa hazikuwa zimeeleweka vizuri kwa baadhi ya Mahakama, hivyo Mahakama kuu ya ndoa, Rota Romana, imeandaa warsha kwa ajili ya maaskofu wawakilishi toka nchi mbali mbali, ili kutoa dukuduku na kuweka majibu sahihi ya uendeshaji wa taratibu hizo mpya. Baba Mtakatifu Francisko kawaasa maaskofu hao kujiaminisha katika uweza wa Roho Mtakatifu kwenye utendaji wao, kwani ni Roho huyo ndiye mwenye kuliwezesha na kulitakatifuza Kanisa.

Na Padre Celestine Nyanda

Idhaa ya Kiswahili, Radio Vatican.








All the contents on this site are copyrighted ©.