2016-04-16 15:14:00

Wahamiaji 12 kutoka Lesvos kuhudumiwa na Papa Francisko!


Katika maadhimisho ya Mwaka Mtakatifu wa Jubilei ya huruma ya Mungu, waamini wanahamasishwa kuhakikisha kwamba, wanamwilisha katika maisha na vipaumbele vyao matendo ya huruma: kiroho na kimwili, kama kielelezo makini cha imani tendaji! Baba Mtakatifu Francisko baada ya kuhitimisha hija yake ya kitume Kisiwani Lesvos, nchini Ugiriki, Jumamosi, tarehe 16 Aprili 2016 ameambatana pamoja na watu kumi na wawili na kati yao kuna watoto wadogo sita, ambao watapewa hifadhi na kuhudumiwa na Vatican kama kielelezo makini cha matendo ya huruma kwa maskini!

Padre Federico Lombardi, msemaji mkuu wa Vatican anafafanua kwamba, hawa ni wakimbizi na wahamiaji waliokuwa kwenye kambi za wakimbizi huko Lesvos kabla ya makubaliano yaliyofikiwa kati ya Jumuiya ya Ulaya na Uturuki. Kielelezo hiki cha upendo na mshikamano kutoka kwa Baba Mtakatifu Francisko kimetekelezwa na Sekretarieti kuu ya Vatican kwa kufuata mchakato na taratibu zote zinazohitajika kati ya Serikali ya Ugiriki na Italia, ili wakimbizi na wahamiaji hawa weweze kupata hifadhi nchini Italia kwa kuhudumiwa na Vatican yenyewe! Huduma ya kwanza kwa familia hizi inatolewa na Jumuiya ya Mtakatifu Egidio yenye makao yake makuu mjini Roma.

Na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.

Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.








All the contents on this site are copyrighted ©.