2016-04-19 15:20:00

Mkristo wa kweli si Yatima maana anaye Baba wa Mbinguni


Mkristo asiyevutwa na upendo wa Mungu kwa njia ya Yesu Kristo, ni Mkristo anayeishi katika hali ya upweke wa yatima asiyekuwa na Baba . Ni mafundisho ya Baba Mtakatifu Francisko , wakati wa Ibada ya Misa, mapema  Jumanne,  katika kanisa dogo la Mtakatifu Marta . Papa ameuzungumzia moyo mgumu usiotaka kuelewa ujumbe wa Mungu, akitaja kwamba huko ni kukosa imani.Moyo wenye kusikiliza sauti ya Mungu, ni moyo wenye  kujifunua wazi kwa Mungu, na huisikia habari njema  inayoletwa na  Roho Mtakatifu.

Papa alieleza akilenga  katika jinsi binadamu anavyokuwa na moyo mgumu katika kusadiki, moyo wenye kudai  kwanza ishara na miujiza na bado huendelea kuhoji  iwapo ni kweli ni  Kristo anayetenda  miujiza. Alilenga katika somo la Injili ambamo Mafarisayo na Waandishi  wanamwuliza Yesu swali, hadi lini ataendelea kuwaweka  katika hali ya kusubiri ,  walitaka kufahamu mara moja kama kweli ndiye Kristo, wanayemsubiri. Hawakusadiki miujiza na ishara nyingi zilifofanywa na Yesu, bado walitaka awaambie  waziwazi kama ndiye Masiya.  Papa ameeleza swali hili la Waandishi na Mafarisayo la mara kwa mara, kimsingi linatokana na upofu wa moyo.  Upofu  wa imani. Yesu  aliwaambia waliokuwa wakimhoji kwamba hawawezi kuelewa kwa sababu hawakuamini. Na bila imani wanakuwa si sehemu ya wanakondoo wake, si sehemu ya Kundi la Mungu maana kuwa mmoja wa Kundi la Mungu inahitaji kuwa  moyo  ulio wazi , moyo wenye kusikia sauti ya Mungu na kuitikia wito. 

Na kwamba Kondoo wake  huisikia sauti yake, naye anawajua na humfuata. Na yeye huwapatia  uzima wa milele; nao hawatapotea milele, na hakuna mtu awezaye  kuwapokonya kutoka mkono wake. Kondoo hao  wamejifunza kumfuata Yesu na wanaamini. Na ni  Baba yake aliye mkuu ndiye aliyempa , na ni yeye Baba anayewapa moyo unaowavutia kwa Yesu.

Papa alieleza na kuitaja mioyo migumu ya  waandishi na Mafarisayo, ambao waliona Yesu akitenda lakini hawakuamini kama yeye ndiye Masiha , waliona kama vile Yesu anafanya mchezo wa kuigiza hadi kumpeleka katika njia ya Kalvario. Papa alieleza na kusema hata baada ya ufufuko waliendelea kutosadiki, wakisema maaskari walinda kaburi  walilala usinginzi na kisha wanafunzi wake wakauiba mwili wa Kristo. Walikataa kusadiki ushuhuda wa kusisimua uliotolewa  juu ya Yesu Kufufuka . Walibaki katika maisha yao ya giza kama yatima wapweke, wakikataa  kusadiki neno la Baba.

Licha ya kuwa walimu wa sheria mioyo yao ilibaki imefungwa katika mambo yao ya kale,  kwa kweli, walikuwa yatima, kwa sababu hawakuwa na uhusiano na Baba. Walizungumzia, ndiyo, wahenga wao ,   Abraham, Isaka  na wengine lakini mioyo yao ikiwa mbali na ukweli unaoelezwa  na Kristo kuwa ndiye Masiya waliyekuwa wakimsubiri.  Mioyoni mwao waliendelea kuishi katika hali ya yatima.

Papa alikamisha homilía yake kwa kutoa mwaliko kwamba kuwa mfuasi wa Yesu, ni lazima sisi wenyewe tuvutiwe na Upendo wa Baba katika kumwelekea Yesu. Ameitaja  sala ya  unyenyekevu wa mwana, tunayotakiwa sisi kuitoa , kumwomba Baba atupeleke kwa mwana, kwa kumtuma  Roho Mtakatifu  mwenye uwezo wa  kufungua mioyo na kutuongoza  kwa Yesu . Mkristo asiyevutwa na upendo wa Baba,  huyo huishi maisha ya kiyatima. Ambapo Wakristo wa kweli si yatima maana wanaye Baba. 








All the contents on this site are copyrighted ©.