2016-11-15 14:23:00

Ujumbe wa Papa Francisko kwa washiriki wa mkutano wa COP22


Uharibifu wa mazingira ni matokeo ya mmong’onyoko wa tunu msingi za maisha ya binadamu, kimaadili na kijamii, changamoto kwa kila mtu kuhakikisha kwamba, anatekeza wajibu wa kulinda mazingira kadiri ya uwezo na nafasi yake katika jamii; hii ni dhamana inayowawajibisha wote. Mkutano wa kimataifa kuhusu mazingira nchini Morocco, COP22 unafanyika baada ya kuanza utekelezaji wa Itifaki ya utunzaji bora wa mazingira iliyopitishwa mjini Paris, Ufaransa kunako mwaka 2015. Athari za mabadiliko ya tabianchi zinahitaji uwajibikaji wa pamoja, ili kushiriki kikamilifu katika utunzaji bora wa mazingira nyumba ya wote.

Huu ni wajibu wa kuhakikisha kwamba, Jumuiya ya Kimataifa inatumia kikamilifu maendeleo ya sayansi na teknolojia ili kudhibiti kikamilifu athari za mabadiliko ya tabianchi sanjari na kutumia nguvu kwa ajili ya mchakato mbadala wa maendeleo endelevu na bora zaidi, unaojikita katika tunu za kiutu na kijamii. Lengo ni kuhakikisha kwamba, uchumi wa dunia unakuwa ni kwa ajili ya huduma kwa binadamu, ili hatimaye, kujenga msingi wa haki na amani, ili kulinda na kutunza mazingira, nyumba ya wote.

Hii ni sehemu ya ujumbe wa Baba Mtakatifu Francisko kwa Bwana Salaheddine Mezouar, Waziri wa mambo ya nchi za nje na ushirikiano wa kimataifa nchini Morocco, kwa niaba ya wajumbe wanaoshiriki katika mkutano wa kimataifa wa tabianchi mjini Marrakech kuanzia tarehe 7- 18 Novemba 2016. Baba Mtakatifu katika ujumbe huu, anaendelea kusema, Itifaki ya Paris imeonesha dira na njia ambayo inapaswa kutumiwa na Jumuiya ya Kimataifa kwa ajili ya kulinda na kutunza mazingira. Itakumbukwa kwamba, waathirika wakubwa wa mabadiliko ya tabianchi ni maskini na kizazi kijacho, jambo linalohitaji uwajibikaji unaozingatia kanuni maadili bila kuchelewa wala kuwa na mashinikizo ya kisiasa na kiuchumi, tayari kuvuka mipaka ya mafao binafsi.

Ni matumaini ya Baba Mtakatifu Francisko kwamba, wajumbe katika mkutano huu watashikamana ili kuweza kupata matunda yanayokusudiwa kama ilivyokuwa kwa Itifaki ya Paris, COP21, tayari kuanza utekelezaji wa itifaki hii, kipindi tete sana kinachohitaji sheria, sera na mikakati ya kitaasisi itakayoiwezesha Jumuiya ya Kimataifa kutekeleza itifaki si tu kiufundi kwa kuungwa mkono pia na sera za kisiasa kwa kutambua kwamba, wote wanaunda familia moja ya binadamu isiyokuwa na mipaka ya kisiasa na kijamii inayoweza kuwagawa au kwa kujikita katika utandawazi usiojali wala kuguswa na mahangaiko ya wengine.

Lengo la utekelezaji wa itifaki hii ni kusaidia kukoleza mchakato wa maendeleo kitaifa na kimataifa kwa kujikita katika utunzaji bora wa mazingira unaofumbata mshikamano na maskini wanaoendelea kujizatiti kupambana na athari za mabadiliko ya tabianchi pamoja na umaskini. Hili ni jukumu pevu ambalo haliwezi kushughulikiwa kikamilifu mintarafu mwelekeo wa kiufundi na kiuchumi peke yake. Hapa kuna haja ya kujikita katika kanuni maadili na kijamii, ili kuleta maendeleo endelevu. Elimu makini isaidie kuleta mabadiliko katika mtindo wa maisha katika uzalishaji na ulaji wa bidhaa na huduma, kwa kuzingatia kanuni za utunzaji bora wa mazingira, nyumba ya wote. Hapa wadau wote wanahamasishwa kushiriki kikamilifu katika utunzaji bora wa mazingira kila mtu kadiri ya uwezo na nafasi yake.

Mwishoni, Baba Mtakatifu Francisko anasema ni matumaini yake kwamba, wajumbe wa mkutano wa mazingira kimataifa huko Marrakech wataongozwa na dhamiri ya uwajibikaji kwa ajili ya utunzaji wa mazingira nyumba ya wote na upendo kwa jirani. Ni changamoto ya kuondokana na mtindo wa maisha yasiyojikita katika elimu na maendeleo endelevu, changamoto kubwa kwa Jumuiya ya Kimataifa katika ulimwengu mamboleo. Ni wakati wa kutekeleza kwa dhati kabisa Itifaki ya Paris kwa ajili ya mafao na ustawi wa wengi.

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.

Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.








All the contents on this site are copyrighted ©.