2016-08-02 14:36:00

Papa aunda tume kushughulia Ushemasi wa Wanawake Ndani ya Kanisa


Baba Mtakatifu Francisko baada ya kusali na kutafakari kwa kina kuhusu Ushemasi wa wanawake ndani ya Kanisa Katoliki baada ya kukutana na kuzungumza na wajumbe wa mkutano mkuu wa wakuu wa Mashirika ya Kitawa na Kazi za kitume hapo tarehe 12 Mei 2016 ameamua kuunda tume ya maalum itakatochambua Ushemasi wa Wanawake ndani ya Kanisa Katoliki. Upembuzi huu utazingatia kwa namna ya pekee Kanisa la mwanzo. Wajumbe wa Tume ya Ushemasi wa Wanawake watakuwa chini ya Askofu mkuu Luis Francisko Ladaria Ferer, Katibu mkuu wa Baraza la Kipapa la Mafundisho Tanzu ya Kanisa.

Tume hii itakuwa na wajumbe kumi na wawili kati yao kuna watawa na maajalimu wanawake kutoka vyuo mbali mbali duniani watakaosaidiana na Wakleri kutoka katika masuala ya kitaalimungu, Mababa wa Kanisa, Elimu ya Kanisa, Mafundisho Tanzu ya Kanisa, Tume ya Taalimungu Kimataifa, Taalimungu ya maisha ya kiroho. Wajumbe hawa baada ya kukamilisha kazi yao, wataiwasilisha kwa Baba Mtakatifu kwa ajili ya maamuzi baadaye!

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP. S.

Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.








All the contents on this site are copyrighted ©.