2016-09-22 08:50:00

Katekesi ya Papa: yaonya kutohukumu wengine ila kusamehe .


Baba Mtakatifu Francisko , amewaataka Wakristo kuwa na huruma,  kama Bwana wao  alivyo na huruma kwao. Ametaja kwamba, hiyo ni njia nzuri zaidi ya kuushuhudia Upendo wa Kristo kwa watu wote. Na wasipende kuhukumu wengine, isipokuwa kuwa wasamehevu. Papa alitoa kauli hiyo mbele ya maelfu kwa maelfu ya watu, waliokuwa wamekusanyika kama kawaida ya Jumatano asubuhi, katika uwanja wa Kanisa Kuu la Mtakatifu Petro,  kwa nia ya kusikiliza Katekesi ya Papa , licha ya hali ya mvua mvua na unyevu mwingi.

Baba Mtakatifu Francisko, alielekeza mafundisho yake katika Injili ya Luka 6: 36 -38, ambamo Yesu , alikataza tabia za kuwahukumu au kuwalaumu wengine  bali akihimiza kusamehe na kusaidia wengine hasa wahitaji.

Aliwakumbusha kwamba , aya hizi zinamkumbusha kila Mkristo, wajibu wa kuwa na huruma,  kama Baba yetu wa mbinguni  alivyo  mwenye huruma . Maelezo ya Baba Mtakatifu yalilenga katika historia ya wokovu, ambamo  tunafunuliwa kwamba  upendo wa Mungu kwa binadamu hauna kipimo wala hauchoki, kama inavyodhihirishwa katika kifo cha Yesu Msalabani. Hili linaonyesha kipeo cha juu sana cha upendo, kwa mtu kuyatoa maisha yake kwa ajili ya mwingine.  Hivyo upendo huo ni wito wa Yesu kwa binadamu kuwa huruma kama Baba. Papa alionya dhidi ya kuhesabu mara ngapi tunasamehe ,laklini ni kusamehe daima  maana upendo wa kweli  hauwezi pimika badala yake ni wito na ni ishara ya kutembea katika  njia  yake Kristo  kama mashahidi wa huruma yake.

Papa alieleza na kutaja kwamba huo ndiyo utume wa Kanisa. Ni kuwa  kafara wa huruma ya Mungu  kila mahali na kila wakati. Kama Wakristo, kwa hiyo, Mungu anatutaka tuwe mashahidi wake, kwanza kwa kufungua mioyo yetu wenyewe katika huruma yake , na kisha kwa kuipeleka huruma hiyo kwa watu wote, hasa wale ambao wanakabiliwa matatizo.  Kwa njia hii, kwa matendo ya huruma, upendo wa Kristo,  utaweza kuonekana  duniani. 

Papa Francisko alieleza na kuongeza kwamba , katika Injili, Yesu analenga hasa kutuonyesha sisi huruma ya Mungu Baba  katika kutusamehe, ili nasi tuweze kuwasamehe wengine. Kama sisi tunavyoupokea msamaha kutoka kwa Mungu bure vivyo hivyo hata sisi tusamehe wengine bila kudai malipo au shinikizo, lakini katika njia ya uongofu na kutembea pamoja kwa amani. Na kwamba Yesu anatualika pia kusamehe kwa  uhuru wote , kama sisi tunavyopokewa kwa uhuru kamili pia sisi kwa uhuru kamili  tuwasamehe wengine, maana kwa kufanya hivyo, tunapata uwezo wa kuwajulisha wengine kwamba huruma ya Mungu haina mipaka wana miisho.

 

 








All the contents on this site are copyrighted ©.