2016-11-02 08:04:00

Makanisa ya Kikristo Onesheni mshikamano wa umoja na udugu!


Baba Mtakatifu Francisko katika sala ya Malaika wa Bwana, Siku kuu ya Watakatifu wote, tarehe 1 Novemba 2016 baada ya adhimisho Takatifu la Misa, huko Malmo, Sweden, kawashukuru wote kwa ushirki wao, viongozi wa Kanisa katoliki, Rais na Katibu mkuu wa Shirikisho la Makanisa ya Kiinjili ya Kilutheri Duniani, wawakilishi wa kiekumene, wawakilishi wa kidiplomasia, serikali ya Sweden, na wote waliowezesha tukio hilo kufanikiwa.

Amekumbusha kwamba, wakatoliki wanajitambua kuwa ni sehemu ya Familia kubwa ya umoja wa Wakristo. Kawatia moyo wote washiriki kudumu katika sala, Masakramenti na huduma za ukarimu kwa wahitaji. Kawaalika kuwa chumvi na mwanga mahali popote watakapokuwa, kwa namna ya maisha yao ya kila siku, na waoneshe heshima kubwa na mshikamano kwa ndugu wa Makanisa na jumuiya za Kikritso na watu wote wenye mapenzi mema. Amesisitiza kwamba, katika maisha na utume wao, Wakristo hawapo peke yao, wanao watakatifu waliowatangulia mbele ya Baba Mungu, na wa kwanza kati yao akiwa Mama Bikira Maria. Hivyo kawaalika kujiaminisha katika maombezi yao kwa ajili ya ulinzi, furaha na katika mahangaiko ya kila siku.

Na Padre Celestine Nyanda

Idhaa ya Kiswahili, RadioVatican.  








All the contents on this site are copyrighted ©.