Kwa ajili ya Maadhimisho ya kutimia miaka 35 ya uwepo wa Kituo cha kupokea na kuhudumia wakimbizi cha Astalli cha Shirika la Wajesuit , Baba Mtakatifu Francisko kwa njia ya Video, ametoa ujumbe wake kwa ajili ya maadhimisho haya yaliyofikia kilele chake katika Ukumbi wa Michezo wa Argentina wa hapa Roma, ambako pia kulitolewa Ripoti ya mwaka 2016 ya Kituo , juu ya hali ya watu waliotafuta hifadhi kama wakimbizi katika kituo hicho.
Papa Francisko katika ujumbe wake , amepongeza uwepo wa huduma hii kwa kipindi cha miaka 35, na kwa namna ya kipekee akionyesha kufurahi kwamba, kwa mwaka huu inafanyika sambamba na Jubilee ya Mwaka Mtakatifu wa Huruma. Hivyo ameutaja kuwa ni wakati wa kipekee wa kutembea pamoja kama jamii moja , ni jambo jema na inapendeza.Kwa mtazamo huo, Papa amehimiza umuhimu wa kuendeleza huduma hii kwa pamoja tena kwa ushupavu zaidi kutimiza Neno katika Injili ya Matayo: "Nilikuwa mgeni, mkanikaribisha" (Mt 25,35).
Kwenye ujumbe huu, Papa amekumbusha kwamba, kila mkimbizi anayebisha hodi mlangoni ana sura ya Mungu, ni mwili wa Kristo. Na kwamba, maisha ya wakimbizi yaliyojaa uchungu na matumaini, humkumbusha kila mmoja wetu kwamba sisi wote ni wasafari katika uso wa dunia hii, tulipokelewa kwa ukarimu na wengine tena bila kustahili. Papa ameeleza na kuongeza kila aliye mgeni, mtu aliyekimbia nchi yake ana sababu za kufanya hivyo,ingawa zinaweza kuwa sababu mbalimbali, kama ukandamizaji, vita, majanga asilia, uchafuzi wa mazingira na kuenea kwa jangwa, au kuenea kwa dhulumu dhidi ya rasilimali za dunia, kila mmoja wa wakimbizi hao ana sababu zake. Hivyo ni ndugu wanao hitaji tugawane nao mahitaji ya lazima kama chakula, makazi na huduma za maisha.
Papa ameonyesha kujali kwamba, kwa mara nyingi tunashindwa kutimiza hayo. Mara nyingi kutokana na sababu au za kutojali mahangaiko na mateso ya wengine au kwa kuhofia kwamba wataleta mabadiliko katika maisha na wawazo yetu. Hivyo Wakimbizi wanachukuliwa kama mzigo, tatizo na gharama, badala ya kupokewa kama zawadi.
Papa hivyo amekitaja kituo hiki cha Astalli kama ni shahidi wa Jinsi Mungu mwenye neema na huruma, anavyojua jinsi ya kugeuka uovu na dhuluma kuwa mazuri kwa kila mtu. Pia ameshukuru uwepo wa kituo hiki kama daraja la kuwaunganisha pamoja na watu mbali, kikitoa uwezekano wa kukutanisha tamaduni na dini mbalimbali , kama njia ya mpya ya ya kugundua ubinadamu kwa watu wote.
Ameendelea kurejea maneno ya Injili. “ mlinikaribisha” ,” nilikuwa mgeni mkanikaribisha”, kwa kurudia kukitaja Kituo cha Astalli kuwa mfano thabiti hai, kila siku katika kuwapokea wahitaji , akikumbuka mwanzilishi wake Padre Arrupe, kwa wamimbizi wa Asia. Na hivyo akaitumia nafasi hiyo, kuwashukuru wote , wake kwa waume, walei na watawa na wafanyakazi wa kujitolea walioungana katika njia hii yakutoa msaada bila kuchoka wala kuongopa.
Papa amewahimiza waendelee na moyo huu. Na kwamb a miaka 35 waliyopitisha na ionekane kama ni mwanzo tu wa huduma yao hii muhimu , kama njia pekee ya kurudisha matumaini kwa binadamu aliyemizwa na mateso na dhiki. Amewaomba waendelee kuwa msaada kwa jamii kuweza kuisikia sauti inayoita ya wakimbizi. Waendelee kutembea kwa ujasiri pamoja nao, kuongozana na wakimbizi, hadi hapo watakapoweza kuitambua njia inayoweza kuwarejesha katika amani,kwa kutambua ubaya wa vita.
All the contents on this site are copyrighted ©. |